Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. John Michael Sallu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. JOHN M. SALLU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Kwanza ninatoa shukrani nyingi kwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kuwa na political will kwenye kilimo, hii inatusababisha wakulima sasa tuwe na imani kwamba kilimo kitakuwa ndiyo mkombozi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ninashukuru sana Mheshimiwa Bashe Waziri wa Kilimo, Naibu wake, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu kwa jinsi ambavyo wanachapa kazi. Kwa mfano, katika Bunge hili niliwahi kuongelea inzi weupe wanaosumbua matunda hususani machungwa kwenye Jimbo langu, kwa kweli timu hii ilifanya kazi kwa haraka sana na wakaleta viuatilifu katika awamu mbili, kwa kweli wakulima wangu wamenufaika sana na hivyo viuatilifu na Kata zote zinazolima machungwa sasa hivi wanakamata wale inzi na machungwa yanaendele kuwa bora, nashukuru sana timu yote ya Wizara ya Kilimo kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ninashukuru Watafiti, kwetu zao la muhogo liliingia kama zao la kuokoa njaa lakini baada ya muda limekuwa ni zao la uchumi. Watafiti pale walituunga mkono wakaja kutukomboa kutoka kwenye kilo tatu mpaka tano kwa shina, mpaka kilo 10 hadi 15 kwa shina na sasa muhogo umeendelea kuwa na tija. Uzalishaji baada ya kuhamasika umekuwa mkubwa sana, sasa hivi hekta zipatazo 70,135 zina muhogo ambazo tuna makisio ya kuvuna takribani tani Milioni Kumi lakini tatizo kubwa linalotukabili sasa ni masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TANTRADE wamejitahidi kututafutia masoko ya nje lakini bado yanasuasua, kuna soko la ndani ambalo hatujaligusa kabisa, kwa utafiti nilioufanya tuna makampuni takribani 20 yanayoagiza starch kutoka nje lakini hawanunui kabisa starch yetu ya ndani. Namuomba Mheshimiwa Waziri Bashe akishirikiana na Wizara ya viwanda tuweze kuli-tap hili soko kwa sababu soko la ndani ni soko la uhakika zaidi ambalo linaweza kuleta tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Viwanda tuhakikishe kwamba waagizaji hawa wa starch waweze kutumia starch yetu ya ndani. Kweli kuna ambao wanaweza kutumia hii starch moja kwa moja kama raw ilivyo, lakini wapo wanaotumia modified starch, kwa hiyo Wizara hizi zishirikiane kuona kwamba hiyo modified starch inayotakiwa ni ya mtindo gani ili viwanda vyetu viweze kuelimishwa na hata wale ambao wanataka kuwekeza sasa wanaweza kujua wawekeze kwenye viwanda vya namna gani ili kukidhi soko hilo la ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka kwenye muhogo niende kwenye alizeti, napenda kumshauri Waziri ana mikakati mizuri ya kukomboa nchi yetu kwa zao la alizeti lakini katika ile Mikoa aliyoweka ya kimkakati Mikoa ambayo ina mvua mbili kwa mwaka hawakuiweka. Kuna Mikoa ambayo ina mvua mbili kwa mwaka ambapo na Jimbo langu lipo kwenye eneo hilo, ambalo unaweza kulima alizeti mara mbili kwa mwaka na ukavuna mara mbili kwa mwaka. Hii ingeweza kutatua tatizo la mafuta tulilonalo kwa haraka Zaidi. Ardhi tunayo ya kutosha, wananchi wapo tayari kabisa, tunaomba hizo ruzuku za alizeti nazo zije kwetu tuweze kukomboa shida iliyopo kwenye nchi yetu kwa sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la umwagiliaji nchi yetu ina mabonde mengi ya umwagiliaji na vilevile kwenye Jimbo langu kuna Mabonde ya mto Pangani na mabonde ya mto Msangazi, ninaomba Idara ya umwagiliaji ifuatilie mabonde haya na kuweza kuweka mbinu sahihi ya kutumia mabonde haya ili tuweze kuzalisha mbogamboga kwa wingi ambazo zinaweza kutuletea tija kwa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache nashukuru sana naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)