Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, tunamshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa majaliwa yake kwetu sote na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, ninaipongeza sana Serikali yetu chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na viongozi wetu wakuu na watendaji wote Serikalini. Kwa namna ya pekee nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Stergomena Tax, Waziri wetu wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, pamoja na wakuu wote wa vyombo vya ulinzi kwa kuendelea kuitunza na kuilinda heshima ya kulinda mipaka ya Taifa katika nyanja za kitafa, kikanda na kimataifa. Rai yetu kwa vyombo vyetu waendelee kudumisha utii, uzalendo, ukakamavu, weledi na utaifa kwanza. Kwa kweli wanatuheshimisha mbele ya mataifa, hongereni sana Mwenyezi Mungu awabariki.

Mheshimiwa Spika, aidha niungane na Watanzania wote kukupongeza sana wewe Spika wetu na waheshimiwa Wabunge, viongozi wote waliochaguliwa na walioteuliwa kwenye nafasi zao mbalimbali tunawaombea kwa Mwenyezi Mungu aweze kuwajalia kufanikisha majukumu yenu.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nitoe mchango wangu kupitia hotuba ya Wizara hii muhimu sana kwa mustakabali wa Taifa letu; kwanza kutokana na umuhimu wa ujenzi wa Makao Makuu ya JWTZ Kikombo, Dodoma, tunaiomba sana Serikali itoe fedha za kukamilisha ujenzi huo. Hata hivyo tunaipongeza sana Serikali kwa kutumia mfumo wa force account kwani kutokana mfumo huu umeisaidia sana Serikali kuokoa gharama kubwa za fedha katika ujenzi huo.

Mheshimiwa Spika, tunaishauri Serikali iangalie vyombo vyetu vingine vya ulinzi ili wawezeshwe kupata fedha za kutumia kujenga miradi ya maendeleo na miundombinu mingine kama vile magereza, vituo vya polisi, ofisi za mikoa na wilaya.

Pili, Serikali iangalie mpango wa kuwezesha upatikanaji wa fedha za kutosha, vitendea kazi, wataalam, kwenye mashirika ya NYUMBU, MZINGA na SUMA JKT ili mashirika hayo ambayo yana dira ya uzalishaji mali yaweze kutanua matawi ili kuongeza wigo wa ajira kwa vijana wote wanaomaliza mafunzo ya JKT na kuzalisha bidhaa ambayo zitakidhi haja kwenye masoko ya ndani ya nchi na nje.

Tatu, kutokana na ongezeko kubwa la idadi ya watu katika mji wa Ddodoma hali itakayochochea mahitaji makubwa sana ya huduma za jamii hususan sekta ya afya, tunaiomba sana Serikali yetu ijitahidi sana kutoa fedha za ujenzi wa Hospitali ya Jeshi hapa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, nne, kutokana na mabadiliko ya teknolojia kubwa sana duniani, tunaiomba sana Serikali iongeze bajeti ya Wizara hii katika nyanja za vifaa vya ulinzi na mafunzo ya muda mfupi, muda wa kati na mrefu ili kuongeza medani za kisasa zaidi katika ulinzi wa mipaka yetu na Taifa letu kikanda, kitaifa na kimataifa.

Mheshimiwa Spika, mwisho siyo kwa umuhimu naendelea kuvipongeza sana vyombo vyetu vya ulinzi katika utendaji wao.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na naomba kuwasilisha.