Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ya Bajeti Kuu ya Serikali ambayo iko mbele yetu. Nitumie nafasi hii kumshukuru Mungu kwa kunipa afya njema ya kuweza kusimama mbele ya Bunge lako. Lakini nitumie nafasi hii kumshukuru na kumpa pongezi za dhati Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo ameifanya katika kupaisha uchumi wa Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii vilevile kukupongeza Mheshimiwa Waziri Ndugu yangu Dkt. Mwigulu, Naibu Mheshimiwa Chande lakini watendaji wa Wizara na taasisi kupitia Wizara ya Fedha kwa kazi kubwa ambayo mnaifanya ya kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kuweza kukamilisha maono yake kwa Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu nianze na pongezi. Napenda nitume pongezi za dhati kwa Serikali kwa kuendelea kupeleka fedha kwenye Halmashauri ya Morogoro Vijijini na hususani katika Jimbo langu kwenye upande wa afya tumepokea fedha karibu shilingi milioni 200 kwa ajili ya kujenga zahanati Gwata, Kisemo, Mgata na Rukulunge katika Halmashauri ya Morogoro Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata vilevile fedha shilingi milioni 500 kwa ajili ya vifaatiba kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya na kwenye zahanati. Nimepata fedha lakini vifaa tiba vya shilingi milioni 751 kwenye halmashauri yetu kwenye Hospitali ya Wilaya. Tuna kila sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Rais na hata wale watu wanaosema tunaendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais hakuna sababu yule mtu ambaye anaejua ukipata una kila sababu ya kushukuru na kupongeza. Kwa hiyo, sisi tutaendelea kupongeza kwa sababu Mama anafanya kazi nzuri lakini na wewe Mheshimiwa Dkt. Mwigulu unafanya kazi nzuri ya kutafuta fedha kwa kumshauri Mama na kuzileta kwenye halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru vilevile kuna suala la ajira tumepokea ajira karibu watumishi 33 kwenye halmashauri yetu upande wa kada ya afya. Tuna kila sababu ya kupongeza katika hilo. Ombi langu kwako Mheshimiwa Waziri na kwenye Serikali ni kwamba pamoja na kazi hii nzuri iliyofanyika kwenye upande wa afya bado tuna changamoto. Changamoto ya kwanza ni gari la wagonjwa kwenye Hospitali ya Wilaya lakini vilevile kwenye Kituo cha Afya cha Tutume. Tungeomba Mheshimiwa Waziri katika mapitio pitio yako angalia uwezekano wa kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna changamoto za gari za hospitali kwenye idara ya afya kwa ajili ya kuweza kufuatilia shughuli za uendeshaji wa shughuli za afya lakini vilevile generator kwenye Hospitali ya Wilaya hatuna. Lakini vile vile kwenye vituo sita hivi ambavyo nimevizungumza hatuna generator, tungeomba tusaidiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile majengo ya OPD kwenye Kituo cha Afya cha Kisemo, Kisaki pamoja na Kinongo. Tunakuomba Mheshimiwa Waziri utuangalie. Nitumie nafasi hii vilevile kutoa pongezi za dhati kwenye suala la elimu. Ndani ya kipindi hiki kifupi juzi tu tumeletewa shilingi bilioni tatu ambayo itajenga Shule Maalum ya Wasichana kwenye Kata ya Bwakila Chini ambayo itaanzia O level hadi A level. Tuna kila sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Rais lakini tukupongeze wewe Waziri unayefanya kazi kwa dhati katika kufanya kazi hii. Lakini tulipata juzi tena shilingi bilioni 750 kwa ajili ya Mradi wa Boost katika kuendeleza shule zile ambazo zilikuwa kongwe. Tuna kila sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Waziri lakini vilevile kumpongeza Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Serikali kwa upande wa elimu pamoja na walimu kupatikana tuendelee kupata walimu wengine. Bado tuna upungufu wa walimu kwenye maeneo hasa ya pembezoni kwenye halmashauri yetu, kata za milimani Singisa, Kisaki na kwenye maeneo mengine. Tunakuomba Mheshimiwa Waziri uone jinsi gani ya kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi kukupongeza sana Mheshimiwa Waziri kwenye hili suala la kufuta ada kwenye vyuo vya ufundi. Nimetokea kwenye vyuo vya ufundi, nimeajiriwa railway, nilikwenda kusoma Railway Training College mpaka nimemaliza nilipofikia hapa. Sasa kwa kufuta ada kwenye vyuo vya ufundi ambavyo umevitaja DIT, MUST na Arusha Tech tunaenda kutengeneza wataalamu wengi ambao watakwenda kulisaidia Taifa lakini ombi langu kwako hebu tuviangalie Chuo cha NIT nacho tunakokwenda. Tuangalie Chuo cha Reli vilevile tunakokwenda. Kule nako tunaweza tukasaidia sana vijana wetu wakaweza kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa Waziri kwenye suala la kilimo niipongeze Serikali kwa kazi kubwa ambayo imeifanya kwenye kuwekeza kwenye kilimo lakini ombi langu kwa Serikali kutokana na tabianchi inavyoendelea uharibifu bado kutegemea kilimo cha mvua hatutaweza kufanikisha katika dhana ya kupata chakula kingi katika nchi kwa faida ya chakula cha ndani na cha kuuza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe tuangalie kwenye suala la uwekezaji kwenye kilimo cha umwagiliaji. Katika yale mabonde mwaka jana nimechangia kwenye Bajeti kuna mabonde pale Kilosa, kuna mabonde hapa tukitoka hapa kuna Kibaigwa, kuna suala la Mto Dumila lakini hata Ruvu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tuangalie tukachimbe mabwawa, watu wafanye kilimo cha umwagiliaji ili tutoke kwenye lile lakini kwenye suala la kilimo niombe na nadhani Ndugu yangu Bashe yupo. Mwaka huu Morogoro tumebahatika kupata ufuta mwingi sana lakini umeingizwa kwenye suala la stakabadhi ghalani wakati watu hawajajiandaa lakini vile vile hata hiyo Serikali haijajiandaa. Imeleta taharuki na changamoto kubwa. Niwaombe Wizara ya Kilimo hebu kwa mwaka huu tuacheni wananchi walime ufuta wao na wauzie watu wanaowataka ili waondokane na adha ambazo wanazipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye suala lingine Mheshimiwa Waziri nikuombe. Kuna suala la CSR la Bwawa la Mwalimu Nyerere. Nakumbuka nilikufuata uliniambia tumtafute Waziri mwenye dhamana hatukuweza kumpata lakini juzi wakati nachangia nilichangia majibu waliyonipa hayakutupa matumaini watu wa Rufiji na watu wa Morogoro Vijijini. Nikuombe wakati unachangia; je, sisi watu wa Morogoro Vijijini ambao na Rufiji ambao ndiyo tunafanya kazi kubwa ya uhifadhi lakini tunafanya kazi kubwa ya kuangalia huo mradi. Je, tunapata nini? Tuelewe ili twende tukapange na tukuleteeni kwamba tusaidieni hiki na hiki na hiki wananchi wetu wapate kufaidika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee vilevile kuzungumza kwenye suala la kodi. Mimi ni mfanyabiashara, siyo mkubwa sana lakini ni mfanyabiashara. Bado tuna changamoto kwenye sheria zetu za kodi. Mheshimiwa Waziri unazungumzia suala kwamba hakuna kufunga maduka, hakuna kufunga account, Mheshimiwa Rais alisema jambo hili. Mimi ni mhanga, mwaka huu nimefungiwa account bila sababu yoyote ya msingi. Niangalie na nikuombe lazima tukae na wafanyabiashara. Kaa na wafanyabiashara katika Sekta mbalimbali wa Kilimo, wafanyabiashara wa mahoteli, wafanyabiashara wakandarasi tuone jinsi gani tunaweza tukachangia wote kwa pamoja tutokaje hapa tulipo ili watu waweze kulipa kodi bila shuruti lakini kodi ambayo itaenda kuleta maendeleo makubwa kwa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii habari ya kusema tumefunga, hao watu wa TRA kupitia sheria ambazo zimetunga ukifika wanakwambia hayo ni mambo ya siasa na kwa kusema mambo ya siasa kwa kauli yako Waziri maana yake wanakufedhehesha wewe. Lakini vilevile Rais akisema kwamba hili lisifanyike watu wakifanya ukienda wanakwambia ni mambo ya kisiasa vilevile tunamvunga nguvu Rais wetu lakini tunamchonganisha Rais na wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri kama kuna suala linawapa mandate watu wa TRA kufunga hizi maduka tuletee hapa tuangalie jinsi gani ya kuifanya tuondoe ili hizi kauli mnazozitoa ziende sambamba na hayo ambayo tunayataka kwenye Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nikuombe kwenye suala la kupandisha cement. Naamini kabisa tutaenda kupeleka maisha magumu kwa Watanzania. Kuna maeneo mengi ya kuangalia na bahati nzuri kuna hili ambalo limezungumzwa ETS. Nilishauri siku za nyuma lilipoanza lilikuwa katika maeneo madogo lakini sasa hivi kama alivyotoka hata Engineer Chiwelesa kuzungumza limekwenda kwenye cement liende kwenye nondo, liende kwenye maeneo mengi tukajihakikishe kwamba kile kinachozalishwa kule je, kinafanana na kile tunachopewa? Tukiweza kujiridhisha matokeo yake nini? Tutaenda kuendelea kukusanya kodi nyingi ambazo upo uwezekano tusiende tukaingiza gharama kwenye cement twende kuingiza gharama kwenye nondo ambazo tutaenda kuwatilia wananchi wetu washindwe kujenga majengo mazuri vilevile washindwe kufanya mambo mengine ya kisiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kwenye suala la kodi nakuomba sana, nakuomba sana bado kuna changamoto. Umezungumza mwenyewe wafanyabiashara ni wachache lakini mahitaji ya Serikali ni makubwa. Bado tunaweza kwenda ndani zaidi kutafuta wafanyabiashara wengine ambao watasaidia hawa ambao wamejiandikisha ambao wana mzigo mkubwa na unawaumiza wanashindwa kwenda mbele na mwisho kama tutaendelea hivi hata hawa tuliokuwa nao milioni nne tunaweza tukawapoteza na Serikali ikaingia katika wakati mgumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)