Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Kilimo, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Kilimo kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendeleo endelevu na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Spika, kulingana na taarifa ya Wizara ya Kilimo, Tanzania ina hekta milioni 44 zinazofaa kwa kilimo cha mazao, kwa wastani hekta milioni 10.8 tu sawa na asilimia 24 ndizo zinazolimwa kila mwaka. Sekta hii kwa mwaka 2020 imechangia asilimia 26.9 kwenye Pato la Taifa, imetoa ajira kwa wananchi kwa wastani wa asilimia 61.1 na imechangia asilimia 65 ya upatikanaji wa malighafi za viwanda. Sekta ya kilimo ni mhimili wa uchumi wa nchi na inachangia pato la mkulima mmoja mmoja, kaya na Taifa kwa ujumla. Sekta ya kilimo na hususani sekta ndogo ya mazao imechangia asilimia 15.4 katika Pato la Taifa na zaidi ya asilimia 100 ya upatikanaji wa chakula kinachozalishwa nchini na kupelekea kupunguza mfumuko wa bei kwa takribani asilimia 59.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kujitosheleza kwa chakula na kuchangia katika uchumi wa Taifa, takribani mazao yote yanazalishwa kwa tija ndogo katika eneo husika. Uzalishaji wa mahindi wa tani 1.76 kwa hekta moja ni asilimia 29 tu ya uzalishaji unaotegemewa wa tani sita kwa hekta moja. Uzalishaji huu wa chini kwa mazao yote unatokana na ukosefu wa ushauri wa watalaam wa kilimo ikiwemo matumizi yasiyo sahihi ya mbolea na pembejeo zingine. Katika hali hii, kilimo hakijamsaidia mkulima kwa kiasi kikubwa kunajinasua kwenye umaskini na kimeendelea kutoa mchango mdogo kwenye Pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, upatikanaji wa mbolea nchini hadi Februari, 2022 ulikuwa tani 436,452 sawa na asilimia 63 ya mahitaji ya tani 698,260, lakini kutokana na bei kubwa ya mbolea mauzo yalikuwa tani 173,957 tu sawa na asilimia 25. Wakulima wengi walishindwa kumudu kununua mbolea kutokana na mfumuko wa bei wa asilimia 100 na ikichangiwa na hali isiyoridhisha ya mvua inaweza kupelekea upungufu wa uzalishaji hasa mazao ya nafaka. Napendekeza Serikali ichukue hatua za kurudisha ruzuku ya pembejeo pamoja na kuanzisha Price Stabilization Fund kwa pembejeo hasa mbolea ili kuongeza tija kwenye uzalishaji wa mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, nashauri Serikali iendelee kuimarisha usalama wa chakula nchini kwa kununua na kuhifadhi nafaka kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula. Kutokana na vita ya Urusi na Ukraine kunaashiria upungufu mkubwa wa nafaka na kwa kuzingatia gharama kubwa za uzalishaji wa karibu asilimia 100, Serikali ichukue hatua za makusudi kusaidia wakulima wapate bei nzuri ya NFRA badala ya kuuza kwa walanguzi na kutorosha chakula nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, Serikali iangalie fursa za kiwanda cha Viuadudu cha Kibaha kuanza uzalishaji wa viatilifu inayotokana na pareto ambayo inazalishwa hapa nchini na imekuwa inauzwa nchi za nje kama semi-finished product kwa bei ndogo ya kutupa. Viatilifu kutokana na pareto ni suluhisho la soko la pareto na pia suluhisho kwa upotevu wa mazao kushambuliwa na wadudu (post-harvest losses). Pia Serikali ianze mchakato wa kutumia madini (calcium carbonate, agricultural lime, phosphates, natural gas etc.) yanayopatikana kwa wingi hapa Tanzania, kuanza uzalishalishaji wa mbolea hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha bajeti ya mwaka 2021/2022, Serikali ilitenga shilingi 164,748,000,000 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo ambapo shilingi 82,180,000,000 ni fedha za ndani na shilingi 82,568,000,000 ni fedha za nje. Utekelezaji wa miradi hadi kufikia Februari, 2022 hasa utekelezaji kwa fedha za nje uko chini sana. Kutokana na hali hii sekta ya kilimo imeendelea kudorora katika kuchangia Pato la Taifa. Matumaini pekee ni hatua zilizooneshwa kwenye bajeti ya ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji na Serikali iweke mikakati madhubuti kuhakikisha ufanisi wa utekelezaji wa bajeti hii ya umwagiliaji. Pia mikakati hii iweke nyongeza za ujenzi wa mabwawa hasa maeneo yenye mafuriko makubwa ikiwa ni pamoja na kuzuia mafuriko.

Mheshimiwa Spika, pia napendekeza Serikali iweke msukumo mkubwa wa kuharakisha utekelezaji wa miradi iliyomo kwenye mradi wa Bonde la Mto Songwe (Songwe River Basin Development Programme - SRBDP), wenye ofisi zake Kyela, Tanzania. Mradi huu unaotekelezwa kwa pamoja na Serikali za Tanzania na Malawi, ni muhimu sana kwa sasa kutokana hasa na ujenzi wa mabwawa ambayo pamoja na manufaa mengine yatasaidia kupunguza mafuriko ya Bonde la Kyela. Mabwawa haya yamelenga kuzalisha umeme, kilimo cha umwagiliaji, shughuli za uvuvi na hata utalii ambao unahitajika sana katika Wilaya ya Mbeya na ukanda wote wa Nyanda za Juu Kusini.

Mheshimiwa Spika, Serikali ichukue hatua za haraka kuleta Bungeni mapendekezo ya Sheria ya Kilimo ambayo pamoja na mambo mengine itawezesha usimamizi wa matumizi bora ya ardhi ya kilimo ambayo inaendelea kupotea kwa matumizi ya makazi. Pia kutokana na changamoto za tabia nchi, kumekuwepo na uharibifu mkubwa wa mazingira na ongezeko la upungufu wa vyanzo vya maji. Uharibifu unaotokana na shughuli za kibinadamu umepelekea misitu mingi kuharibiwa na uchomaji moto, ukataji mkaa na hata kilimo kwenye vyanzo vya maji.

Napendekeza Serikali iongeze msukumo kwa Wizara za Maji, Kilimo, Maliasili na Mazingira kufanya kazi kama timu moja ili kukabiliana na janga hili kubwa ikiwemo ujenzi wa mabwawa makubwa katika maeneo yanayokumbwa na mafuriko. Kama ilivyo kwa athari za mafuriko ya Kyela, hata Ziwa Rukwa linaathirika sana na kujaa mchango na udongo unaosombwa na mito kutokana na mmonyoko wa udongo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.