Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa. Nami nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri. Nimemsikiliza na nimesoma kurasa zote 277 za hotuba yake, zimesheheni mambo muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza wakulima kote nchini, nawapongeza wakulima wangu wa Jimbo la Kisesa kwa kazi nzuri sana wanayofanya ya uzalishaji mali. Katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri amezungumza suala la kuanzisha Benki ya Taifa ya Ushirika. Hili suala la kuanzisha Benki ya Ushirika ya Taifa halina tija yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, watu wa ushirika hawajakosa mahali pa kukopa. Tuna Taasisi nyingi sana za mikopo ambazo zinaweza zikatoa mikopo kwa washirika. Tunayo Benki ya Kilimo, unakwenda kuanzisha benki nyingine ya nini? Benki yenyewe hii ya Kilimo bado hatujaiimarisha, tunaenda tena kuanzisha benki nyingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, wanazungumzia urahisi wa kupata mikopo. Masharti na vigezo vinasimamiwa na Benki Kuu. Kwa hiyo, suala la kusema kwamba eti washirika wakianzisha benki watapata mikopo kiurahisi ni nadharia, kwa sababu vigezo na masharti yote yanasimamiwa na Benki Kuu na yatakuwa ni yale yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, majukumu ya Vyama vya Ushirika ni mengi sana. Tumewapa jukumu la kufufua viwanda vilivyotelekezwa, tumewapa jukumu la kuwasaidia wakulima kupata mbegu bora, kuwasaidia wakulima waweze kupata huduma ya afya ya udongo, kupambana na magonjwa. Wanaliacha hili jukumu la msingi, wanakimbilia kuanzisha benki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao mfano, kuna Benki hapa zilianzishwa kwa mbwembwe nyingi, matokeo yake benki hizo tumeenda kupata hasara kubwa, benki zikafungwa, fedha za Watanzania zimo humo ndani. Kwa mfano Bank (M) iko wapi? Twiga Bank iko wapi? Benki ya Wanawake iko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, makosa hayo hayo, leo tunaenda kuanzisha Benki tena za mfano huo huo. Hata kidonda hiki bado hakijapona, Benki Kuu bado wanalitatua hili tatizo, hatujamaliza kulitatua, leo Waziri unaenda kuruhusu kuanzisha Benki nyingine, kwa ajili ya jambo gani? Benki Kuu nanyi mmekubali kuanzisha hii Benki wakati tunayo Benki ya Kilimo? Duplication hizi ni za kazi gani? Mnataka kuzichukua fedha za wananchi ambazo zingeweza kuwasaidia wananchi, ziende zikagawanywe huko kujenga majengo na mambo mengine wakati wakulima wana shida kubwa hapa! (Makofi)

Benki Kuu na ninyi mmekubali kuanzisha hii benki ilhali tunayo ya kilimo, duplications hizi za kazi gani? Mnataka kuzichukua fedha za wananchi ambazo zingeweza kuwasaidia wananchi ziende zikagawanwe huko kujenga majengo na mambo mengine ilhali wakulima wana shida kubwa hapa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni suala la mbolea. Wenzangu wanezungumza hapa, upandishaji wa bei za mbolea, narudia kusema mfumuko bei za mbolea zetu ni wa kutengenezwa. Waziri amekuja hapa ameshindwa kusema utatuzi wa bei za mbolea zilizotengenezwa. Moja, kwa wafanyabiashara wametengeneza, bei za mbolea zimepanda, urea hapa imetoka 50,000/= imeenda mpaka 110,000/= mpaka 150,000/= kwa maeneo mengine, lakini ukiangalia kwa undani hizi bei zimetengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ninasema, na hasa takwimu ambazo wanazo Serikali waziangalie. Kwa mfano Waziri anaposema kwamba, bei za mbolea zimepanda katika soko la dunia, bei ya urea imepanda kutoka dola 251 mpaka dola 1,214; kwa maana hiyo katika soko la dunia unataka kutuambia kwamba, bei ya mbolea ya urea kwa kilo 50 imepanda kutoka 28,000 mpaka 139,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama hizo ndizo takwimu mnazotuambia, kama katika soko la dunia mbolea ya urea ya kilo 50 inauzwa kwa bei ya 139,000/= utaiuza kwa bei gani hapa? Kwa hiyo, hizo takwimu zenyewe sijui ni source gani na sijui kama Serikali wanajiridhisha na takwimu hizo, zinatoka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la tatu ni Serikali na Wizara hii ya kilimo; waliamua kufuta utaratibu wa bulk procurement system. Badala ya kutatua matatizo yaliyokuwemo kwenye bulk procurement system wakaenda kuiondoa bulk procurement system ili kufanikisha njama za wafanyabiashara wachache waliokuwa wamepanga njama za kuja kuwaongezea wakulima bei za mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Waziri atuambie toka walivyoondoa mfumo wa bulk procurement system mwaka 2021, Juni, bei za mbolea zilianza kupanda palepale, hata kabla ya vita ya Ukraine ambayo ndiyo inayozungumzwa hapa bei za mbolea zilianza kupanda kwa kasi bila usimamizi. Kwa hiyo kuna usimamizi dhaifu katika jambo hili. Na kwa uthibitisho hata Mheshimiwa Waziri mwenyewe anakiri kwamba wale TFRA walipoenda kufanya ukaguzi walienda kukuta mambo ya ajabu, wakakuta mbolea zinauzwa zikiwa hazijasajiliwa, hazina vibali, ziko wazi na vilevile kulikuwa na zilizokuwa na uzito wa chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote yanathibitisha kwamba, hakuna usimamizi thabiti katika hili eneo la mbolea na kusababisha wananchi kwenda kuuziwa mbolea kwa bei kubwa sana. Halafu sasa mfumo tumeutengeneza sisi wenyewe nab ado kuna nchi jirani zetu ambao wanauza mbolea chini. Wanatumia Bandari ya Dar-es-Salaam, wanasafirisha mbolea na bado wanaenda kuuza huko kwa bei ya chini; kwa nini sisi hapa bei yetu hapa iko juu? Na haya yote tunayokubali na tumeyatengeneza sisi wenyewe Wizara ya Kilimo halafu tunatoka tunasema kwamba, eti bei ya mbolea tunamfumuko wa bei ya mbolea kwa bei ambazo tumezitengeneza wenyewe? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Muda wako umeisha Mheshimiwa, nilikupa umalizie tu.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kukisema hapa, ni majonzi makubwa sana kwa Taifa letu, tunatengeneza mfumuko wa bei sisi wenyewe. Leo hii tunatenga fedha trilioni 150 kwa ajili ya kwenda kuweka ruzuku, unaenda kuweka ruzuku kwenye bei iliyotengenezwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi za Watanzania bilioni 150 ziende kwenye bei ya halisi ya mbolea. Wizara ya Kilimo ihakikishe kwamba inaenda kuondoa makandokando yote yaliyosababisha bei za mbolea kupanda… (Makofi/kicheko)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.