Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyenijalia afya njema na kusimama ndani ya Bunge lako hili Tukufu, lakini nichukue fursa hii kuwaombea Wabunge wote afya njema ndani ya Bunge lako hili, Mwenyezi Mungu awajaliwe afya njema pamoja na akili timamu katika kuisimamia Serikali yetu hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru sana wananchi wa Jimbo langu, lakini pia nichukue fursa hii kuwakumbuka wazee wetu waliotangulia, nikianza na Bibi yetu Bibi Titi Mohamed ambaye alikuwa Mbunge wa kwanza katika Jimbo la Rufiji, ambalo leo hii historia yake inapotea, hata pale tunapoona sherehe za kumkumbuka mama Bibi Titi Mohamed amekuwa akisahaulika, nichukue fursa hii kumkumbuka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwakumbuke wazee kina mzee Ngauka, mzee Mkali pamoja na Marehemu mzee Mbonde, Mwenyezi Mungu aiweke roho yake mahali pema peponi! (Makofi)
Mheshimiwa Naib Spika, nimkumbuke pia Profesa Idrissa Mtulia ambaye ni Babu yangu huyu, aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Rufiji na Dkt. Seif Seleiman Rashid ambaye pia alikuwa Mbunge wa Rufiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona nizungumze hili kwa kuwa Rufiji imetoa mchango mkubwa sana katika Taifa hili letu. Asilimia zaidi ya 60 ya wapigania uhuru wa nchi hii wote walitoka Rufiji na kama hakutoka Rufiji basi atakuwa na asili ya Rufiji, hata wale Wamakonde watakuwa ni asili tu ya Rufiji. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona niliseme hili kwa kuwa Rufiji imekuwa ikisahaulika sana kwa muda mrefu sana! Nimesikiliza kwa umakini sana hotuba za Mawaziri wetu wote hata waliopita. Hotuba hata ya Waziri wetu wa Kilimo ameshindwa kuizungumzia Rufiji. Mimi sielewi unapozungumzia kilimo ukashindwa kuisema Rufiji, Bonde la Mto Rufiji, lakini pia hata Mawaziri wengine hata nikija pale kwa Maliasili na Utalii tunafahamu atasoma hotuba yake siku ya Jumanne, lakini nafahamu matatizo makubwa ya kero za wananchi wa Jimbo la Rufiji na inawezekana siku ya Jumanne nisiwepo, niseme tu, Wizara ya Maliasili na Utalii iliweza ku-introduce kodi ya kitanda ambayo ni gharama kubwa kila mwananchi wa Rufiji analazimika kulipa shilingi 130, 000/= kwa kitanda anachokilalia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona niliseme hilo japokuwa nitachangia kwa maandishi. Nirudi katika hotuba yetu hii ya siku ya leo ya Wizara hii. Nimesikiliza kwa makini hotuba ya wenzetu Wapinzani baadhi ya waliokuwa wakichangia, lakini pia mchango alioutoa Mheshimiwa Keissy, siku ya jana.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba Mheshimiwa Kessy amezungumza mambo mengi sana ya msingi ambayo, niseme Mheshimiwa Waziri ayachukuwe kwa kina sana, ule mgawanyo wa pato hili la Taifa, mgawanyo huu uende vyema na sisi wananchi wa Jimbo la Rufiji tuweze kunufaika na pato hili la Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wapo wengine katika Bunge lako hili Tukufu wameomba wanunuliwe ndege, wengine wameomba meli, wengine wajengewe reli; tunafahamu siku Mheshimiwa Waziri atakapokuja kujibu hoja zake hapa atajikita sana kwenye reli na ununuzi wa ndege, lakini atasahau yale maeneo ambayo yanahakikisha Chama cha Mapinduzi kinaingia madarakani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo langu la Rufiji limemchagua Dkt. John Pombe Magufuli kwa imani kubwa sana wakiamini kwamba kero hizi za kwao walizonazo toka Rufiji inazaliwa mwaka 1890, kabla ya 1900 Rufiji ilikuwepo. Pia kwa kutambua kwamba Rufiji ni kubwa kuliko Mkoa wa Kilimanjaro, Rufiji peke yake, Rufiji hii ambayo ina shule moja tu ya Sekondari kidato cha tano na sita, basi Mheshimiwa Waziri wa Miundombinu atusaidie sisi Rufiji na nazungumza kwa uchungu kabisa, tuweze kupata angalau barabara ambazo zitawasaidia wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mgawanyo huu wa Pato la Taifa nawaomba Waheshimiwa Mawaziri wawe wanazingatia mchango wa Taifa katika Pato la Taifa. Sisi Rufiji tunayo Selous ambayo ni Hifadhi ya Taifa kubwa kabisa Afrika, lakini pia tunayo misitu, katika pato la Taifa Rufiji tunachangia zaidi ya asilimia 19. Mchango huu mkubwa wa Pato la Taifa tunaochangia Rufiji, mchango huu wote unakwenda kujenga barabara na kutengeneza reli maeneo mengine ya nchi na sisi Rufiji ambao tulikuwepo hata kabla ya uhuru, tunapoizungumzia Rufiji tunazungumzia wakati wa mkoloni ambao tulikuwa na wilaya sita nchini, Wilaya ya Rufiji ilikuwepo. Hakuna asiyefahamu boma lile la Utete, hakuna asiyefahamu katika historia ya nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nina imani kubwa sana na Waziri wangu huyu, Profesa, sina ubavu wala uwezo wa kumpinga, kwa sababu kwanza yeye ni Profesa na uwezo wake umejidhihirisha baada ya Mheshimiwa Rais kumteua kwa nafasi aliyopata leo hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, yeye atakuwa shahidi mara ngapi nimemfuata kwa ajili ya kuzungumzia barabara zetu za Rufiji, atakuwa shahidi mkubwa. Nimemfuata mara kadhaa, lakini si kwake tu, nimekwenda mpaka kwa Makamu wa Rais kwa ahadi yake ya tarehe 9 Septemba, 2015 aliyoahidi ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami, barabara ya Nyamwage kuelekea Utete. Rufiji ndiyo wilaya pekee ambayo haiunganishwi na lami japokuwa Rufiji ina zaidi ya miaka 55 katika nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana Serikali itufikirie, kipindi hiki kwa kweli tunawaomba sana. Ahadi za Marais, tukianzia ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete wakati anakwenda kule Selous alipita barabara ya Mwaseni- Mloka, Ikwiriri kwenda Mwaseni, Mloka kule, akielea Selous, barabara hii ni mbovu sana. Leo hii kutoka Mwaseni - Mloka kufika Ikwiriri unatumia zaidi ya saa kumi kwa kilometa 90 peke yake, lakini kutoka Nyamwage kuelekea Utete, kilometa 33 tunatumia zaidi ya saa tano. Hii ni aibu, aibu kubwa sana kwa Serikali yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana basi Serikali yetu iweze kutufikiria. Ombi maalum kabisa kwake Mheshimiwa Waziri, nina imani na yeye kama nilivyosema, atufikirie barabara zetu hizi ambazo Marais wetu walituahidi. Barabara ya Nyamwage kuelekea Utete kwenye Makao Makuu ya Halmashauri yetu, namwomba sana Mheshimiwa Waziri akisimama atueleze anafanya nini kuhusiana na hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukurasa wa 257 wa kitabu chake umezungumzia barabara hii itakarabatiwa tu ukarabati wa kawaida. Sasa tunashindwa kuelewa, kwa sababu katika kikao chetu cha mkoa cha barabara Mhandisi wa Mkoa alituahidi kwamba barabara hii itarekebishwa kwa kiwango cha lami, lakini nashangaa katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri amezungumzia ukarabati mdogo. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri suala hili atujibu wakati anajibu hoja zake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini barabara ya kutoka Ikwiriri kuelekea Mwaseni, Mloka ni kilio kikubwa. Huku ndiko Serikali inakusanya zaidi ya asilimia 19 ya Pato la Taifa, watalii leo hii wanatumia zaidi ya saa kumi, tunawa-discourage. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa barabara hii ni barabara ya TANROADS sasa wafikirie ijengwe kwa kiwango cha lami. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa muda wangu ni mdogo, nikumbushie barabara ya Bungu kuelekea Nyamisati kwa ndugu yangu, Mwenyekiti wa Wandengereko, Mheshimiwa Ally Seif Ungando na barabara ya Kibiti kuelekea Ruaruke pamoja na suala zima la minara ya simu, nimwombe sana…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda wako umekwisha!
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.