Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa hii fursa ya kuchangia hii Wizara muhimu. Nami napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu na Wizara hii kwa kutuletea bajeti nzuri sana ya kilimo. Hii bajeti ya kilimo kwa kuiangalia kwa juu juu, itatuletea mapinduzi makubwa ya uchumi wetu hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nami napenda kuishukuru Kamati ya Kilimo, imetoa maangalizo mazuri sana ambayo naomba Mheshimiwa Waziri, ayafuatilie kwa ukaribu, la sivyo bajeti hii asipoangalia hayo maangalizo ya Kamati, inaweza isitekelezeke kama anavyotarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala ambalo Kamati imeelekeza, ni kwa jinsi ya wataalam waliopo kilimo inaona kama hawajitoshelezi, lakini naona kama wataalam wanajitosheleza. Unapokuwa na transformational budget kama hii, inabidi lazima ubadilishe na culture ya watu utakaowakuta. Kwa vile kwa muda mrefu walikuwa hawajawahi kuona fedha nyingi kiasi hiki, sasa unapowapelekea fedha nyingi kiasi hiki, watashindwa hata namna ya kuzitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi fedha ukiziangalia zinatokana na mkopo wa IMF ambao wana discipline kubwa katika matumizi ya fedha zao. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, nina imani na taaluma yake kwa kiasi kikubwa, hebu aangalie kwa namna gani haya matumizi ya fedha za IMF ambazo ni za uhakika zitatuletea fedha nyingi zaidi? Naamini Sekretarieti yake, Katibu Mkuu wake, ni mtu mwenye uwezo mkubwa sana; hebu mtumie vizuri, nina imani kuwa Wizara hii itabadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mbolea siyo ruzuku tu, mbolea ni namna ya uagizaji wa mbolea. Mwelekeo wa bei za mbolea sasa hivi haueleweki. Shilingi bilioni 150 zinaweza kusaidia, lakini hizi zitawapa matumaini wananchi. Mimi naona bado tunahitaji kuufumua muundo mzima wa mbolea. Mbolea haiagizwi kama kama tunavyokwenda sokoni, mbolea inatumia taasisi ambazo ninaimani Waziri anazifahamu kuna mambo yanaitwa futures, hygiene na kadhalika na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ndiyo ambazo zinaweza kutusaidia kununua mbolea kwa wakati muafaka, wakati bei ni sahihi kwa nchi yetu. Kwa kuwatumia wafanyabiashara watanunua kwa bei kubwa watatuuzia kwa bei kubwa. Kwa hiyo, nchi ichukue jukumu la kuagiza mbolea yenyewe, aidha kwa kuwadhamini hao wafanyabiashara, tununue katika kipindi ambacho Brazil na zile nchi ambazo zinatumia mbolea kwa kiasi kikubwa haziagizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, jukumu la kuagiza mbolea lisiwe kwa walanguzi wafanyabiashara. Hawa ni traders, hawawezi kukusaidia. Hebu chukua jukumu wewe mwenyewe, weka miongozo, lakini hiyo iendane pamoja vile vile Shukuma kuwepo na Sheria ya Kilimo. Transformation kama hizi huwezi ukazitekeleza bila ya kuwa na sheria sahihi ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hiyo, napenda kwenye kuongeza thamani za mazao; zao la pareto. Pareto inaweza kutusaidia kwenye viuadudu. Kwa kutumia kiwanda chetu cha Kibaha, pareto inaweza kusaidia kuzalisha viuatilifu. Sasa ni kwa nini tusiwe na mpango kabambe wa taasisi zetu za utafiti ifanyike haraka ili tuweze kukisaidia kile kiwanda kiweze kuzalisha viuatilifu pamoja na mbolea? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo jambo ni muhimu sana, litatusaidia, kwa vile pareto inayolimwa Tanzania, wengi hawajui, tunaongoza Afrika, ni wa pili duniani. Hii inaweza kutusaidia kutuletea fedha nyingi za kigeni na kuwasaidia wananchi ambao kwa sasa hivi wanalanguliwa sana kwa bei ndogo ya pareto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Bunge hili, kwa hiyo, naomba kwa sababu Bunge hili tuliamini na tunaamini kuwa ni Bunge ambalo litajikita kwenye kilimo, kwa hiyo, tunaomba huo mwongozo ambao ulikuwa umeutoa tuendelee nao tuhakikishe kuwa kilimo ndiyo kinabebwa na Bunge lako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)