Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi. Kwanza nampongeza Waziri, Naibu Waziri na timu nzima ya Wizara naona wamejipanga vizuri, na tumeona mwanzo umekuwa mzuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda nitaongelea hoja moja ya Kahawa. Nampongeza sana Waziri, kwa muda mfupi ametoa taarifa, ameanza kusambaza miche ya kahawa katika maeneo yale yanayolima kahawa. Kwa bahati mbaya, sisi wana Mbinga tunalima kahawa na kwa bahati mbaya hatukupata miche. Nina uhakika kwa sababu ulikuwa mwanzo, sasa hivi ataenda kutoa miche Wilayani Mbinga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Mbinga wamenipigia simu hapa, wana imani kubwa sana na Mheshimiwa Waziri. Wanaomba kwamba akimaliza bajeti hii, basi apange muda akawatembelee. Wako tayari kumpokea na wana mashamba wameandaa, wanachosubiri sasa hivi ni miche ya kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, suala la Bodi ya Kahawa. Mimi sifahamu, Bodi nyingine unasikia zimechangamka zinafanya hivi, lakini Bodi ya Kahawa sisikii chochote. Kwani wao siyo Bodi kama Bodi ya Pamba? Kwani wao siyo Bodi kama Bodi ya Korosho? Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ongea na huyu Bwana wa Bodi ya Kahawa, kwa sababu tunataka tuone nchi inachangamka. Kama Korosho Bodi inafanya hivi, Pamba inafanya hivi tunataka kuona na Kahawa pia mtu wa Bodi anafanya kitu fulani. Mpaka saa hizi sijaona Bodi inafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, waliweka malengo ya kuongeza uzalishaji kwenye kahawa, lakini sijaona mikakati hasa ya nini kinaenda kufanyika. Kama Bodi, wao wanafanya nini? Kwa hiyo, nakuomba Mheshimiwa Waziri, najua umejipanga vizuri kwenye hili na ulininong’oneza pembeni kwamba Mbinga watapata miche mingi kwa sababu Kahawa ya Mbinga ni nzuri zaidi halafu tamu na inapendwa zaidi duniani huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala la mbolea. Sisi wana-Mbinga bila mbolea hatujavuna. Tunamshukuru Mungu safari hii tulitumia miujiza. Maana yake mfuko mmoja tumetumia zaidi ya ekari mbili mpaka tatu. Kwa hiyo, tunashukuru mazao yamekua lakini uzalishaji hautakuwa kama ule tuliouzoea miaka yote. Kwa hiyo, uzalishaji kidogo utapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa lile wazo la ruzuku ya mbolea. Nami nikuomba suala hili kama ulivyosema jana, uko tayari ukose vingine vyote lakini tupate ruzuku ya mbolea. Mbinga ni wazalishaji wakubwa wa mahindi, lakini hatuwezi kuzalisha bila mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda huu mfupi, nashukuru sana. Nilikuwa na mambo hayo mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)