Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kutoa mchango wangu katika Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyetujalia kufika siku ya leo tuko ndani ya jengo hili tukiwa na afya njema na uhai.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa hotuba nzuri ambayo ina mipango inayoonesha dhamira ya dhati. Kuna Mbunge alizungumza jana akasema kwamba zaidi ya asilimia 46 ya bajeti ya maendeleo kwenye bajeti kuu inakwenda katika Wizara hii ya Ujenzi. Baada ya kupitia kitabu nimeona pesa nyingi imekwenda huku kuna sababu maalum ya kulipia madeni ya wakandarasi. Dawa ya deni ni kulipa na inaonesha ni jinsi gani Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga vizuri kuwalipa wakandarasi hawa ili waendelee kujenga zaidi barabara zetu na kufungua milango ya uchumi katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mbunge mmoja jana ametoa takwimu nyingi sana kuilaumu Serikali kwa kusema kwamba pale bandarini mizigo imepungua, mizigo inayoenda Malawi, Zambia, Congo lakini amesahau kusema jambo moja tu kwamba pamoja na kupungua huko lakini mapato yameongezeka. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali pamoja na kwamba mizigo inapungua lakini mapato yameongezeka. Hii maana yake ni kwamba imedhibiti uvujaji wa mapato na hapa tunajali ubora na sio uwingi, bora kiingie kichache lakini tunakusanya zaidi. Hii inatuhakikishia kwamba sasa barabara zetu ambazo tulikuwa tunaomba na zinapitishwa na Bunge lakini pesa hazipelekwi sasa zitapelekwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo kwa Serikali nitoe angalizo tu, wenzangu wamezungumza lakini na mimi nisisitize kwamba Bunge hili kazi yake ni kuisimamia na kuishauri Serikali. Tunapitisha hizi bajeti, lakini tunategemea hizi bajeti zitakwenda kwa wakati ili bajeti hii itekelezwe ili tuendelee kuaminiwa na wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, natoa mfano mmoja tu katika Jimbo langu, bajeti zilizopitishwa mwaka jana kwa ajili ya matengenezo ya kawaida tu barabara ya Bigwa - Kisaki, Madamu - Kinole mpaka leo pesa hizo hazijafika na barabara hazijaanza kutengenezwa. Hiyo ni bajeti ya mwaka jana na tumebakiza mwezi mmoja na nusu kumaliza muda wa bajeti ya mwaka wa fedha.
Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi ni vizuri mipango ambayo mmeileta hapa na tunaipitisha kuhakikisha kwamba inatekelezwa ili tuendelee kujenga uhalali wa kuongoza nchi hii miaka mingi ijayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kuhusu msongamano wa Dar es Salaam, Mbunge mwenzangu kutoka Morogoro kaka yangu Mheshimiwa Saddiq alivyozungumza lakini amesema mkoa wowote lakini mikoa ambayo ina nafasi kubwa ya kuwa na bandari kavu kama alivyosema ni Pwani au Morogoro, lakini Morogoro una nafasi kubwa zaidi ya kuwa bandari kavu kwa sababu zifuatazo:-
Kwanza, kijiografia inaunganishwa na kanda zote, Kanda ya Kati, Kusini na Kaskazini. Kwa hiyo, tukiweka bandari kavu pale itatuondoshea msongamano kule Dar e Salaam na kufanya shughuli kutekelezeka kirahisi. Pia tutafungua milango ya kiuchumi kwa mkoa wa Morogoro na mikoa mingine ya jirani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijielekeze katika Jimbo langu katika Wilaya yangu ya Morogoro Vijijini. Wilaya ya Morogoro Vijijini hususani Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki, siasa kubwa katika jimbo lile sasa hivi imekuwa ni barabara hususani barabara ya Bigwa - Kisaki. Ni barabara ya muda mrefu, Rais wa Awamu ya Nne alitoa ahadi 2005 kwamba itajengwa kwa kiwango cha lami akiwepo Waziri wa Ujenzi ambaye sasa hivi ndiye Rais aliyeko madarakani. Mwaka 2010 tena Rais, Dkt. Jakaya Kikwete akatoa ahadi ya kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami. Pia mwaka 2014 alipokuja kutuaga watu wa Morogoro Vijijini akiambatana na Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi ambaye sasa ni Rais aliyeko madarakani, Dkt. John Pombe Magufuli akaahidi tena kwamba hii barabara itajengwa kwa kiwango cha lami. Barabara hii sijaiona katika kitabu hiki, namwomba sana Mheshimiwa Waziri akija katika majumuisho yake atupe matumaini ahadi hii ya Rais itatekelezwa lini kujengwa kwa kiwango cha lami barabara?
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ni muhimu sana kwani inaunganisha mkoa wa Morogoro pale Kisaki na mkoa wa Pwani kupitia Wilaya ya Rufiji. Pia inakwenda katika mbuga ya Selous, lakini ndiyo barabara pekee katika Mkoa wa Morogoro ilikidhi vigezo vya MCC. Hii ndiyo barabara iliingia katika mradi wa MCC. Kama Wamarekani waliona barabara hii ni muhimu naamini kabisa Serikali yetu ya Awamu ya Tano itaona ni muhimu zaidi na itaitekeleza haraka sana kwa kuijenga kwa kiwango cha lami. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji mradi huu ulikuwa chini ya MCC. Namwomba Waziri akija atupe matumaini baada ya hao MCC kuleta madoido na kuweka pembeni Serikali ina mpango gani kuchukua jukumu hilo na kuimalizia kwa kiwango cha lami. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye suala la kupandisha hadhi barabara ya kutoka Ngerengere - Mvuha kuwa ya mkoa.
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.