Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Michael Mwita Kembaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika sekta hii ya kilimo ambayo ni uti wa mgongo katika uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama unavyoelewa nchi yetu asilimia kubwa ya wananchi wetu wanategemea kilimo ili kujipatia kipato cha kila siku, matatizo mengi yanaweza kutatuliwa kupitia sekta hii ya kilimo ikiwemo chakula, pesa za kigeni, malighafi katika viwanda vyetu na ajira kwa vijana wetu. Majibu ya matatizo haya yanayoikabili nchi yetu yanaweza kutatuliwa pale ambapo Serikali itawekeza na kuipa kipaumbele sekta hii ya kilimo ambapo itaweza kutatua changamoto ya ajira katika nchi yetu lakini pia kupata malighafi za kutosha katika viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya kazi nzuri na kuwekeza pesa nyingi katika upande wa utafiti. Kama unavyojua ili kilimo chetu kiweze kufanya vizuri Serikali inapaswa iweke pesa nyingi katika utafiti, maana utafiti utaweza kuleta majibu ni wapi tunaweza tukalima mazao mazuri na yakafanya vizuri. Pamoja na kuwekeza pesa nyingi katika utafiti, umwagiliaji bado tija ni ndogo sana, hauleti majibu ambayo yanatosheleza. Kwa mfano, tunavyo vituo vingi vya utafiti katika nchi yetu mfano tunavyo vituo vikuu ambavyo ni TARI Kihinga, Ilonga, Tumbi, Buyola, Makutupola, Seyani, Ukiriagulu, Naliendele Mlingano, lakini pia tunavyo vituo vidogo ambavyo ni TARI Mikocheni, Tengeru, Naruku, Dakawa, Ifakara, Hombolo na Kifyulilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na vituo hivi vyote, Serikali imekuwa ikipeleka pale pesa nyingi, utafiti umekuwa ukifanyika na majibu yanapatikana. Mfano, tulitembelea Kibaha tulipata watafiti wamefanya kazi nzuri sana, kuna muhogo mkubwa ambao ni zaidi ya kilo tano uko pale na umekuwa kama maonyesho katika kituo kile. Pia wataalam wale wamegundua wadudu rafiki ambao wakitumika badala ya kutumia viuatilifu ambavyo ni hatari kwa afya ya binadamu, lakini pia wamegundua hazina kubwa ya tafiti ambazo ni za udongo ambao unafaa na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tafiti hizi ambazo zinagunduliwa na wataalam wetu haziwafikii wakulima wetu. Ni masikitiko yangu kwamba, pale katika Jimbo langu la Tarime Mjini, tumeshaacha kulima zao la muhogo, kwa sababu wadudu wanashambulia muhogo na haufanyi vizuri. Vilevile kuna ugonjwa ambao unashambulia migomba na wataalam hawa wamegundua mbegu nzuri ambayo wakulima wakilima haishambuliwi na magonjwa, lakini bado wakulima hawafikiwi na tafiti hizi ambazo zinafanywa na wataalam wetu. Pamoja na kwamba Serikali inatoa pesa nyingi katika tafiti lakini haifikishi kwa wakulima, hivyo haina tija kwa sababu walengwa wakubwa ni wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa niseme hakuna haja ya kutoa fedha kwa watafiti ambapo tafiti hizi zinawekwa kwenye madroo na zinawekwa kwenye makabrasha badala ya kuchukuliwa na kupelekwa kwa wananchi. Nitoe ushauri wangu kwa Serikali wanapokuwa wanatenga fedha kwa ajili ya utafiti, watenge fedha kwa ajili ya kupeleka ujumbe au matokeo ya tafiti zinazopatikana kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivi, kwa sababu kazi yote tunayojadili hapa, hoja zote zinazotolewa na Wabunge hapa, lengo lake ni wakulima ambao wengi wao wako vijijini hawako mjini. Mara nyingi wanapofanya maonyesho, wanafanya mjini wanaacha wakulima pale vijijini. Ningependa Waziri wa Kilimo kaka yangu, ahakikishe fedha zitengwe kwa ajili ya kuwafikia walengwa ambao ni wakulima, wapate taarifa sahihi. Kwa kufanya hivi wakulima…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana kwa mchango mzuri, mengine andika.

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)