Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Rahim, kwa ruzuku ya uhai na afya ambayo imeniwezesha kuja kutoa mchango wangu. Aidha, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kutoa mchango na mimi nianze kwanza kwa kumshukuru kwa dhati kabisa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake madhubuti lakini kwa kasi kubwa ya maendeleo ambayo tunayaona katika nchi yetu, ikiwa ni pamoja na kuendeleza miradi ya kielelezo na miradi mikubwa lakini pia ustawi wa wananchi unazidi kukua katika nyanja zote chini ya uongozi wake mahiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumpongeza kwa dhati kabisa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Waziri wa Fedha, pamoja na Naibu Waziri, Mheshimiwa Hamad Hassan Chande, Katibu Mkuu Dkt. Dr. Natu El-Maamry Mwamba na Naibu Makatibu Wakuu kwa bajeti hii mwanana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwamba katika bajeti hii Jimbo la Kilosa katika miradi mikubwa tumewekwa, ikiwa ni pamoja na kujenga barabara ya kutoka Kilosa kwenda Mikumi pia kuanza upembuzi yakinifu na usanifu wa daraja kubwa la Mto Mkondoa. Ni imani yangu kwamba fedha hii itapatikana katika mwaka huu wa fedha na ni miradi hiyo kuanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchangia kuhusu umuhimu wa sekta ya nyuki na hasa katika mazao yake ikwemo asali katika kukuza uchumi wa nchi yetu na kuipatia nchi yetu fedha za kigeni. Tanzania ni nchi ya pili kwa kuzalisha asali nyingi katika Bara la Afrika, nchi ya kwanza ni Ethiopia, Tanzania ni ya pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ndiye supplier mkubwa wa asali na mazao ya asali kama vile Nta kwenye soko la Umoja wa Ulaya kutoka Afrika (European union). Inakadiriwa kuwa Tanzania inauza nje wastani wa tani 770 za asali na tani 283 za Nta kwa mwaka. Aidha, inakadiriwa kuwa sekta ya ufugaji nyuki na mauzo yake yanaleta wastani wa dola za Kimarekani 5,182,126 kwa mwaka katika miaka minane iliyopita kila mwaka hizo fedha ziliingia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta hii inaajiri na kuhusisha takribani watu milioni mbili waishio vijijini katika maeneo mbalimbali hususani Tabora, Singida, Katavi, Morogoro kule Kilosa. Mfano kule Singida kuna Kijiji cha Nyuki na Jiji la Nyuki. Pia Kilosa Kata za Maguha na meneo Unone katika Kata ya Ludewa wote wanafanya shughuli hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta hii ina uwezo mkubwa wa kukua na kuongeza mapato ya nchi kwa kuuza asali na nta na mazao mengine nje ya nchi. Tunaweza tukauza vumbi yaani pollen, tunaweza tunaweza tukauza royal jelly yaani maziwa ya nyuki. Hata hivyo, sekta hii inakabiliwa na changamoto nyingi hasa inapokuja katika kuuza asali na nta nje ya nchi. Kikwazo kikubwa au changamoto kubwa ni urasimu mkubwa na fomu nyingi na nyaraka nyingi ambazo wale wanaouza asali nje ya nchi wanatakiwa kuzijaza na kila unapojaza iwe ni nyaraka au ni fomu lazima wanatozwa, wanalipa tozo. Kwa hiyo, eneo hili pia lina tozo nyingi takribani 30 katika hatua mbalimbali za kuhakikisha kwamba wanaweza kuuza asali nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Tanzania wanajaza fomu 31 ukilinganisha na nyaraka sita Rwanda, matokeo yake asali yetu nyingi msimu huu wa kurina asali ukifika maeneo kama Itigi, utakuta malori mengi yanakusanya asali inakwenda Kenya na ikifika Kenya itauzwa nje kwa jina la Kenya, moja ya sababu kubwa ni urasimu huu na tozo nyingi ambazo zimewekwa katika sekta hii hasa kwa wale ambao wanataka kuuza asali yao nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mtu anayetaka kusafirisha asali nje anatakiwa aende kwenye taasisi nyingi na akienda kwenye taasisi hizo mifumo yao haisomani. Kwa hiyo, anajikuta taarifa ambazo ametoa kwenye Taasisi moja inabidi taarifa hizohizo azirudie kwenye Taasisi nyingine. Anatakiwa aende kwa Wakala wa Misitu (TFS), anatakiwa aende TCCIA apate Certificate of Origin, anatakiwa aende Veterinary ili ahakikishiwe kwamba nyuki waliotoa hiyo asali walikuwa ni salama, anatakiwa aende Tanzania Atomic Energy Commission, anatakiwa aende TASAC anatakiwa aende TRA, anatakiwa aende TBS, anatakiwa aende TPA na hao wote mifumo yao haisomani na matokeo yake tunapoteza ufanisi wa kupeleka asali nyingi nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyohuyo anayepeleka asali nje anajikuta anatakiwa kupata aina hiyohiyo ya cheti au ruhusu au payment kutoka sehemu mbili tofauti lakini juu ya jambo hilohilo. Kwa mfano, anatakiwa aende veterinary ili apewe sanitary certificate ya kutoa ushahidi kwamba nyuki aliyetoa asali hiyo alikuwa salama, halafu anatakiwa aende Wakala wa Misitu ili apate sanitary certificate ya kuonesha kwamba asali hiyo ni salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapendekeza fomu hizi zipitiwe upya tukilinganisha na za wenzetu nchi ya Rwanda, Kenya na Uganda ili tuwe na ufanisi na tija zaidi katika kupeleka mazao haya ya asali. Mimi nina uhakikia kabisa tukiboresha mifumo yetu, tukitoa hamasa kwa watu mbalimbali na sekta binafsi kununua, kuchakata na kuuza asali nje, tunao uwezo kwa mwaka kuingiza dola milioni 20 kutokana na asali na mazao ya asali kama nta na royal jelly. Wote tunafahamu kabisa royal jelly ina bei kubwa sana na faida kubwa tuliyonayo sisi maeneo yetu ambayo tunafuga nyuki maeneo haya mengi hayana mazao yanayotumia viuatilifu au mbolea, maana yake asali hii ni organic na ina uwezo wa kuwa na bei kubwa katika masoko ya Ulaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mapendekezo yangu Mheshimiwa Waziri tupitie tena zile fomu kutoka 30 tuzipunguze ikiwezekana zifike tisa kama ilivyo kwa Rwanda. Pia tupunguze tozo katika sekta hii, nashauri pia tutoe fedha ya kutosha ya kuwahamasisha wafugaji wa nyuki katika maeneo mbalimbali, Tabora, Singida yote Itigi na Manyoni lakini Kilosa na maeneo mengine yoyote yale ili wananchi wetu waweze kuwa na mizinga ya kisasa ya kufuga nyuki lakini yenye ubora na tukusanye asali hiyo na tuichakate na kuuza nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili naomba kupongeza Serikali kwa hatua ya kuondoa ushuru wa bidhaa unaotozwa kwa magari yanayotumia nishati ya umeme ambayo yamo katika hotuba ya bajeti ukurasa wa 107 na 108. Kwa mujibu wa ripoti ya Africa E-Mobility Alliance inaonyesha kuwa Tanzania kuna electric vehicles, yaani kwa maana ya magari, pikipiki, bajaji skuta 5000 na sisi ndiyo tunaoongoza katika eneo hili la Afrika Mashariki kwa kuwa na hizi electric vehicles nyingi, pia tunazo kampuni karibuni kumi ambazo zinaagiza aina hii ya magari. Kwa hiyo, kuondoa ushuru wa bidhaa katika eneo hili utaongeza kuingizwa nchini kwa magari mengi, pikipiki nyingi na skuta nyingi ambazo zinatumia umeme badala ya mafuta na hivyo kutunza mazingira lakini pia kupunguza matumizi ya fedha za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili Tanzania tumefika mbali na mambo haya wakati mwingine hatuyasemi, sisi ndiyo nchi pekee katika Afrika Mashariki ambayo tunayo kampuni ambayo sasa inabadili magari haya ya mafuta kuwa magari yanayotumia umeme. Kampuni hiyo ni Kampuni ya Hanspaul ipo pale Arusha na wao wanashirikiana na kampuni ya Ufaransa na Kampuni ya Gardy Electronics, hawa sasa wanabadili magari yanayotumia mafuta kwenda kuwa katika mfumo wa umeme na wamejenga vituo vya kuongeza umeme vinavyotumia solar katika sehemu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo langu ni kuwa jitihada hii ipewe musukumo ili tuweze kuanza kutengeneza magari ya umeme sisi wenyewe ndani ya nchi yetu. Tumejaliwa kuwa na madini yote ya kimkakati ambayo yanahitajika katika magari ya umeme Nickel, Cobalt, Lithium pamoja na Graphite, kwa hiyo, hatua hii ni muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza pia Chuo cha Ufundi cha Arusha kipewe fedha zaidi, kwa sababu ndiyo chuo ambacho kimeanza kufundisha mafundi wa kuhudumia magari haya ya umeme, kuyatenegeneza magari haya ya umeme na wakitoka katika kuhudumia magari haya ya umeme na kuyatengeneza magari haya ya umeme waende sasa kwenye kuunda magari ya umeme, pikipiki za umeme, skuta za umeme na vitu vinavyotumia umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayasema haya kwa sababu mara nyingi Watanzania tunafanya vitu vikubwa sana lakini ni wazito wa kuvitangaza, ni wazito wa kuvieleza. Kwa hiyo, niwapongeze sana Hanspaul Group, na wengine, pia Chuo cha Ufundi Arusha kuingia katika sekta hii ya magari ya umeme. Dunia ya sasa inahama kutoka kwenye magari ya mafuta kwenda kwenye magari ya umeme na magari yanayotumia Gesi asilia. Tanzania tuwe ndiyo nchi inayofanya mambo yote hayo kwa kasi kubwa sana. Nchi za jirani zinakuja kubadili magari yao ya mafuta kuwa magari ya umeme kwa ajili ya utalii na duniani zinatangazwa kwamba magari yale yametengenezwa katika nchi zao kumbe magari hayo yote yamekuja Arusha yamebadilishwa na kuwa magari ya umeme lakini dunia inafahamu kwamba magari hayo yametoka kwenye nchi hizo. Kwa hiyo, ninapendekeza tuseme kwa sauti kubwa kwamba shughuli hii inafanywa Tanzania pia tuwape hawa wanaofanya kazi hii motisha mbalimbali ikiwa ni pamoja na hii hatua ya kufuta au kuondoa huu ushuru wa bidhaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ambalo ningependa kulizungumzia ambalo pia tuwekeze katika hilo, tuwekeze katika haki miliki ya umahususi wa kijiografia yaani geographical indications. Maeneo hayo tuyatumie kuuza bidhaa ambazo zinatoka katika maeneo hayo. Moja ya mazao ambayo tunaweza tukayatangaza kwa bidii kubwa sana ni Kakao. Kakao ya Kyela ina ubora mkubwa sana duniani na inatumika kuchanganya na kakao hafifu kutoka nchi nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuja na kakao hii, kakao hii inauzwa Ufaransa, ili kuonesha kwamba Kakao hii ya Tanzania ina thamani kubwa ndiyo maana wanaonyesha kwamba asilimia 75 ya kakao katika chocolate hii imetoka Tanzania, imetoka Tanzania kwa sababu ina ubora mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiishie tu katika hayo pia tuanze kutangaza kutumia umahususi wa kijiografia wa mazao mengine ya kilimo ili yapate bei ya juu. Kwa mfano, Kahawa ya Mbinga ndiyo kahawa inayolimwa bila kutumia mbolea ni organic. Kahawa ya Manyovu na hivi vyote vitatusaidia siyo tu kupata fedha ya kigeni lakini kuitangaza nchi yetu kwamba ina bidhaa za ubora wa hali juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchele wa Kyela, mchele wa Kilombero na sasa kuhusu Mvinyo wa Dodoma. Mvinyo wa Dodoma una ubora mkubwa sana duniani, ndiyo maana mvinyo wa Dodoma unachukuliwa na nchi nyingine kwenda kuongeza ubora wa mivinyo yao ambayo ni hafifu. Kwa hiyo, ni wakati sasa wa nchi yetu kuwekeza pia katika maeneo hayo ambayo yanaonekana siyo muhimu lakini duniani ni muhimu sana, hatimiliki ya mazao yote yenye umahsusi wa kijiografia yaani geographical indicators. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja katika bajeti hii mwanana na bora sana. (Makofi)