Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi ili nichangie katika Wizara hii muhimu, Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri kaka yangu Bashe na Naibu wake; lakini pia niwapongeze Makatibu Wakuu wote watatu kwa kazi nzuri wanayoifanya. Kipekee nimpongeze Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mama Samia Suluhu kwa kazi nzuri na kwa kuijali Wizara ya Kilimo kwa kuongeza takribani shilingi bilioni 751. Hiki si kitu kidogo, hongera sana Mama yetu, kazi unaipiga na unaupiga mwingi Mama yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niingie sasa kwenye hoja zangu. Kwa sababu ya muda niongelee suala la pembejeo. Mkoa wa Rukwa maisha yetu sisi ni kilimo lakini pia mbolea ndiyo kila kitu. Hata hivyo, changamoto iliyopo mbolea imepanda bei kubwa sana. Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea kuhusu mbolea. Mbolea ndiyo habari ya mjini, mbolea ndiyo imeshika maisha ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Bashe akiweza kutatua changamoto ya mbolea kwa bajeti iliyopangwa hii kwa kweli maisha ya Watanzania na kilio cha Watanzania na machozi ya Watanzania yatafutika.

Mheshiimwa Naibu Spika, Mkoa wetu wa Rukwa unalima mazao mengi sana ikiwemo mahindi, maharage, ufuta, miwa na mazao mengine mbalimbali yanalimwa Mkoa wa Rukwa. Hata hivyo changamoto kubwa ni hilo suala la bei ya mbolea. Tunaomba Serikali iweke ruzuku. Hili si ombi, ni lazima Serikali iangalie suala zima la kuweka ruzuku kwenye pembejeo hasa kwenye mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niingie sasa kwenye suala zima la kilimo cha miwa Mkoa wa Rukwa. Mkoa wa Rukwa pamoja na kulima mazao mengine yote tunalima pia miwa. Tunaomba Serikali ifanye utafiti iweze kujenga kiwanda cha kuchakata miwa, tutaweza kupata sukari ambayo imekuwa nayo ni tatizo kubwa sana katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee pia suala la matrekta. Wizara hii kupitia taasisi yake ya NBC iliweza kukopesha matrekta kwa Watanzania, lakini matrekta haya yamekuwa ni kichomi, adhabu, matrekta ni mabovu, matrekta uki-test mitambo tu ukiwa shambani trekta linabongonyoka, trekta linakuwa kama muhogo, ukilishika kidogo mara kichwa kule, mara kiwiliwili huko, matrekta hayaeleweki.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Serikali ikayachukuwe matrekta kwa wananchi, matrekta yale imekuwa ni kichomi, matrekta yale yanawatesa wananchi wanawekwa ndani kila siku. Kama unaweza kuona hata Wabunge humu walikopa yale matrekta yani yale matrekta yamekuwa ni kichomi, ikiwezekana Serikali iweze ikayabeba ikayarudisha huko walikoyatoa, kuliko adhabu hii wanayopata wananchi, wanawekwa ndani wanalipa kila siku, lakini matrekta ni mabovu hayaeleweki.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee tena suala lingine, niingie kwenye suala la benki. Benki ya Kilimo haijatunufaisha hasa sisi wa Mkoa wa Rukwa. Benki ya Kilimo tunaisikia tu iko Dar es Salaam na Dodoma, lakini kwenye mikoa hii ambayo inalima sana mazao hakuna hiyo benki. Sasa maana yake ni nini benki inaitwa Benki ya Wakulima, kwa wakulima hakuna benki hiyo, basi naomba Serikali iweze kupeleka benki kwenye mikoa ambayo inalima sana mazao, kwa mfano, Rukwa ipelekwe kabisa iandikwe Benki ya Kilimo kama zilivyoandikwa benki zingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, benki nyingine zinaandikwa Benki ya NBC, NMB zinaeleweka, lakini Benki ya Kilimo hatujaona, kwa hiyo Serikali ijitathimini sana kupitia Benki hii ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee tena suala lingine…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa mchango mzuri.

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)