Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa nafasi hii ambayo umenipa. Awali ya yote nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mheshimiwa Bashe Waziri wa Wizara ya Kilimo na watendaji wakuu wote wa Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeisoma hotuba hii ya kilimo ukurasa ule wa 83, nimejiuliza, na umezua manung’uniko makubwa sana kwa sisi wakulima wa kahawa. Mazao ya korosho, pamba na tumbaku ni mazao ya kimkakati sambamba na zao la kahawa. Haya matatu yana ruzuku, lakini zao la kahawa halina ruzuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia katika mauzo ya nchi, zao la kahawa kwa muhula uliopita limetuingizia Tanzania Dola za Kimarekani milioni 142, tumbaku milioni 90. Tumbaku ina ruzuku, lakini zao la kahawa ambalo linatuingizia fedha nyingi za kigeni halina ruzuku. Ninaleta kwako manung’uniko makubwa sana ya wakulima wa kahawa kutoka katika Mkoa wa Kagera, Ruvuma, Songea, Kilimanjaro, Mbeya, Arusha, Kigoma, Mara, Tanga, Njombe, Iringa, Manyara, Katavi, Morogoro, Mwanza, wanaomba ruzuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii Serikali inatakiwa iwe na will. Haiwezekani kabisa tukalia miaka yote. Ukilinganisha na nchi zinazolima zao hili la kahawa, ukiangalia Uganda ambayo kila mwaka inauza tani 389,000 na Ethiopia ambayo inauza zaidi ya 457,000 uzalishaji wao unaongezeka, lakini sisi unadorora, sababu kubwa ni kuwepo kwa manung’uniko kutoka kwa wakulima wa kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nitoe mapendekezo yangu ili hakika kabisa kuwepo na mapinduzi makubwa katika uzalishaji wenye tija wa kahawa nchini Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja. Serikali iweke mipango madhubuti ya kuendeleza zao la kahawa. Mpaka sasa hivi hakuna mipango chanya yoyote ile ya kuendeleza zao hili la kahawa ambayo inaonekana licha ya kutupatia fedha nyingi za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili. Kipaumbele kiwekwe kwenye uzalishaji wa mbegu bora na miche bora. Sisi Tanzania kwa takwimu iliyopo kila mwaka tunazalisha miche bora milioni 20, wenzetu wa Uganda kila mwaka milioni 124, tuongeze ruzuku hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele imeshagonga.

MHE. KAVENJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi ninaomba angalao hata dakika mbili. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa umemaliza muda. Sentensi yako ya mwisho imeeleweka, nimeikatiza kwenye sehemu inayostahiki.

MHE. KAVENJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi ninaunga mkono hoja. (Makofi)