Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Kilimo. Awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii na fursa hii

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa muda ni mdogo naomba nijikite kushauri tu kwa maneno machache.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia katika hotuba hii ya Waziri yote, na ninaomba nishauri mambo machache. Waziri aangalie kumlenga mwananchi mnyonge wa hali ya chini katika bajeti hii ya Shilingi milioni 751. Nakuomba rafiki yangu pamoja na Naibu Waziri Mavunde, msipoangalia hizi fedha zinaenda kuishia kwenye mikono ya watu wachache, hazitamsaidia mwananchi yule wa kawaida anayelima kwa jembe la mkono.

Mheshimiwa Naibu Spika, hisia za Mheshimiwa Rais pamoja na viongozi wote, pamoja na hotuba zote tukiwa kwenye kampeni mwaka 2020 tuliahidi kwamba tutawasaidia wanyonge. Nakuomba Waziri kupitia ubunifu uliouunda kutengeneza kombati pamoja na mavazi special kwa ajili ya mkulima, ufuate mfumo huo huo, tengeneza programu nyingine, acha kutegemea mabenki. Wakulima huwa hawana akaunti benki, lazima ulijue hilo. Wazazi wetu hawana akaunti benki.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia mkulima, lazima umfikirie mkulima yule wa hali ya chini. Unaenda kumwezeshaje aliye na jembe la sheli ya ng’ombe? Unaenda kumwezasheje yule anayelima kwa jembe la mkono? Mheshimiwa Waziri fikiria mambo kama yale, tutaonekana watu wa maana, washauri wazuri, ukifuata ushauri wangu huu wa mwishoni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, kule Mbogwe ninazo sehemu nyingi sana, sioni hata sababu ya kufanya utafiti. Kitu kikubwa sana sana huwa ni mvua tu. Mheshimiwa Waziri sijui unanisikia! Sijui umeangalia pembeni! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Waziri atakapokuja kuhitimisha hapa, naomba aje na Mpango, Wilaya ya Mbogwe ananisaidiaje? Ninazo Mbuga kubwa ambazo zinahitaji scheme, ukinisaidia skimu hata 20 hutasikia njaa katika Taifa hili la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nikupongeze tu Mheshimiwa Waziri, mwaka 2021 ukiwa Naibu Waziri nilikuja kwako nikalia kuhusu kiwanda changu cha Kagiri kile ulichokuja kukiangalia na kukifungua. Ulinipatia Shilingi bilioni sita na mwenyewe umeyaona matokeo, tumeingiza faida pamoja na wanakulima wanapewa ruzuku. Mwaka huu tumeandika andiko, tunataka Shilingi bilioni 13, tunataka tuzalishe mafuta wenyewe ya pamba pale Mazumbwe Kagiri na tunataka tuzalishe mafuta ya alizeti. Usisite. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyabiashara na wakulima tunajuana, ukisema unahitaji kusaidia wakulima kupitia Jeshi lile uliloligawia pikipiki, sasa hivi wanawajua wakulima. Usiangalie watu wanaokimbia sasa hivi kusajili makampuni, wanakuja kukuangusha hao Waziri, waepuke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiria mwaka 1992 katika utawala wa Rais Mwinyi, tulikuwa tukiletewa mbegu za pamba mpaka Kijijini. Sasa hivi mnashindwaje kutuletea moja kwa moja mbegu za pamba, tukalima pamba na tukafaidika? Kwa nini mnapitia Mawakala? Mheshimiwa Waziri hebu jaribu kulifikiria hilo. Wewe uzuri umezaliwa kwetu huko, unajua maisha ya Kijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi fedha naomba zisiishie mjini, zisiende kwa watu wenye makampuni ya mjini. Wakulima walio wengi huwa hawana akaunti. Utaweka akaunti vipi wakati wewe ni Mkulima! Kwa hiyo, kupitia watu wako wale uliowapa pikipiki Mheshimiwa Waziri, wewe kaa nao, waulize huko una wakulima wangapi; ili uweze kuwasaidia. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana kwa mchango wako mzuri.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naunga mkono hoja. Mchango mwingine nitaandika kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)