Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na watendaji wake kwa kazi nzuri wanazofanya kuilinda nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Ulinzi wa Taifa ya mwaka 1966 Sura 192 na Sheria ya JKT ya mwaka 1963 Sura 193, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imekabidhiwa jukumu la kusimamia Jeshi la Wananchi wa Tanzania na Jeshi la Kujenga Taifa katika kutekeleza majukumu yake.

Mheshimiwa Spika, Wizara hii ina wajibu wa kuvipatia vyombo hivi mahitaji yake ya kimsingi ili kuviwezesha kutekeleza majukumu hayo. Katika hili, bado baadhi ya wanajeshi wetu hawajapatiwa huduma ya msingi ya kupatiwa nyumba za kuishi na walio wengi kuishi uraiani.

Mheshimiwa Spika, katika maeneo mengi duniani huwezi kumkuta mwanjeshi akipanga kwenye nyumba uraiani. Hii imewasaidia kuwajenga kisaikolojia askari wao na kutanguliza utaifa kwanza kutokana na Serikali zao kuwawekea mazingira bora ya kuishi pamoja.

Mheshimiwa Spika, ninapendekeza wanajeshi wetu wote wajengewe mazingira bora na familia zao kwa kujengewa makazi na kuishi kambini. Kwa kufanya hivi, hii itarahisisha kufuatilia nyendo zao na kusimamia maadili yao ya kazi za kijeshi. Vilivile, wakikaa pamoja kambini itarahisisha kuwapatia huduma muhimu kama maji, umeme, tiba na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Ulinzi wa Taifa ya mwaka 1966, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ina majukumu ya kulinda mipaka ya nchi yetu na kuandaa umma wa Watanzania kushiriki katika shughuli za ulinzi wa Taifa.

Mheshimiwa Spika, ili kufanikisha azma hii, ninapendekeza Jeshi la Wananchi wa Tanzania lieendelee kutoa mafunzo ya ulinzi ya kimkakati wa mgambo kama sehemu muhimu ya jeshi la akiba. Napendekeza mafunzo haya yawe ni lazima kwenye mikoa yote inayopakana na nchi jirani.

Mheshimiwa Spika, uzoefu tulioupata kwenye vita inayoendelea kati ya Urusi na Ukraine imeonesha kwamba jeshi la akiba linalohusisha wananchi wa rika mbalimbali huko Ukrane limetoa mchango kubwa kukabiliana na Taifa kubwa la Urusi lenye uwezo mkubwa wa kivita na silaha za kisasa.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.