Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Niungane na wenzangu kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, vijana wenzangu, kwa uteuzi wa kuongoza Wizara hii. Tunawafahamu vizuri, tufahamu uwezo wao na tuna matumaini makubwa sana na wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda niende harakaharaka, muda ukiruhusu nitakuwa na mambo matatu. Jambo la kwanza ni kilimo cha umwagiliaji. Kilimo cha Umwagiliaji kinaongeza tija, kinaongeza eneo la kulima na kinaongeza vipindi na misimu ya kulima. Ninazo takwimu kuanzia mwaka 2015 mpaka sasa tumeongeza hekta ngapi kwenye kilimo cha umwagiliaji, lakini kwa sababu ya muda sitaki kuzitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona malengo ya Mheshimiwa Waziri, ameweka malengo ya kuongeza hekta elfu tisini na tano na tano kwenye mwaka wa fedha huu unaokuja. Jambo hili litawezekana kama mambo makubwa mawili yatafanyika. Jambo la kwanza ni lazima kama nchi tukubali kutafuta fedha zaidi nje ya bajeti zetu tulizokuwanazo kwa ajili kugharamia kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni kuhakikisha tunasimamia na kutekeleza miradi mikubwa itakayo-cover eneo kubwa. Kwenye eneo hili niwe specific kabisa kwenye eneo la Bwawa la Mkomazi. Bonde la Mto Mkomazi na Bwawa la Mkomazi. Tumesema sana, tumefanya vikao vingi, ni ahadi ya chama chetu kwenye uchaguzi na Mheshimiwa Waziri alitoa maelekezo kwa watu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji. Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha nataka kusikia nini kinakwenda kufanyika na wakati gani kuhusu Bwawa la Mkomazi, pamoja na urafiki na kazi anayoifanya nisiposikia kitu cha kuwaridhisha watu wa Korogwe, nitakuja kushika Shilingi.

Mheshimiwa Spika, siyo tu Mkomazi kuna Bwawa la Kwamkumbo tunayo ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mheshimiwa Waziri ameshatoa maelekezo hatujaona kinachoendelea, tumekwama wapi? Ukija kwenye majumuisho nitapenda kujua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ili niweze kuzungumza kwenye suala zima la zao la mkonge, Mheshimiwa Waziri nimeona umesema malengo yetu ni kutoka tani 36,698 kwenda mpaka tani 60,000 kwenye mwaka wa fedha unaokuja, naomba kukumbusha jambo, hatuwezi kufikia haya malengo kama hatutaendelea kuwajali na kuwathamini wakulima wadogo wadogo, mchango wa wakulima wadogo ni mkubwa sana kwenye zao la mkonge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2019 kwenye tani tulizozalisha, mchango wa wakulima wadogo ni asilimia 24, mwaka 2020 ni asilimia 30 na mwaka 2021 ni asilimia 37. Lakini wakulima wanachangamoto, Mheshimiwa Waziri tumehamasisha, Waziri Mkuu amefanyakazi nzuri, lakini bado kuna changamoto kubwa kwa wakulima wadogo wadogo. Mashine za kuchakata mkonge imekuwa ni changamoto. Tumeleta kampuni kule Sisalana imechukua mitambo kuwa ya katani wanawazalishia wakulima wetu. Gharama ya uchakataji ni kubwa sana inawaumiza wakulima wetu, lakini mitambo ile ni mibovu inafanya tunapata mkonge mchache lakini pia hata ubora wa mkonge wenyewe unapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema sana, ninashauri mambo matatu kwenye jambo hili. Jambo la kwanza, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo Naibu wako alikuja Korogwe, Bodi ya Mkonge waliunda Kamati ya kupitia zile gharama, wameenda wamekwama wanasema subiri Mkuu wa Mkoa aseme. Bodi ya Mkonge ndiyo yenye dhamana ya kusimamia mkonge kwenye nchi hii. Tunawaomba toeni tamko juu ya bei halali inayofaa kulipwa na wakulima wetu wadogo wa mkonge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili Mheshimiwa Waziri tununue mashine, Bodi na Wizara nunueni mashine za kuchakata mkonge muwape wakulima wetu. Jambo la tatu Mheshimiwa Waziri bado wakulima wetu wanamadai na Kampuni ya Katani. Mlichukua mitambo ya katani akapewa NSSF akaenda Kampuni ya Sisalana, lakini ukweli ni kwamba kwa mujibu wa Waraka Na. 31 wa 2005 wa Baraza la Mawaziri, Katani alipaswa kutengeneza kampuni ili wakulima wetu wadogo wadogo wawe hisa kwenye kampuni hizo kwenye zile AMCOS tulizokuwa nazo, mambo hayo hayakufanyika. Leo umechukua mitambo umempa Sisalana anawahujumu wananchi wetu, anawahujumu wakulima wetu. Mashine ambayo ilitakiwa izalishe ichakate mita 100 kwa siku leo wanachakata mita 60. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini cha kufanya Mheshimiwa Waziri, Wizara ya Kilimo ninyi ndiyo wasimamizi wa sera kwenye eneo la kilimo. Kaeni na Msajili wa Hazina tupitie ule mchakato ulivyokuwa, tutoe hizi mashine kwa Sisalana tuwape wananchi, tuwape wakulima wadogo kwenye AMCOS zao wasimamie. Pia mnaweza mkatusaidia kuwa wasimamizi wa mazungumzo kati ya AMCOS zetu na Benki ili wakulima wetu kupitia AMCOS zao wakopeshwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri hakuna hatari kubwa kwenye zao la mkonge kama kutenganisha mchakataji na mzalishaji. Mchakataji akiwa hana uchungu na mazao ya mkulima atamkwamisha, na ndicho kinachofanyika, kampuni hii kwa sasa inawahujumu wananchi wetu. Mheshimiwa Naibu Waziri umeenda umewaambia wachimbe kisima wachakate mkonge mwingi kwa siku, watoe mkonge ulio bora Zaidi, mpaka leo hakuna kilichofanyika. Sisi ndiyo tuna dhamana kusimamia mkonge Wizara ya Kilimo, tusiwaachie watu wakacheza na mkonge wa wakulima wetu, watawakatisha tamaa, wataacha kulima, tutarudi nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni upande wa chai.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mbunge, muda wako umemalizika.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unipe dakika moja nimalizie. Bodi ya Chai isiwasahau wakulima wa Usambara kama inavyofanya kwa wakulima wa Mafinga na Nyanda za Juu Kusini, kiwanda cha Mponde tumekisubiri kwa muda mrefu ni wakati sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)