Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kuwapongeza kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya ya kuwalea vijana lakini kuwajenga katika kulitumikia taifa lao, katika uzalendo wa Taifa lao, lakini kwa sasa kuwatengeneza katika mazingira ya kujitegemea kwenye uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kumshukuru kwa moyo wa dhati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, lakini pia kumpongeza na kumshukuru Mkuu wetu wa Majeshi kwa namna ambavyo waliweza kuwalea, kuwachukulia vijana kwamba wanaweza wakakosea, lakini wakaendelea kulelewa vijana wale ambao walifukuzwa kambini na leo wamerudishwa, tunaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika vijana wale walifanyakazi kubwa sana ya ujenzi wa miradi mbalimbali katika nchi yetu. Lakini ninaombi kwa Mheshimiwa Waziri, nakuomba sana, wapo vijana ambao walikuwa kwenye kambi ya Ukonga wao walitumika kabla ya wale ambao walikwenda kujenga ukuta wa Ikulu na Mererani. Vijana wale walishiriki kujenga maeneo mbalimbali, wamejenga Bwawa la Umeme Rufiji, wamejenga ujenzi wa Chuo cha VETA Lindi; Chuo cha Ualimu Kigoma; Bandari Kavu Kwala; Ofisi ya Manispaa Kinondoni; majengo mapya Mzumbe na maeneo mbalimbali katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini baada ya kazi kubwa hiyo yote vijana ambayo waliifanya, vijana wale waliweza kuchukuliwa na kurudishwa Mgulani na baada ya hapo wakatawanyishwa kurudi majumbani na sasa vijana wale wapo tu majumbani wamekaa. Lakini tunaiomba sasa Serikali, tunaiomba sana Serikali iweze kuwafikiria vijana wale kwa jicho la pili kwa sababu ni hazina kwa taifa letu kwa kuwa wamepata ujuzi mbalimbali ujuzi wa kijeshi lakini na ujuzi pia wakuweza kujiwezesha wao wenyewe kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii pia Wizara hii inawatengeneza vijana vizuri sana katika kwenda baadaye kujiajiri. Wanajengwa katika kilimo, ufugaji, uvuvi, lakini baada ya hapo pamoja na Serikali kwamba imewekeza nguvu kubwa kwa vijana hawa, vijana hawa wanaondoka wanakwenda kuwa hawana tija kwa sababu hawana uchumi mwingine ambao unawawezesha kuweza kuendeleza ule ujuzi wao ambao wamepata wa kilimo, lakini pia uvuvi pamoja na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, JKT inafanya mausala ya kilimo, tumeweza kuambiwa hapa pale Chita mwaka jana walilima kilimo cha mpunga, walitumia fedha nyingi sana kuwekeza, lakini hatima yake faida waliyopata ni ndogo kuliko fedha ambayo wamewekeza. Niombe sasa waweze kuwafikiria vijana wale ambao wanawapatia mafunzo wanapotoka kwa sababu bado Jeshi lina maeneo makubwa vijana hawa kwa sababu wana ujuzi na Serikali iweke mkono wake hapa. Ofisi ya Waziri Mkuu ina mikopo mbalimbali ya kuwawezesha vijana, tuone wanawezaje kuwawezesha vijana hao kwa sababu wana ujuzi wanapokuwa wametoka waandaliwe kwenye kilimo ili wanapolima wao, jeshi hili linajua kwamba sisi tunalima hapa mpunga, lakini tuna vijana pembeni ambao wanazalisha na wataleta kwenye jeshi ili tuweze kuunganisha nguvu ya pamoja na hatimaye jeshi hili katika upande wa kilimo liwe lina tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini halikadhalika, niombe jeshi letu hili linafanyakazi kubwa sana ya kuwaanda vijana, basi lisijifungie liweze kuunganisha nguvu na Wizara ya Kilimo kwa sababu tayari tunaona Wizara ya Kilimo imeshatoa fursa kwa vijana na vijana hawa tayari wameshaandaliwa siyo vijana tena wa kwenda kuanza kuwafundisha. Lakini Wizara ya Viwanda na Biashara ili vijana hawa waweze kupatiwa fursa ya masoko pale ambapo watakuwa wamepewa mitaji na kuweza kuwajenga vijana vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vijana wale ambao niliwaongelea mwanzo walikuwa chini ya Kanali Ashraf Bakari Hassan. Niendelee kusisitiza kwamba tuone vijana wale waangaliwe kwa jicho la pili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa inafanyika Kikosi cha Mizinga, tuombe sasa nguvu kubwa ipelekwe kule ili kuweza kuendeleza vipaji vya Watanzania vya kuweza kutengeneza vitu mbalimbali na vikaweza kutusaidia sisi wenyewe bila ya kutumia gharama kubwa ya kwenda kuagiza vitu nje ya nchi. Jeshi letu lipo vizuri sana ni kiasi tu cha kuwezeshwa ili waweze kutenda miujiza, kutenda maajabu ambapo itasaidia sana kupunguza gharama ya hivyo vitu ambavyo tunaviagiza kutoka nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)