Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi, awali ya yote ninamshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyenijalia uhai na hatimae kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kweli bajeti hii sasa inakwenda kujibu mahitaji ya wakulima wetu ya muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninamshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Bashe, kwa kweli anafanya kazi nzuri sana. Mheshimiwa Waziri umekuwa ni kielelezo kwa vijana wachapa kazi sana pamoja na Naibu Waziri mnatuheshimisha sana. Mheshimiwa Waziri ninakushukuru na kukupongeza sana namna ambavyo umeshughulika na Ushirika, kati ya maeneo ambayo walikuwa hawamuelewi Mheshimiwa Rais anataka nini ni eneo hili la ushirika. Mheshimiwa Waziri nikupongeze tena kwa kazi hiyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza kwenye suala la mbegu ya alizeti. Katika Halmashauri yetu ya Wilaya ya Nachingwea tulitumia mapato ya ndani tukanunua tani moja na nusu mbegu hizi za alizeti na tukatoa kwa bei ya ruzuku kwa wakulima mapokeo yalikuwa ni mazuri sana, sasa kwenye mpango wa Wizara juu ya kutoa ruzuku hii kwenye mbegu za alizeti Mkoa wa Lindi haumo, ninamuomba sana Mheshimiwa Waziri aiangalie Lindi hususani kwenye Wilaya hii ya Nachingwea ambayo tayari tumeshaanza kuonesha nia na wakulima wetu wamepokea vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine ninaishukuru sana Wizara kwa kutoa bei elekezi kwenye pembejeo, huu ni mwanzo mzuri Mheshimiwa Waziri, kazi hii iendelee, hii itatufanya wakulima wetu waweze kupata bei nafuu na hivyo kuondoa ile changamoto ya bei kupanda mara kwa mara. Mheshimiwa Waziri eneo jingine ni kwenye upatikanaji wa pembejeo Jimbo langu la Nachingwea uhitaji kwa msimu huu ni tani 1,000, mpaka sasa tumepokea Sulphur peke yake tani 99, tunaona bado upatikanaji umekuwa ni wa chini mkituwezesha kupata kwa muda muafaka itatusaidia kuzalisha kwa wingi zaidi pia kuendana na muda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuwashukuru na kuwapongeza sana wakulima wa Wilaya ya Nachingwea kwa kazi nzuri na kubwa wanayoifanya. Hata hivyo, ipo changamoto na kadhia ya Tembo, nafahamu kwamba ninachangia kwenye Wizara ya Kilimo lakini mazao yanayoshambuliwa ni ya kilimo, Wanyama hawa waharibifu ni kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii. Adha hii ni kubwa na kwakweli kwenye maeneo yetu huko changamoto hii ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 16 juzi yupo mwananchi mmoja amekanyangwa na kuuawa na tembo, Serikali hii ni moja, Wizara ya Kilimo niiombe sana kwa sababu mazao haya yanayoharibiwa ni mazao yatokanayo na kilimo lakini waharibifu wapo kwenye Wizara ya Maliasili na Utalii, zungumzeni lugha moja ili muone namna ambavyo hawa wananchi wetu mtawasaidia, changamoto hii ni kubwa kweli kweli, yapo maeneo ambayo ukifika leo utawaonea huruma, anakwenda shambani anakwenda kufanya nini kwa sababu hawa wanyama wameshaharibu sana. Maeneo ya Namapwia, Nditi, Kata ya Ngunichile, Namikango, Lionja, Kipara, Kilimarondo, Matekwe, Kiegei hali ni mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Mheshimiwa Msambatavangu juzi alizungumzia hapa juu ya afya ya akili, hebu huyu mkulima ambaye amefanya kazi kubwa kwa kilimo tena cha kizamani kwa jembe la mkono halafu hawa Wanyama wanakwenda kufanya uhabiribu, matokeo yake kwa kweli huyu mtu anaweza akapata tatizo la afya ya akili. Katika hili ninaiomba sana Serikali izungumze lugha moja, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Maliasili na Utalii na hapa nisema tu Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii najua bajeti yake inakuja kwenye hili aandae kwa kweli maelezo ya kina yatakayonifanya nisiondoke na Shilingi yake kurudi nayo kule Nachingwea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali inatisha hali ni mbaya na sisi kama wawakilishi hatueleweki na mara kadhaa nimekwenda na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii alituahidi kutujengea kituo na kutuletea Askari, mpaka sasa hicho kituo hakuna na eneo hilo ni kubwa. Siyo hilo tu, kwenye Mkoa wa Lindi yapo maeneo mengine ambayo yamekubwa na kadhia hii, kwenye Jimbo la Mchinga kwa mfano, eneo la Milola, Kiwawa, huko nako waliahidiwa kujengewa kituo huko kwa ajili ya Wanyamapori eneo la Lutamba-londo bado hicho kituo kiliahidiwa tangu 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayasema haya kwa uchungu zaidi kwa sababu maisha ya yule mpiga kura wangu hayawezi kurudi tena hata kama akipata fidia, hayawezi tena kurudi kwa sababu tayari ameshafariki, tuchukue hatua sasa kabla ya madhara mengine zaidi kutokea. Hii siyo la kwanza mwaka jana mwezi wa Novemba hawa tembo walishawahi kusababisha tena madhara ya namna hiyo ya kuuawa kwa mtu mwingine, tulikwenda na Naibu Waziri alikwenda kutoa pole hapo, tunachotamani hapa ni kupata dawa ya kudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Kilimo wananchi wale sasa wanakata tamaa kwa sababu hakuna namna ya kwenda shambani tena. Hawa tembo sasa ukienda maeneo haya kwa mfano ya Namapuya ni kama ng’ombe sasa wapo tu wanazagaa, hata leo ukifika inatisha, hii hali hatueleweki.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)