Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa hii, Nimshukuru pia Mwenyezi Mungu, nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri. Pamoja na yote namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kile kitendo ambacho amekifanya kutukwamua sisi watu wa Mtwara kutokana na barabara yetu ya kiuchumi ya Mnivata – Tandahimba – Newala – Masasi. Mheshimiwa Rais amepeleka zaidi ya bilioni 234 kwa ajili ya barabara ile ambayo ilikuwa kwenye ilani kwa muda mrefu na haitekelezwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye bajeti, niipongeze sana Wizara kwa wasilisho zuri, lakini zipo changamoto ndogo ndogo ambazo zinatakiwa kuangaliwa. Kwenye ile bajeti kuna aya inayozungumzia suala la sekta za uzalishaji ikiwemo kilimo. Kilimo ni uti wa mgongo; na tunatambua kabisa watu wetu wengi wanaishi vijijini wanategemea kilimo kwa ajili ya kustawisha maisha yao ya kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto ambayo inawakumba wakulima wetu. Kwa mfano, ukienda mikoa ile ambayo inalima zao la korosho kumetokea na utaratibu mwaka huu wa kufanya sensa wa miche ya mikorosho. Wakulima wametekeleza agizo hilo, lakini sasa wakati wa kutoa zile pembejo ambao unafuatana na zile sensa, mambo yamekuwa magumu kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo baadhi ya kata ambazo vijiji vyake, kwa mfano, ukienda Kata ya Maputi ambayo ipo Jimbo la Newala Vijijini, kati ya vijiji sita vya kata ile, vijiji vitatu havimo kwenye mpango. Vile vile, ukienda Kata ya Mnyambe, Kata ya Malatu, hizo zote zina–miss kuwemo kwenye utaratibu wa kupata pembejeo kwa sababu ya mfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Wizara kuangalia utaratibu mzuri ambao wakulima watapata pembejeo kwa wakati kwa sababu msimu wa upuliziaji wa zao la korosho ni sasa. Inapotokea mkulima hayupo kwenda kurekebisha inachukua muda mrefu sana. Kwa hiyo, tutapishana na wakati. Badala ya wakati wa upuliziaji, upuliziaji utapita, kwa hiyo yale manufaa ambayo tumeyapanga kwamba tunataka kukusanya mazao, tutakosa kupata kile ambacho tulikuwa tunakitarajia. Kwa hiyo, niombe sana hilo lifanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye upande wa elimu; kuna mambo mengi. Tumeona sasa hivi namna ambavyo Serikali inapeleka fedha nyingi kujenga madarasa. Tunashukuru na kwa sasa madarasa mengi yanakwenda yakiwa na madawati yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna changamoto ambayo imejitokeza kwenye yale madarasa ya zamani. Madarasa mengi ya zamani watoto wanakaa chini, hakuna madawati. Ili umwandae vizuri mwanafunzi lazima akae sehemu nzuri ya kujifunza na kujifundishia. Mwanafunzi anapokosa dawati, hawezi kujifunza vile ambavyo tulikuwa tunatarajia. Kwa hiyo niombe, mwaka 2026 kulikuwa na mkakati ambao ulizilazimisha halmashauri kuhakikisha kwamba madawati yanapatikana. Baada ya mkakati ule hapakuwa tena na shinikizo lingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu halmashauri inakumbana na changamoto nyingi kutokana na mambo ya kifedha, lakini kama hatutaweka msisitizo, wanafunzi wataendelea kupata shida ya namna ya tendo la kujifunza na kujifundishia kwa sababu wengi wanakaa chini, tunawasababishia afya zao kuteteleka kwa sababu anajikunja tangu asubuhi mpaka jioni, zoezi la mwaka mzima, tutawasababishia wanafunzi wetu vibyongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana, tunayo misitu yetu ambayo inasimamiwa na watu wa Maliasili, tuone namna ambayo tunaweza kupata magogo tukapeleka yakatengenezwa madawati ambayo yatakwenda kusaidia shule zetu. Nafahamu upo utaratibu, lakini watu wa Wizara ya Maliasili na Utalii wakae pamoja na watu wa TAMISEMI, waone namna ambavyo changamoto hii inaweza kwenda kutatuliwa ili wanafunzi wetu wapate sehemu ya kukalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasafirisha magogo kwenda kuyauza nje, sawa tunapata fedha lakini je, afya na ustawi wa wananchi wetu na watoto wetu tunauweka wapi? Tunapotengeneza mazingira ambayo yatasababisha magonjwa, tunazalisha kitu kingine ambapo tutakwenda kutafuta fedha kwa ajili ya kuwatibu, kitu ambacho kingekuwa solved kama wanafunzi hawa wangekaa katika mazingira mazuri ya kusomea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sio hivyo tu, kuna suala la usafi binafsi. Tunafahamu hali za wananchi wetu ni ngumu. Mtoto anakaa chini, asubuhi anaondoka yuko vizuri, msafi, lakini anaporudi jioni ana vumbi amechafuka kwa sababu amekaa chini tangu asubuhi mpaka jioni. Kwa hiyo, kuna vitu vingi vinatengenezwa hapo, lakini source inakuwa ni ukosefu wa madawati katika madarasa yetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)