Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja iliyoko Mezani. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake wa dhati wa kuongeza Bajeti ya Kilimo kutoka Shilingi bilioni 294 mpaka Shilingi bilioni 751. Haya ni mapinduzi makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee niwapongeze viongozi wa Wizara hii; Mheshimiwa Bashe na Mheshimiwa Mavunde pamoja na Katibu Mkuu na timu yake kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kuifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu unajikita kwenye zao la korosho na nianze na soko la korosho na bei ya korosho. Naomba Wizara iimarishe Kitengo cha Masoko katika Wizara hii lakini pili, na Bodi ya Korosho ili korosho yetu ipate bei nzuri sokoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachoendelea sasa hivi kwenye Mnada wa Korosho, tunapata bei nzuri kwenye mnada wa kwanza na minada yote inayofuata korosho bei inashuka. Hatujui kushuka huku ni kwa kupanga au ni kwa sababu soko limeshuka. Tukiwa na taarifa za kutosha kwenye soko, basi itasaidia kupata taarifa za uhakika na kuimarisha bei yetu ya korosho na kudhibiti uuzaji wa korosho katika minada.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya pili ni kuhusu ubanguaji wa zao la korosho. Tuna mkakati wa kubangua zao la korosho. Tulikuwa na viwanda vyetu 12 hapo nyuma mpaka sasa hivi havifanyi kazi na vingine vimegeuzwa kuwa magodauni. Mheshimiwa Bashe wewe ni bingwa wa kuthubutu, chukua angalau viwanda vitatu vianze kubangua korosho na hilo unaliweza ili tuanze kubangua korosho badala ya kupeleka korosho ghafi huko nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tatu ni kuhusu pembejeo. Naipongeza sana Wizara kwa kutoa pembejeo bure kwa wakulima na nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa mwaka wa pili kutoa pembejeo bure kwa wakulima wa korosho. Naomba udhibiti ufanywe ili pembejeo hizi zifike kwa wakulima husika na siyo mikononi mwa walanguzi. Pili, pembejeo hizi sasa wasambazaji watoe mafunzo kwa wakulima kama ilivyofanya Kampuni moja ya BEZ naipongesa sana. Imetoa mafunzo kwa wakulima ili kupunguza dosari za utumiaji wa dawa hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala langu lingine ni kuhusu Export Levy. Mheshimiwa Waziri utakuja na Muswada hapo wa Export Levy ili fedha isiwe chanzo cha mapato kwa Serikali. Export Levy irudi kwa mkulima ili iongeze uzalishaji, ili tufufue viwanda vyetu vya korosho, ili iimarishe utafiti, ili ile fedha ambayo anachangia mkulima sasa hivi Shilingi 25/= kwa ajili ya TARI Naliendele asikatwe mkulima, ichukuliwe kwenye Export Levy. Export Levy itasaidia kutoa uhamasishaji kwa wabanguaji wa korosho. Kwa hiyo, naomba kwenye Muswada wa Fedha ujao, basi utuletee ili Export Levy irudi na asilimia 65 iende kwenye zao la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)