Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Haji Amour Haji

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Makunduchi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. HAJI AMOUR HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami sina budi kukushuruku kwa kuweza kuniona kuchangia katika Bajeti hii ya Wizara ya Ulinzi wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, pili napenda kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ndiye Amiri Jeshi Mkuu wa nchi yetu katika ulinzi wa nchi yetu na vilevile Amiri Jeshi Mkuu ndiye mpambanaji wa mambo yote katika nchi yetu hii. Rais wetu ambaye ndiye Amiri Jeshi wetu Mkuu hatuna namna ya kuweza kumpongeza yaani inabidi tumpongeze kwa kiasi kikubwa sana maana yake haya yote ambayo anayoyafanya ni kutimiza wajibu wake na kutekeleza Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi hasa katika Sura 505 katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo inahusiana na Ulinzi.

Mheshimiwa Spika, pili tumpongeze Mkuu wetu wa Majeshi Ndugu Venance Mabeyo kwa umakini wake na uzalendo wake wa kipekee katika kuliongoza Jeshi letu la Tanzania na pia uzalendo wake wa kufanikisha nchi yetu hii kuwa katika hali ya amani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije katika mchango wa Wizara; moja katika jukumu la msingi la Wizara ya Ulinzi ni kuwapa vijana wa Kitanzania mafunzo ya awali ya kijeshi, ya stadi za kazi, utamaduni, uzalendo, umoja wa kitaifa na uwezo wa kujitegemea. Lakini mimi vilevile ningeongezea kitu kimoja ambacho ni uwezo wa kuzalisha mali, ambalo hilo ni moja ya jukumu lililokuwa katika moja ya Wizara. Sasa tuje katika uzalishaji mali huu nadhani kwamba Jeshi letu au Wizara yetu inafanya kazi kubwa sana ya kuweza kuwachukua vijana wetu kuwapa mafunzo pale ya stadi mbalimbali na vilevile kuwafundisha ukakamavu pamoja na uzalendo. Lakini bado tunatakiwa kwamba bado tuendelee kujiuliza katika haya mafunzo tunayowapatia vijana wetu je, bado yanakidhi katika uzalishaji mali katika nchi yetu. Maana yake lengo kujenga uzalendo, lengo ni kuwapa stadi, sasa mimi pengine ningeishauri Wizara pamoja na mambo ambayo tunayafanya huko maana yake wakapatiwa zile stadi mbali za kilimo, lakini pia tukawa na stadi za ufundi kama vilivyo vituo vyetu hivi vya mafunzo hivi vituo vya vocational ambako nako huko labda pengine tungeweza kujenga wigo zaidi ili vijana waweze kupata ule ujuzi ambao utakaoweza kuwasaidia. Watakapoweza kumaliza mafunzo wakaweza kujitegemea na kuweza kujiendeleza na tusiangalie tu kwamba suala la kuwapeleka vijana kule kujenga uwezo au kupata ukakamavu ikawa ndiyo sababu ya kwenda kuwachukua kwa kuwaajiri. Wao lengo kubwa maana yake twende kwa kuweza kuwaajiri na kuweza kujenga uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, pili, nije katika kuimarisha Ulinzi na Usalama wa nchi na mipaka yetu yaani katika suala la ibara ya chama chetu inazungumzia suala la ulinzi na usalama ambalo hilo lipo katika hali njema. Lakini muhimu zaidi ambayo nije vilevile katika kazi zinazotekelezwa kupitia fedha za maendeleo. Katika kifungu kimoja ambacho cha fedha za maendeleo kifungu (h) kinazungumzia kutatua migogoro ya ardhi kwa kupima na kufanya uthamini wa maeneo ya Mikoa kama Singida Kaskazini, Mkoa wa Mjini Magharibi na kulipa fidia kwa wananchi wa maeneo matano ambayo yametajwa pale katika fedha za maendeleo. Lakini katika ulipaji wa fidia zile maana yake kuna migogoro ambayo hii imeshazungumzwa, lakini migogoro…

SPIKA: Sekunde 30 malizia Mheshimiwa, kengele imeshagonga.

MHE. HAJI AMOUR HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika migogoro hiyo kuna baadhi ya maeneo sijaweza kuyaona pia kama Ndunga, pamoja na Udunga, Ubago pamoja na Unguja Ukuu. Ningependa au ningeshauri Serikali waweze kuliangalia suala hilo ili kuweze kutatua migogoro ya wananchi kwa ukaribu zaidi.

Mheshimiwa Spika, napenda kuunga mkono hoja Wizara yetu hii, ahsante sana. (Makofi)