Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja hii ya Mheshimiwa Bashe, Waziri wa Kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa nchi yetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa uthubutu wake kuweza kuongeza bajeti kwenye Wizara hii ya Kilimo ambayo ni uti wa mgongo wa Watanzania wote. Lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Bashe na Naibu wake Mheshimiwa Mavunde kwa namna ambavyo wamepangilia na kujitayarisha kufanya kazi kwa ajili ya Watanzania wote wanaoshughulika na kilimo kitaalam kabisa. Hongereni sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala moja tu ambalo mimi nataka kutoa ufafanuzi nalo ni suala la wafugaji kuingiza mifugo yao kwenye mashamba ya wakulima, mashamba ya mahindi ama mazao mengine. Suala hili limezungumzwa kwa uchungu, sauti, inayoeleweka na Mheshimiwa Alexia Kamguna, Mbunge wa Viti Maalum, Morogoro. Nipende kusema tu, hakuna sheria ya nchi yetu inayoruhusu wafugaji waende kuchunga kwenye mashamba ya wakulima ambao wamelima mazao yao. Hakuna sheria ya namna hiyo. Hata sheria zinazotuongoza kutenga maeneo ya kufugia hazisemi hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi pia nimewahi kuchunga mifugo, ilikuwa marufuku kwenda kupeleka ng’ombe kwenye shamba la mtu la mahindi au mazao mengine na kulisha; ukifanya hivyo ukirudi nyumbani utapata adhabu kali; na familia yenye ng’ombe iliyokuwa inafanya hivyo, inachukua ng’ombe wake inakwenda kulisha mashamba ya watu wengine ilikuwa inajulikana kama familia ya watu wenye dharau, wasio na heshima na hivyo ilitengwa kwa namna fulani, hata ikiwa na mabinti wazuri kiasi gani, mabinti wale walikuwa hawaolewi kwa sababu wanatoka katika familia yenye dharau. Hata ikiwa na vijana wa kiume wazuri jinsi gani, vijana wale hawawezi kuoa kwenye kile kijiji, wataoa kijiji cha mbali ambako hawajulikana kwamba wanadharau na familia yao inadharau kwa sababu inatabia ya kupeleka mifugo yake kwenye mashamba ya watu wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, vitendo hivi havikubaliki. Niombe tena wafugaji popote mlipo, nchi yetu inaruhusu tuishi mahali popote ili mradi tusivunje sheria za nchi. Sasa wafugaji acheni kupeleka mifugo yenu kwenye mashamba ya wakulima, hairuhusiwi kwa sheria zetu; sisi Wizara ya Mifugo na Uvuvi miongozo yetu inakataa. Tuna miongozo ya malisho na rasilimali za vyakula vya mifugo. Hakuna mahali tumetaja mifugo ikale mazao ya wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana sana sana, tunaendelea kutoa elimu kama Wizara ili kuwaelimisha wafugaji waelewe na wasipeleke mifugo yao kwenye mashamba ya wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe sana viongozi, ngazi za Serikali za vijiji, Kata, ngazi za wilaya waangalie jambo hili. Jambo hili linatokea na wenyewe wapo pale. Wakulima wanapigwa, wanadhulumiwa mazao yao, kusema kweli ni kama kitendo cha kuhujumu uchumi; kwa sababu tunafahamu, mkulima ametegemea amelima hekali zake tatu, amefikia mahali pa kuvuna, halafu mifugo inaachiwa inakula mazao yote. Maana yake huyo mkulima kwa mwaka mzima atakuwa hana kipato, chakula, kwa hiyo hana namna ya kuishi mpaka mwaka mwingine utakapokuja. Kusema kweli tabia hii siyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie tu kwa kusema kwamba, wafugaji tufuge kileo, tufuge kwa kuelewana na wenzetu wanatumia ardhi ileile. Tufuge na wenzetu anaofanya shughuli za kiuchumi, tuziheshimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nakushukuru sana, sisi kama Wizara tutaendelea kutoa elimu kwa wafugaji ili waweze kuelewa kwamba jambo hili ni baya. Nitakwenda Mkoa wa Morogoro, nitatembelea mahali ambapo wafugaji wapo wengi tuelimishane, tuelezane ni namna gani tunaweza kushi na Watanzania wengine vizuri kuliko kuendeleza migogoro ya namna hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.