Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Issa Ally Mchungahela

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Nijielekeze moja kwa moja katika uchangiaji wa hotuba kutokana na ufinyu wa muda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kwamba, kilimo ni uti wa mgongo kama ilivyoanza kusemwa hapo mwanzo. Kilimo ni chakula, watu tunaishi kwa sababu ya chakula cha kilimo, lakini kilimo ni biashara. Takribani asilimia kubwa ya biashara yetu ya ndani na ya kimataifa inategemea sana kutoka kwenye mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ni uchumi. Takribani asilimia 30 ya Pato la Taifa inachangiwa na mazao kutoka kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ni ajira. Takribani asilimia 70 ya ajira zote za Tanzania zinachangiwa na kilimo. Katika hali kama hii hakuna njia yoyoye tunaweza tukapishananacho kilimo. Tunatakiwa kwa nguvu zote tuwekeze kwenye kilimo ili kuhakikisha kwamba, uchumi wetu unakua, lakini unakuwa imara. Nchi zote zilizoendelea ni kwa sababu, zimefanya mapinduzi ya kilimo na kwa kupitia mapinduzi ya kilimo ndipo unaweza ukaenda kwenye mapinduzi ya viwanda kwa sababu, viwanda na kilimo vinategemeana; kwa nini? kilimo chenyewe kinakuwa ni malighafi ya kiwanda, kwa hiyo huwezi kuzungumzia suala la kiwanda kama kilimo hakiko imara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina shaka na mipango iliyowekwa kwenye kilimo na Mheshimiwa Waziri na timu yake, ameweka mipango mizuri kabisa. Shaka yangu ni jinsi mtiririko wa fedha kutoka kwenye vyanzo hivyo; kwa maana ya vyanzo vya bajeti kwenda katika maeneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano halisi, muhula uliopita wa bajeti kilimo katika eneo la umwagiliaji kwenye suala la maendeleo kiliwekewa kiasi cha takribani bilioni 46.5, lakini cha kushangaza mpaka Februari mwaka 2020/22 imepelekwa milioni 590 pekee, hivyo kufanya asilimia 1.27 pekee katika suala la maendeleo la umwagiliaji, hasa ukizingatia kwamba umwagiliaji ndilo dira na umwagiliaji ndiyo maamuzi sahihi ya kufufua kilimo na kufanya kiwe bora. Sasa kwa mtindo huo sioni kama kweli tunaweza tukafikia lengo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hapo naomba nijielekeze mchango wangu katika kilimo cha nyumbani kwetu; kwa maana kilimo pendwa. Kilimo cha mazao pendwa, mazao ya korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hapo, naomba nielekeze mchango wangu katika kilimo cha nyumbani kwetu kwa maana ya kilimo pendwa, kilimo cha mazao pendwa cha mazao ya korosho. Korosho limekuwa ni zao pendwa, kadri siku zinavyoongezeka limekuwa zao mahsusi kabisa katika matumizi ya shughuli mbalimbali katika dhima za kitaifa na za Kimataifa. Kwa maana hiyo hata wanunuzi wa korosho wamekubali wenyewe kabisa kuwa na hiari kutoa bei nzuri kabisa katika korosho, lakini cha kushangaza ni kwamba bei hii haimfikii mkulima. Kwa maana hiyo Waziri pamoja na timu yake kuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba bei halisi inamfikia mkulima ambaye ni mvuja jasho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojaribu kuzungumzia tatizo kubwa la bei linatokana sana katika maeneo mawili, eneo la kwanza ni kwa sababu korosho zinauzwa ghafi huko India pamoja na nchi nyingine za Mashariki. Pia korosho zimezingirwa na wadau waliokosa weledi. Wadau wengi waliozingira kwenye korosho wamekosa weledi kwa namna moja au nyingine. Wako kwa mfano wafanyabiashara ambao wao kwao faida ndiyo msukumo pekee kwenye biashara hii au kwenye sekta hii. Halikadhalika wapo madalali ambao wao wamekaa kwa ajili ya kuwanyonya wakulima na wala hafanyi jitihada kubwa ya kuhakikisha kwamba korosho zinakuwa zao lenye tija kwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa kwa mchango huo.

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)