Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika kuendeleza ulinzi na usalama wa Taifa letu, na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness).

Mheshimiwa Spika, ulinzi na usalama ni mojawapo ya nguzo kuu katika kuongeza imani kwa wawekezaji hasa wa kutoka nje (FDI). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni “kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.”

Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio makubwa ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, bado kuna wapiganaji wetu ambao ni wastaafu na wengine walishiriki kwenye vita kwa kulinda mipaka yetu hususani vita ya Kagera, wanalalamikia stahiki zao kutolipwa kikamilifu. Kwa kuzingatia kuwa wamefanya kazi kwa uzalendo mkubwa na iwe motisha kwa askari wetu wote kwenye majeshi yetu yote, napendekeza Serikali iangalie jinsi ya kutatua changamoto hii na kuangalia upya stahiki zao ikiwemo kuboresha mafao ya pensheni zao.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Wizara ya Ulinzi kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu kuangalia jinsi ya elimu ya ulinzi na usalama kuunganishwa kwenye mitaala ya elimu. Pia Serikali iendelee kuboresha mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa ikiwemo mafunzo ya uzalendo na ujasiriamali. Kutokana na mafaniko makubwa huku nyuma ya mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria, Serikali irudishe utaratibu wa mafunzo hayo kwa miezi kumi na mbili na mafunzo haya yawe maandalizi ya kuwajenga vijana kwenye uzalendo na ulinzi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.