Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye Wizara hii ya Ulinzi. Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu kwa kuona umuhimu wa kuongeza bajeti kwenye Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilipongeze sana Jeshi letu la Ulinzi wa Tanzania, kwa kweli wamekuwa ni kielelezo, wazalendo na wachapakazi. Jeshi letu linafanyakazi vizuri, lakini siyo tu kwenye masuala la ulinzi na usalama, wanatoa huduma za afya, lakini kwenye elimu, ujenzi na huduma nyingine za kijamii, hongereni sana makamanda wetu na wapiganaji wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina maeneo mawili naomba kuchangia; kwenye jimbo langu la Nachingwea kuna mgogoro wa muda mrefu wa ardhi baina ya wananchi na Jeshi letu. Jeshi linafanyakazi nzuri na kwa kweli tunaishi nao vizuri sana. Upo mgogoro kati ya 41KJ na 843KJ; mgogoro huu ni wa muda mrefu, aliwahi kuja aliyekuwa Waziri wa Ulinzi wa wakati huo ambaye sasa ni Rais wa Zanzibar na alitoa maelezo, alizungumza na wananchi akasema watalipwa. Lakini baada ya muda alikuja afisa mwingine kutoka Makao Makuu ya Jeshi, akasema hawatalipwa ardhi badala yake watalipwa yale maendelezo waliyoyafanya kwenye ile ardhi. Wananchi wale kwa upendo mkubwa na jeshi na mahusiano mazuri waliridhika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya muda alikuja afisa mwingine kutoka Makao Makuu ya Jeshi, akaongea na wananchi hawa tena akasema hakuna malipo mengine yatakayofanyika, si yale ya ardhi wala si yale ya maendelezo. Hawa wananchi wana mapenzi mazuri na tunaishi nao vizuri sana hawa wanajeshi na kati ya huduma za afya ambazo zinatolewa vizuri ni kwenye Hospitali Kuu ya Jeshi Majimaji Nachingwea, wanafanyakazi nzuri na wananchi wakawaida wanakwenda kupata huduma hapo. (Makofi)

Sasa niiombe sana Wizara ione umuhimu wa kuondoa changamoto hii kwa haraka ili wananchi hao waweze kujua hatima yao. Hawana maneno wananchi hawa, wapo tayari kupokea maelekezo yoyote ambayo yatatolewa na Serikali. Kwa unyenyekevu mkubwa naiomba sana Wizara ili hao wananchi waweze kujua hatima yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna shule ya sekondari Farm 17; eneo hili ni la Jeshi lakini kielelezo cha kwamba tuna maisha mazuri, tunaelewana vizuri na wanajeshi, jeshi wametupa Halmashauri eneo hili tulitumie kama shule ya sekondari. Eneo hili ni muhimu na sisi tunahudumia zaidi ya kata tatu wanatumia hii shule ya sekondari.

Sasa ombi langu, eneo hili sasa niiombe sana Serikali, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, mfikirie kutuachia, kwa sababu kwa sasa tukitaka kufanya miundombinu ukarabati ni lazima tupate kibali kutoka jeshini. Eneo hili tukilipata, mkituachia rasmi, mkitukatia eneo hili ambalo linazunguka shule tutawashukuru sana ili tuweze kuboresha miundombinu na wananchi wa maeneo yale waweze kupata huduma bora kwa ajili ya kupata ile elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kumpongeza tena Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya ameingia kwa kweli tunaona Wizara hii inamelemeta. Nakushukuru sana. (Makofi)