Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kutoa mchango wangu kwenye bajeti kuu ya nchi yetu.

Nianze kwa kumpongeza kwa dhati kabisa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri anayofanya ya kujenga na kuimarisha uchumi wa nchi yetu. Kipekee nimpongeze Mheshimiwa Waziri kaka yangu Dkt. Mwigulu, kazi yake ni njema, yeye na timu yake na niseme tu kwamba hatuna mashaka na uwezo wako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nichangie bajeti kwenye maeneo mchache. Eneo la kwanza ni kwenye hali ya makusanyo. Nimeona kwenye ukurasa wa 19 Mheshimiwa Waziri ameeleza hali ya makusanyo. Na kwa ninavyomfahamu alivyo bingwa wa namba ameweka fedha tu hakuweka asilimia. Mimi nikajipa kazi ya kwenda kwenye asilimia nikajikuta makusanyo ambayo tumeshakusanya mpaka anawasilisha taarifa ile Aprili, 2023 tuko kwenye asilimia 78. Niwapongeze kwa kazi hii nzuri lakini kwa mahitaji ya nchi yetu bado tuna haja ya kuongeza nguvu zaidi kwenye makusanyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, niwaombe Waheshimiwa Wabunge na Watanzania tuungane na Mheshimiwa Waziri. Suala la kusisitiza umuhimu wa ulipaji wa kodi sio suala la Waziri peke yake na wala si suala la Serikali peke yake. Hakuna nchi inayoweza kuwezeshwa bila watu kulipa kodi. Sisi kama viongozi tuungane pamoja kuhamasisgha ulipaji wa kodi kwenye nchi yetu ili tuendelee kutengeneza maendeleo ya kwetu sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yako maeneo mawili naomba nitoe ushauri, eneo la kwanza nimeona kwenye ukurasa wa 107 Mheshimiwa Waziri ameeleza kuanza kutoza shilingi 20 kwa kilo ya saruji inayotoka nje na inayozalishwa ndani. Ukisema shilingi ishirini maana yake kwa mfuko mmoja unakwenda kuongeza shilingi elfu moja. Leo hii hatujaongeza tozo hii bei ya saruji ni kubwa na malalamiko ya watu wetu ni mengi, maeneo mengi watu wanashindwa kufanya kazi ya ujenzi kwa sababu ya bei hii ya saruji. Tukaliangalie vizuri jambo hili, sioni kama litakwenda kuwasaidia sana Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia watu watafanya ulinganisho, unakwenda kutoza shilingi 20 kwa kilo moja ya saruji lakini wakati huo huo kwenye ukurasa wa 97 unakwenda kutoa msamaha wa VAT kwenye gaming odds na kwenye gaming software. Jana amesema vizuri sana ndugu yangu Mheshimiwa Jerry Silaa, jambo hili si zuri. Tunaomba mkaliangalie vizuri kama Serikali na ikiwezekana kwenye finance bill marekebisho yafanyike ili tuliondoe jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ambalo nataka nichangie ni kwenye upatikanaji wa fedha za kigeni. Mheshimiwa Waziri amesema vizuri kwenye ukurasa wa 50 na 51 wa hotuba yake, kwamba nchi nyingi ziliingia kwenye changamoto ya kuwa na upungufu wa fedha za kigeni ikiwemo nchi yetu. Lakini umeeleza jitihada na hatua ambazo Serikali inafanya ikiwemo kuongeza uzalishaji ili tupunguze kuagiza bidhaa kutoka nje, ninawapongeza wa hatua hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwenye eneo hili, pamoja na hii ya kuongeza uzalishaji na kupunguza kuagiza bidhaa liko eneo ambalo tunaweza kutengeneza fedha nyingi za kigeni kwenye nchi yetu, na si eneo lingine, ni kwenye eneo la sekta yetu ya utalii. Sekta ya utalii inaweza kutuingizia fedha nyingi za kigeni kwenye nchi yetu. Na bahati nzuri amesema mwenyewe kwenye hotuba yake. Niungane naye kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuamua kufanya kazi ya kutangaza utalii wa nchi yetu kwa vitendo. Matokeo ya Royal Tour yameonekana, amesema mwenyewe kwamba tumeongeza fedha za kigeni kutoka dola 1,310,000 mwaka 2021 hadi dola 2,527,000.7 mwaka 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ninayoiona hapa, tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa Royal Tour, tunampongeza kwa maneno au tunampongeza kwa dhati ya mioyo yetu na kwa kazi ambazo tunazifanya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo changamoto; mwaka 2019 wakati wa kupitisha bajeti ya mwaka 2019/2020 tulifanya marekebisho kwenye Finance Bill. Marekebisho tuliyoyafanya tukaleta utaratibu mpya wa taasisi za uhifadhi kukusanya fedha, akina TANAPA, Ngorongoro kwamba fedha zao zikusanywe moja kwa moja kwenye mfuko mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuna shida na jambo hilo limefanyika lakini tangu tumeanza jambo hili changamoto zimekuwa ni nyingi. Tukaja na mawazo ndani ya Bunge hili kwamba pamoja na makusanyo haya kwenda moja kwa moja tuhakikishe tunaweka retention kwa taasisi hizi ili ziweze kujiendesha, shughuli za uhifadhi ni za gharama, zina dharula nyingi, wazo hilo halikusikilizwa. Wakati wa kupitisha bajeti ya mwaka 2021/2022 kamati ya bajeti ikashauri kama retention imeshindikana basi angalau muweze kutoa hali ya miezi miwili au mitatu mbele kama OC kwa taasisi hizi, mpaka leo imeshindikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tunapozungumza leo, hali ya taasisi za uhifadhi ni mbaya. Tunakwenda kwenye high season hawana fedha, miradi ya barabara imesimama, OC haziendi. Hiyo high season tunakwenda nayo namna gani, tunatengenezaje fedha? Tunaomba Mheshimiwa Waziri walete utaratibu mpya, tutoe retention kwa taasisi hizi. Wakishindwa retention basi OC za taasisi hizi wa akina TANAPA, Ngorongoro, TAWA zitoke mapema, ikiwezekana awe na advance ya miezi mitatu. Tembo wanasumbua wananchi taasisi hazina fedha, majangili wanarudi kwa kasi taasisi hazina fedha lazima tuziwezeshe taasisi hizi ziweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho Mheshimiwa Waziri akija atuambie, wakati wa bajeti ya Wizara ya Maliasili tulisema lakini hatukupata majibu. tumekwama wapi kwenye zoezi la kuhamisha watu kwa hiari kwenye hifadhi ya Ngorongoro? Zaidi ya miezi saba zoezi limesimama. Kama unataka kunusuru hifadhi ile ni lazima tuhakikishe, tunahamisha watu na watu wamekubali, wamejiandikisha, wamesimamisha shughuli zao tumekwama wapi? Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha atuambie... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana naunga mkono hoja.