Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Kwanza ni shukurani kwa Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma aliyetuwezesha kufika siku ya leo. Pili ni kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani kubwa aliyonipa ya kuniteua kuwa Naibu Waziri katika Wizara hii ya Kilimo; na pia kuwashukuru wananchi wangu wa Dodoma Mjini kwa heshima kubwa waliyonipa kuwa Mbunge wao; na la tatu, ni kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Hussein Mohamed Bashe ambaye amekuwa kaka, rafiki, mwalimu, Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana. Pia nichukue fursa hii kuwashukuru sana watendaji wote wa Wizara wakiongozwa na Katibu Mkuu Andrew Masawe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza ambalo nilikuwa nataka nizungumzie ni suala la program ya vijana kushiriki kwenye kilimo. Tunatambua kwamba vijana wetu wa nchini Tanzania si kwamba hawapendi kilimo lakini mazingira ya kuwafanya wafanye kilimo hayakuwa rafiki sana. Walikuwa na changamoto ya maeneo, mbiundombinu, pembejeo, masoko na mitaji. Tumekuja na program maalum ambayo inaitwa, jenga kesho bora ya vijana, ambayo lengo lake kubwa ni kuhakikisha kwamba tunawapatia vijana maeneo, ambayo tutapima afya ya udongo. Pia tutawapatia pembejeo, tutawatafutia masoko na hatimaye lengo letu ni kuwa na kitu kinaitwa Kijiji cha Vijana cha Kilimo. Tunaamini kabisa hii itakuwa sehemu nzuri ya kuweza kuwavutia vijana wengi kufanya kilimo. Kwa kuanzia tutaanzia hapa Dodoma ndiyo itakuwa sehemu ya pilot zaidi ya ekari 20,000 zitatengwa kwa ajili ya block farms ambazo vijana wengi watahusishwa kushiriki katika kilimo hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni la zabibu. Tumejipanga kuendelea kuhamasisha wakulima wa zabibu kulima kwa tija ili hatimaye zao hili liwaletee mafanikio. Mwezi ujao tutakamilisha uanzishwaji wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Wakulima wa Zabibu ili wawe na sauti moja. Lakini vilevile tumekwenda mbali zaidi, tunakwenda kuanzisha viwanda vitatu vikubwa vya uchakataji na uhifadhi wa mchuzi wa zabibu ili wakulima wetu waache kuuza zabibu wauze mchuzi wa zabibu na uwaletee tija kwenye kilimo chao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumeongeza utafiti kwenye eneo hilo la zabibu na hivi sana ndugu zetu wa pale TARI Makutupora wametuongezea mbegu zingine. Tunataka wakulima wetu pia waanze kuuza zabibu za mezani; na hivi sasa tumeshagundua mbegu ya ruby seedless ambayo itakuwa ni zabibu za mezani. Lakini vile vile na zabibu za viungo (raisins), hizi zote zitafanyika katika kukuza zao letu hili zabibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumeingia makubaliano na wenzetu wa TBL kwa ajili ya kilimo cha mkataba cha wakulima wa zabibu ili wapate uhakika wa masoko yao ya zabibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ni masuala la mboga mboga na matunda. Tumeingia makubaliano na wenzetu wa TAHA chini ya Dkt. Jacquline Mkindi ambaye ametenga muda wake mwingi kuikuza tasnia hii ya mboga mboga na matunda. Makubaliano hayo ambayo tumeingia yatakuwa ni katika mfumo mzima wa usafirishaji wa mazao ya mboga mboga na matunda (cold chain management) ambayo itasaidia katika kulinda ubora wa mazao yetu. Hapa pia tunakuja na kitu kinaitwa green channel ambacho kitasaidia katika kusafirisha matunda hayo pasipo kikwazo chochote mpaka kufikia katika destination yake, kwa maana ya Airport au Bandarini. Tunafanya haya kwa ajili ya kulinda ubora wa mazao yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na vilevile ndugu zetu wa TARI tumekubaliana nao katika eneo lingine kubwa kabisa ambalo ni la kusaidiana kuanzisha miongozo maalum kwa ajili ya kuratibu zoezi la mazao ya mboga mboga na matunda ili tupate mwelekeo mmoja ndani ya nchi yetu ya Tanzania. Pia tunakwenda kujenga common use facility tatu ambazo zitajengwa katika Mikoa ya Kilimanjaro, Iringa na Dar es Salaam. Lengo lake kubwa ni kuhakikisha kwamba tunakuwa tuna collection center moja yakupokea parachichi au na matunda mengine kuya-grade na kuya-sort na mwisho wa siku ni kuhakikisha tunafikia lengo tulilojiwekea, la kwamba ifikapo mwaka 2030 tuwe tunauza mazao yetu ya matunda yenye thamani ya kufikia Dola bilioni mbili kutoka Dola milioni 750 ilivyo hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la mkonge tunajua kuna changamoto kubwa, na mimi nilikwenda mwenyewe nimetembelea kule Korogwe. Changamoto kubwa ya mkonge ni kwamba wakulima wa mkonge wanashindwa kuvuna mara mbili mkonge wao na unaoza shambani kwa sababu ya ukosefu ya korona. Nilitangazie Bunge lako, tumeshamuelekeza Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Mkonge kuhakikisha anatangaza zabuni ya kununua korona tatu kwa ajili ya wakulima wa mkonge kule Korogwe. Korona hizi zitasaidia pia kujibu swali la Mheshimiwa Mnzava juu ya ubora, tunatambua ya kwamba hivi sasa daraja la ubora wa Mkonge wetu wakulima wengi wanapata ile inayoitwa UG; lakini lengo letu ni wakulima waende katika 3L na 3S, watoke kwenye UG. Ukipata desiccator ambayo ni ya kisasa na bora itamsaidia pia mkulima kupata mkonge ambao unakidhi matakwa ya soko na ambao mkonge wa 3L and 3S una soko kubwa na bei yake ni kubwa zaidi kuliko ile ya UG na ile nyingine ya UF. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine pia ambalo tunalifanyia kazi ni la kuhakikisha kwamba tuna-diversify matumizi ya mkonge wetu, badala ya kujielekeza tu katika kutengeneza nyuzi na magunia, tumekaa na wenzetu Chama cha SAT na tumekubaliana waongeze pia wigo mpana wa matumizi haya ili kutafuta soko la uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkonge una uwezo wa kutengeneza dashboard za magari, cabin za ndege, milango na mkonge ukiuchakata vizuri una uwezo wa kutengeneza pombe kali ile aina ya Tequila. Kwa hiyo, tumezungumza nao kwa ajili ya ku-diversify kwenda katika eneo hilo pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumetoa maelekezo kama Wizara ya kwamba mazao yote ambayo yako chini ya Bodi zinazoshughulikia mazao, waanze kutumia magunia yatokanayo na mkonge. Lengo letu ni kuhakikisha kwamba tunaongeza soko kwa ajili ya mkonge wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine katika mkonge hapa ambalo nataka niligusie kwa haraka haraka ni eneo la nyuzi za nailoni za kufungia magunia ya mkonge. Tumekubaliana na wenzetu wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira kwamba sisi tumetoa maelekezo mazao yote ya kilimo, yatafungwa kwa kamba zitokanazo na mkonge na sio nailoni ili tuongeze soko la mkonge wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumejipanga pia kuja na Sheria ya Kilimo na Sheria ya Ushirika tunataka tuwalinde wakulima wetu tulinde maeneo yetu, tupate maeneo ya kilimo ambayo pia tutayapima na tutaya-gazette ili mwisho wa siku tuondoe migogoro ya wakulima na wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeboresha eneo la maabara yetu iliyopo Arusha ambayo inatusaidia kwa ajili ya mazao yanayokwenda nje ya nchi. Maabara yetu imetambulika, imepata ithibati na tumefunga mitambo ya kisasa. Hivi sasa mazao yanayotoka Tanzania yakitua pale Arusha hakuna mtu yeyote atayatilia mashaka. Kazi kubwa ambayo Mheshimiwa Rais ameifanya na investment kubwa ya mashine za kisasa na hivi sasa mazao yetu yanatoka pasipo changamoto yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni kazi kubwa ambayo imefanyika na tunaamini Waheshimiwa Wabunge mtatuunga mkono kwenye safari hii. Safari hii ndio tunaianza, tunaomba twende pamoja, mtuunge mkono, tunajua matokeo yatakuja baadaye, lakini kazi ndio tumeianza, mtuunge mkono, tuko tayari kwa ajili ya kuwatumikia Watanzania, kuifikisha Tanzania katika nchi ya ahadi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsanteni sana, Mwenyezi Mungu awabariki, naunga mkono hoja. (Makofi)