Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Abdulhafar Idrissa Juma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtoni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nikawa wa kwanza kuchangia katika bajeti hii muhimu sana kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu. Kwa sababu maendeleo yoyote ni usalama na hata matibabu mazuri yanatendeka vizuri pakiwa na usalama.

Mheshimiwa Spika, napongeza bajeti hii kwa namna ambavyo imesomwa na kwa namna ambavyo nayo imejielekeza pamoja ni masuala ya ulinzi lakini imejielekeza kutekeleza Ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi ambayo inasimamiwa na Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, napongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipongeze pia kwa namna ambavyo Jeshi letu limeendelea kukabiliana na baadhi ya changamoto ambazo zimekuwa zikijitokeza katika mipaka yetu. Katika moja ya kazi ngumu sana ambazo zinahitaji kujitolea mno ni kazi ya kuwa mwanajeshi. Daktari tunamhitaji pale tunapokuwa tunaumwa tu, tukishapona hatumuhitaji tena daktari. Lakini mwanajeshi ama jeshi letu tunalihitaji tukiwa wazima, tunalihitaji tukiwa tunaumwa, tunalihitaji tukiwa na uchumi imara na tunalihitaji uchumi wetu ukitetereka ili liendelee kudhibiti mipaka yetu tuendelee kuwa salama. Nalipongeza sana kwa namna ambavyo limekuwa likifanya vizuri katika kutimiza wajibu wao huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mimi nizungumzie kuhusiana na mahusiano baina ya majeshi yetu hasa Jeshi letu la Wananchi Tanzania na wananchi wanaokaa karibu na Kambi zao hasa zilizoko Mjini. Mimi hapa nataka nipongeze kupitia Kambi ya JWTZ ya Mwanyanya iliyokuwepo katika Jimbo langu la Mtoni. (Makofi)

Kambi ile imezungukwa yote na makazi ya watu, kambi ile ina mahusiano mazuri sana wananchi katika eneo lile na askari wetu katika Kambi ile wamekuwa ni mfano mzuri wa askari wengine katika Jeshi letu Tanzania nzima. Kambi ile imejitolea baadhi ya vitu ikachanga na wananchi ili watengeneze sehemu ya njia iliyoharibika. Jeshi pale lilitoa kokoto, jeshi lilitoa simenti, jeshi lilitoa mchanga wananchi na vijana wakajikusanya na sisi viongozi tukaongeza nguvu, wakamwaga zege katika eneo korofi ambalo linatumika na wananchi na wao askari wanalitumia kwa uchache sana. Napongeza sana nidhamu na uimara wa Jeshi letu katika kushirikiana na wananchi wetu katika kipengele hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukarimu huu wa Jeshi letu kushirikiana na wananchi umesababisha wananchi wengi katika Jimbo la Mtoni wanaoishi karibu na Kambi ile ya Mwanyanya kupenda kutumia Hospitali ya Jeshi iliyokuwepo katika Kambi ile. Sasa ombi langu kwa sababu ukarimu wao umetuvutia sana pamoja vituo vingine vya afya vilivyokuwepo, lakini tunapenda kutibiwa kwao, ukarimu na namna ambavyo wanatupokea basi naiomba Wizara hii katika fedha zake za kuboresha vituo vya afya vilivyopo katika majeshi na nyingine ipelekwe pale katika Kambi ya Mwanyanya ili pawe na vifaa vingi zaidi vya kuhudumia wananchi. Vifaa hivyo pale vikipelekwa vitahudumia wananchi.

Mheshimiwa Spika, mimi naomba nikwambie hatuendi pale pia kwa sababu hakuna Hospitali nyingine laa! lakini ni namna ambavyo Jeshi letu limekuwa na ukarimu na linawapa wananchi tiba sahihi. Kwa hiyo, naomba katika bajeti hii pamoja najua kuna mambo pale yanafanywa wakati mwingine linakarabatiwa taratibu naomba mtupelekee fedha katika kambi ile ikaboreshwe hospitali na katika hospitali nyingine zote. Hospitali zilizopo katika kambi zetu zinahudumia sana wananchi yawezekana kuliko majeshi tuliyokuwa nayo. Sasa mimi naomba hospitali ile iboreshwe, hospitali nyingine ziboreshwe na hospitali zote hasa ambazo Kambi zipo karibu na makazi ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba niendelee kulipongeza Jeshi letu, sisi tuko pamoja, bajeti yenu tutaipitisha kwa kishindo muendelee kulinda mipaka yetu, tuko pamoja nanyi na Mungu awajaalie kila kheri. Naunga mkono hoja. (Makofi)