Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii muhimu ya wananchi na wakulima wetu. Kwanza nianze kabisa kwa kumpongeza na kumshukuru sana Rais wetu, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kuamua kuongeza bajeti hii ya kilimo kutoka Shilingi bilioni 294 mpaka Shilingi bilioni 751. Kwa kweli huu ni ushindi mkubwa sana kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kitu kimoja ambacho nataka Wabunge wenzangu tukione na kama tunaweza kusaidia kubadilisha. Mwaka jana bajeti ilikuwa Shilingi bilioni 294 na katika hizo fedha za maendeleo zilizochangiwa kwenye hiyo bajeti zilikuwa Shilingi bilioni 164, lakini ni asilimia 46 tu ya bajeti nzima ya maendeleo iliyotoka Serikalini kwenda kwenye Wizara ya Kilimo. Sasa mwaka huu bajeti imepanda zaidi imekuwa Shilingi 751 bilioni, na katika hizo bajeti zaidi ya Shilingi bilioni 630 zinakwenda kwenye maendeleo kwa mafungu yote mawili 43 na 05. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali la kuuliza. Je, hizo fedha zitatoka? Kwa sababu kupanga bajeti na hela kutoka ni vitu viwili tofauti. Kama tutakaa hapa tutaongea hata kwa wiki nzima nakushauri hiki, nakushauri kifanyike hiki au kipi tunataka lakini kama Serikali haitatoa fedha za bajeti ya maendeleo kwenye hii Wizara ya Kilimo itakuwa ni kazi bure. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nimuombe Waziri wa Fedha aiangalie bajeti hii ya Wizara ya Kilimo kwa jicho la tatu. Au ikiwezekana sisi Wabunge tufunge angalau kwa wiki moja tumuombe Mwenyezi Mungu awaguse Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri wa Fedha kuhakikisha bajeti ya Wizara hii ya Fedha fedha zote zilizoombwa zinakwenda kama zilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu tangu uhuru haijawahi kutokea bajeti ya Wizara ya Kilimo ikazidi Shilingi bilioni 300; lakini mwaka huu bajeti imekuwa mpaka Shilingi bilioni 751. Na kama Mungu akitujalia hii bajeti yote ikapita kama ilivyo na fedha zote zikaenda, mimi naamini nchi yetu ya Tanzania itakuwa imepiga mageuzi makubwa sana kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ina maana bajeti zote za ushirika zitafanya kazi, miradi yote ya maendeleo itapata fedha, kila kitu kilichoombewa kitakuwa na fedha, na kaka yangu Bashe nafikiri utaongezeka at least kilo 10. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine nafikiri imefika sasa tuwe na sheria ya kilimo. Huko vijijini watu wanauza mbegu feki. AMCOS nyingi hazilipi wakulima zinachukua mazao zinalima. Hawa watu hata wakikamatwa wakipelekwa mahakamani inageuka kuwa ni kesi za madai. Sasa mtu umemuuzia mtu mbegu feki, mtu umekopa fedha zake hujalipa mazao yake itakuwaje kesi ya madai? Mimi naomba hii iingizwe iwe kesi ya uhujumu uchumi. Na mimi naomba Mheshimiwa Waziri kama hutaleta muswada kwenye bajeti ya mwezi wa tisa hawa watu tu-criminalize basi mimi nitaleta muswada binafsi na ninaomba Wabunge wenzangu mniunge mkono hii iingizwe iwe sheria ya uhujumu uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani watu wawauzie wakulima mbegu feki, vyama vya ushirika visilipe mapato yao kwa wakulima alafu iwe ni kesi ya madai. Hichi kitu hakiwezekani tunawatia umasikini. Kwa hiyo, kuna umuhimu mkubwa wa hii sheria ya kilimo ije.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha mwisho; mimi natoka Mkoa wa Songwe. Sisi tunalima sana mahindi lakini mbegu zetu bora tunazotumia zinatoka Zambia. Sasa mimi naomba, na ambacho ninachoomba Wizara kama basi tunashindwa kuwaruhusu watu wetu waende Zambia kuchukua mbegu basi tufanye mpango hizo mbegu bora za Zambia zije zizalishwe hapa Tanzania. Kwani kuna ubaya gani hizo mbegu za Zambia zikija zikazalishwa hapa? Kwa sababu mbegu zilizopo Tanzania hazikubali kwenye mikoa yetu…

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante.