Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kunipa nafasi na mimi nichangie asubuhi ya leo. Awali ya yote naomba nichukue nafasi hii kuwashukuru Wabunge wenzangu wa CCM kwa kunichagua kwa kura nyingi kuwa Katibu wao. Nawaahidi kwamba kazi naifanya vizuri kwa weledi na ustadi mkubwa, sitawaangusha!
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nizungumzie barabara yangu moja iliyoko Jimboni kwangu. Barabara hii inaanzia Kanazi kwenda hadi Katolo, hii barabara ni kubwa sana, ni barabara ya TANROAD, ni barabara ya TANROAD, kubwa, lakini ina hali mbaya sana! TANROAD ni kama vile wameitelekeza, hawaitengenezi mara kwa mara, hawaiweki lami hata kama si lami angalau wangekuwa wanaitunza inakuwa inapitika vizuri mwaka mzima! Mara nyingi inakuwa na mashimo makubwa sana na ni barabara ambayo inaunganisha wilaya tatu, Wilaya ya Bukoba yenyewe, Wilaya ya Misenyi na Wilaya ya Muleba sasa barabara kama hii ina umuhimu wa pekee, inahudumia Kata 19, watu karibu 300,000. Kata zenyewe ni Kata ya Kemondo, Kata ya Katerero, Kata ya Igwela…
MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Kata ya Mikoni, kikomelo, Kishogo, Kashalu, Kibimbili, Kaibanja, Katolo, Kyamulaile, Mugajwale, Luhunga, Chaitoke, Izimbya, Kibilizi, Lukoma, Lubale na Butelankuzi, bila barabara hii hawa watu hawafiki Bukoba Mjini na wa mjini hawafiki kwenye Kata hizi, bila barabara hii. Sasa barabara hii ina umuhimu wa kipekee, kule tunalima mazao mengi sana, kahawa nyingi sana, ndizi nyingi sana, lakini ina hali mbaya sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, jana Mheshimiwa Savelina Mwijage aliongelea barabara hii ndiyo yenye daraja la Kalebe, daraja bovu kweli kweli ni hatari pale! Sasa naomba sana Mheshimiwa Waziri barabara hii ipewe fedha, kwenye kitabu hiki cha hotuba ya Waziri haimo na ni barabara kama nilivyosema ya TANROAD.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kuna barabara nyingine ambayo inaanzia Mjini Bukoba kwenda Kabango Bay, kilometa 42 barabara ya mpaka, inakwenda Uganda, nimeisema mara nyingi hapa Bungeni, lakini kwenye kitabu hiki imepangiwa shilingi milioni 200, barabara ya mpaka, barabara ya usalama, barabara ya ulinzi, milioni 200 ni fedha kidogo sana! Tumeisema muda mrefu sana. Hata Mheshimiwa Shein alipokuwa Makamu wa Rais aliwahi kuisemea kwamba ijengwe kwa kiwango, miaka karibu 10 iliyopita hadi leo haijaguswa! Naomba na yenyewe ipewe fedha, itengenezwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo lingine kubwa, pale Halmashauri ya Bukoba Vijijini nilisema hapa Bungeni, wiki mbili zilizopita kulikuwa na ubadhirifu wa fedha za barabara. Fedha ya Road fund, fedha ya Mfuko wa Jimbo na fedha ya ombi maalum, fedha nyingi karibu bilioni moja. Nikapiga kelele kule kwenye Halmashauri, Mkuu wa Mkoa aliyekuwepo ambaye sasa amehamishwa akaanzisha utaratibu wa kuwashughulikia hawa watu, akaunda Tume wakakamatwa, nashangaa mpaka leo hawajapelekwa Mahakamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, niliandika barua kwa CAG kwamba apeleke Tume ya Wakaguzi wakague fedha hii imeliwa namna gani, fedha nyingi namna hii. Cha kusikitisha, CAG amenijibu kwamba hana fedha ya kwenda kufanya kazi hii! Unamwambia fedha imeibiwa anasema sina fedha ya kwenda kukagua wizi, nasema inasikitisha sana! Anasema aliyeomba ndiye agharamie, sasa naangalia namna gani nitapata fedha ya kuwalipia watu wa CAG waende kule wakague wizi huu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mbaya zaidi, nimesema jambo kubwa, kutokana na ubadhirifu huu watu wa Road Fund wamekataa kutoa fedha kwenye barabara za vijijini nyingine ambazo inabidi wazihudumie kwamba hadi fedha hii irudishwe ndiyo watoe fedha! Sasa anayeadhibiwa siyo aliyekula zile fedha, ni wananchi wa Bukoba Vijijini. Mkurugenzi amehamishwa, Engineer amehamishwa ingawa nasikia wamekamatwa na wenyewe sasa hivi, lakini anayeadhibiwa ambaye sasa hivi hana pa kupita, barabara zimekongoroka zote zimekuwa mashimo ni Wwnanchi ambao hawana hatia! Naomba sana jambo hili liangaliwe kwa kina kwa nini uwaadhibu wananchi ambao hawana hatia, uwaache wenye hatia hata leo hawajapelekwa Mahakamani, wanawaangalia tu, wako tu wanaangalia, hili kwa kweli ni jambo ambalo linasikitisha sana!
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini, nizungumzie SUMATRA, SUMATRA imeagiza kwamba mabasi ya shule yapakwe rangi ya njano, nitangaze maslahi mimi ni mliki wa shule na nina mabasi hayo mengi. Sasa wanaagiza kwamba yapigwe rangi ya njano, jambo hili ni la kuchekesha, ni kichekesho na si jipya waliwahi kusema huko nyuma tukamwambia Waziri aliyekuwepo, Mheshimiwa Nundu akazuia jambo hili, leo tena wamelirudisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, basi moja la Costa kulipaka rangi ya njano si chini ya milioni tatu, uchomelee chomelee kwanza kwenye kutu upige rangi ya njano, three milion shilings unazipata wapi, analipa mzazi? Unafanya shule ziwe na gharama kubwa bila sababu, haina faida yoyote kwa mzazi kwa shule wala kwa mwanafunzi! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, huu ni uhuni wa hali ya juu sana, yamkini kuna mtu ana rangi zake kule, amenunua rangi nyingi Dubai au Japan anataka aziuze kwa nguvu. Jambo hili halikubaliki, lazima Mheshimiwa Waziri atoe maelezo kuhusu jambo hili kwa nini tunafanyiwa jambo ambalo ni la uovu kama hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie na uwanja wa ndege wa Mkajunguti ambao uko Kagera, Wilaya ya Misenyi. Uwanja huu umezungumziwa siku nyingi sana. Michoro imefanyika, fidia imeandaliwa, lakini haikutolewa, uwanja huu ujengwe, kwenye bajeti hii haumo. Uwanja huu unaunganisha nchi tano, Uganda, Rwanda, Burundi, Tanzania na Congo, uko katikati, ni wa kimkakati kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ndege zikitoka Latin America zitatua pale zitaweka mafuta zitaenda Asia, zikitoka Afrika ya Kusini zitatua pale zitaenda Ulaya. Ni uwanja wa kimkakati kabisa, basi ujengwe! Fedha itengwe ipatikane kwenye bajeti na kazi iendelee.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishie hapo, nakushukuru sana!