Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Dr. Stergomena Lawrence Tax

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, muda mchache uliopita niliwasilisha katika Bunge lako tukufu hotuba ya bajeti ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kuhusu makadirio na mapato na matumizi ya mwaka wa fedha 2022/2023. Napenda kukushukuru kwa namna ulivyosimamia na kuongoza kwa umakini mjadala wa bajeti ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. (Makofi).

Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge waliochangia kwa kuzungumza, sina uhakika kama waliopo wamechangia kwa maandishi, lakini kama wapo hoja tutazipokea na tutazifanyia kazi, kwa hoja nzuri zitakazochangia katika kuimarisha utendaji na ufanisi wa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie kuwa maoni na ushauri wenu tumeuchukua na tutaufanyia kazi ili kuendelea kuboresha utendaji wa Wizara yetu na kutatua changamoto ambazo mmeziainisha. Wizara inatambua na kuthamini michango iliyotolewa ambayo imetolewa kwa nia njema iliyotawala mjadala na msingi wake ni kuboresha shughuli za utendaji wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kuishukuru kwa dhati Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Vita Rashid Kawawa, Mbunge wa Namtumbo na Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Vincent Mbogo, Mbunge wa Nkasi Kusini na Wajumbe wote wa Kamati kwa maoni na ushauri waliotupatia. Ushauri tumeupokea tumeuzingatia, iliwasilishwa kwa muhtasari, lakini tumekwishaipata hiyo hotuba, kwa hiyo, tutafanyia kazi yale yote yaliyomo kwenye maoni mliyoyatoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upekee napenda niwapongeze watendaji wote wa Wizara na taasisi zake wakiongozwa na Katibu Mkuu, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe, kwa upande wa Wizara na Jenerali Venance Salvatory Mabeyo kwa upande wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kwa kufanya kazi kwa weledi na kujituma na kuwezesha kufikia hatua hii ambapo tunaelekea kuhitimisha mjadala wa bajeti ya Wizara yetu. (Makofi)

Naomba kuwatambua Waheshimiwa Wabunge waliochangia hotuba ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa ujumla wao ambao katika mjadala wa asubuhi hii Waheshimiwa Wabunge 16 wameweza kuchangia. Asanteni sana Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na ufinyu wa muda napenda kuwahakikishia kuwa maelezo na majibu ya kina kuhusu hoja zote na michango yote iliyotolewa yataandaliwa kwa maandishi na kila hoja itajibiwa na tutawasilisha Ofisi ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo ya utangulizi naomba nitoe ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge wakati wakichangia hotuba niliyoiwasilisha leo. Naomba nijikite katika hoja chache, kama nitaweza nitajibu zote ambazo kwa sehemu kubwa zimetawala mjadala wa hotuba ya Wizara yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze tu kwa kusema kwamba Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania tangu kuanzishwa kwake hapo tarehe 01 Septemba, 1964 limeendelea kukua na kuimarika kizana, kinyenzo, kiteknolojia na kiweledi kulingana na mahitaji ya wakati. Hali hii imeliwezesaha jeshi letu kutekeleza majukumu yake kwa umahiri mkubwa na kuiwezesha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuendelea kuwa na amani na usalama hata pale ambapo pamekuwa na matishio, matishio hayo yamedhibitiwa ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, nalijibu hili kutokana na msisitizo mkubwa ambao mmeutoa Waheshimiwa Wabunge pamoja na Kamati kwamba Jeshi letu na taasisi zake halina budi kuongezewa nyenzo, halina budi kuongezewa rasilimali fedha na niwahakikishie tu kwamba hii imekuwa ni dhamira ya Serikali na Serikali imeendelea kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, pongezi nyingi zimetolewa kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Awamu ya Sita na Amiri Jeshi Mkuu, na ni kweli ametoa uzito mkubwa sana kuhakikisha kwamba Jeshi letu linawezeshwa na taasisi zote. Kwa hiyo, pongezi zote ambazo mmezitoa mafanikio yote ambayo yametolewa naomba pongezi hizo ziende kwa Amiri Jeshi wetu Mkuu ambaye ametoa uzito stahiki, Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu hoja iliyotolewa na Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na Waheshimiwa Wabunge wamechangia pia kuitaka Wizara kuhakikisha kuwa miundombinu ya kiulinzi mipaka kwenye Kamati wamesema pia mpaka katika mwambao wa bahari inaimarishwa napenda kulihakikishia Bunge lako tukufu kuwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania tangu kuanzishwa kwake limeendelea kuwezeshwa kivifaa kama nilivyosema kizana na kiteknolojia kulingana na mabadiliko yanayotokana duniani. Ni dhamira ya Serikali kuendelea kuliwezesha Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania ipasavyo. Aidha, Wizara imeupokea ushauri huu muhimu na Serikali itaendelea kutoa kipaumbele katika eneo hili mahsusi kwa ulinzi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa maelezo mafupi kuhusu hatua iliyofikiwa katika maandalizi ya Sera ya Ulinzi wa Taifa, hili pia limezungumzwa kwa nguvu sana na Mheshimiwa Saada nadhani naomba tu nitoe maelezo kwamba mchakato wa Sera ya Ulinzi wa Taifa ulianza mwaka 2008 ni kweli kama mlivyosema Waheshimiwa Wabunge kwamba mchakato huu ulianza muda mrefu sana. Hata hivyo sera hii ilichelewa kupata maoni kutoka kwa baadhi ya wadau muhimu, baada ya kupata maoni toka pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hii ilikuwa ni mwaka 2021 baada ya kupokea maoni hayo ilibainika pia kuwa yamekuwwepo maendeleo ya kitaifa na kimataifa katika sekta ya ulinzi yanayohitaji kuzingatiwa.

Mheshimiwa Spik,a mwaka 2008 na mwaka 2021 ni muda mrefu sana kwa hiyo ilibidi kuirejea hii sera upya. Kwa hiyo kazi hii imekwishafanyika na rasimu iko tayari kwa hiyo sasa hivi kinachoendelea ni kuhakikisha tunakamilisha sera hii na kwa umuhimu wake sera hii inakamilishwa kwa pamoja na Mkakati wa Usalama wa Taifa na Mkakati wa ulinzi wa Taifa letu. Kwa hiyo mpango tulionao tunatarajia kwamba katika mwaka huu wa fedha 2022/2023 Sera hii itaweza kuwa imekamilika Wizara imetoa kipaumbele kikubwa sana kwa sera hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia kutoa ufafanuzi kuhusu umuhimu wa kuliwezesha Jeshi ikiwa ni pamoja na taasisi zake ikiwemo NYUMBU na ikiwemo Shirika la MZINGA kirasilimali fedha na watu. Kama ilivyo kwa taasisi nyingine Jeshi na taasisi zake zinahitaji rasilimali fedha na zinahitaji rasilimali watu ili kuweza kutekeleza majukumu yake ya msingi ya kuilinda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mipaka yake, kufanya tafiti na ubunifu, lakini pia kuzalisha mazao ya msingi.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema wakati nikiwasilisha hotuba asubuhi hii nilieleza wazi kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan ambaye ni pia ni Amiri Jeshi Mkuu imetoa uzito sana katika sekta ya ulinzi na kwa muktadha huu katika bajeti ambayo nimeiwasilisha tumepata ongezeko la shilingi 53,754,747,000 ikiwa ni sawa na 15% kama ambavyo pia ilielezwa na Kamati ya Bunge wakati ikiwasilisha taarifa yake ambapo Wizara imepata ongezeko la 14%; Ngome imepata ongezeko la 16%; na JKT imepata ongezeko la 10%. Pia kuhusu rasilimaliwatu tayari tumekwishapata vibali vya kuandikisha askari na kuajiri watumishi wapya katika mwaka wa fedha 2023 kwa hiyo hii itatusaidia kuziba pengo ambalo mmelisisitiza Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mashirika ya NYUMBU, TATC na MZINGA pamoja na kutoa fedha kwa ajili ya kununua mitambo mashine na malighafi jitihada zinaendelea ili kuhakikisha kuwa mashirika haya yanawezeshwa kikamilfu ili kutimiza azma ya kuanzishwa kwake. Kwa kutambua umuhimu wa Shirika la TATC ambayo ni NYUMBU inavyoeleweka zaidi mpango wa maendeleo wa miaka 15 ambao ulirejewa wa kuliimarisha Shirika la NYUMBU utaanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha huu 2022/2023 na kiasi cha shilingi 20,445,970,300 tayari kimeshatengwa. Kwa hiyo, hii inaonesha kwamba mawazo yenu, maoni yenu Kamati imesema kwamba imekuwa ikitoa maoni haya kwa muda mrefu yamezingatiwa na sasa mpango uliopitishwa unaenda kutekelezwa.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mpango huu utakuwa na manufaa makubwa ikiwa ni pamoja na kupunguza gharama za uagizaji wa magari, zana, mitambo na vipuri na kukuza uwezo wa nchi katika utafiti na wa teknolojia za magari na mitambo jambo ambalo ni muhimu sana kwa Taifa lolote kuweza kujitegemea katika sekta hii.

Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ametoa uzito lakini naomba ninukuu kauli yake katika hili ambapo amekuwa akisema kwamba; “yajayo yanafurahisha.” Kwa hiyo naomba tu tujipe muda tufanye huu utekelezaji na hayo yajayo yanayofurahisha mtayaona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine iliyoibuliwa na Waheshimiwa Wabunge ni kuhusu umuhimu wa utekelezaji wa miradi ya kilimo cha kimkakati hususan huko Chita na shamba la Mgeta, Mkoani Morogoro na msisitizo umewekwa katika kukamilisha ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji. Miradi hii ni muhimu sana kwa Taifa na kwa maono mapana kama ambavyo ilivyoelezwa unazo faida nyingi ikiwa ni pamoja na kuipunguzia Serikali gharama za kuwalisha vijana, kuchangia katika usalama wa chakula na moja ambalo halikusemwa na pia mradi huu miradi hii inatarajiwa kuchangia katika upatikanaji wa mbegu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri wa Kilimo jana alivyokuwa akitoa hotuba yake alisisitiza pia kwamba umuhimu wa mbegu ni kitu muhimu sana ili kuhakikisha kwamba unachangia katika upatikanaji wa chakula wa Taifa lakini na usalama wa chakula wa Taifa letu. Kwa hiyo, hili pia miradi hii itachangia katika hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu huu Serikali imeendelea kutenga fedha toka vyanzo vya ndani, lakini pia tunatafuta mikopo kwa ajili ya kuendeleza miradi hii na Mheshimiwa Waziri wa Fedha anatusaidia katika hilo. Kama nilivyosema utekelezaji wa miradi hii ya kimkakati utaliwezesha Jeshi la Kujenga Taifa kujitosheleza kwa chakula na hatimaye kuimarisha usalama wa chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la utatuzi wa migogoro ya ardhi limejitokeza kwa kiasi kikubwa katika mjadala; napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge na Bunge lako tukufu kuwa Wizara imetoa kipaumbele kikubwa katika utatuzi wa migogoro ya ardhi baina ya Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania na wananchi na nina imani sote ni mashahidi tumeiona kazi kubwa inayoendelea. Hadi sasa utekelezaji wa mpango huo wa miaka mitatu unaendelea kwa ufanisi wa hali ya juu. Kazi hii ni sehemu ya timu za Wizara nane ambayo timu hii iliundwa na Mheshimiwa Rais lakini inasimamiwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu kama alivyoeleza asubuhi ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpango huo umejumuisha migogoro 87 na mpaka sasa migogoro 58, maeneo 58 yamekwishapimwa na kuwekewa mipaka kwa sababu suala la mipaka limesisitizwa sana na maeneo 17 yamefanyiwa uthamini na kati ya yaliyofanyiwa uthamini maeneo tisa yameshalipiwa fidia na asubuhi niliyataja sita, lakini tisa ni kwa ujumla wake tangu tumeanza kutekeleza. (Makofi)

Kwa hiyo yaliyosalia yanaendelea ikiwa ni pamoja na maeneo yaliyoongelewa leo hapa na Mheshimiwa Haji Amour Haji na Mheshimiwa Saada Mansour na Mheshimiwa Kirumbe Ng’enda na Mheshimiwa Hawa Mchafu yote haya yamejumuishwa katika mpango huu katika yale ambayo yanaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Hawa Mchafu amenitaka nimpe taarifa ya task force hatua iliyofikiwa nimuombe tu kumuhakikishia Mheshimiwa Mchafu kwamba kazi hii tayari ripoti imeshawasilishwa nipatie tu muda niende niipitie ripoti hii na tutawasiliana tuone jinsi tutakavyo kamilisha zoezi hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo napenda kuwashukuru viongozi wote na wananchi katika maeneo mbalimbali kwa ushirikiano mkubwa uliowezesha Wizara kutatua changamoto hizo. Aidha, niwapongeze maafisa na watumishi wa Wizara wengine wametajwa humu kwa kazi kubwa waliyoifanya katika kutatua migogoro hii.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada za dhati za kutatua migogoro hii ambazo ni shirikishi nawaomba sana wananchi watambue umuhimu wa maeneo tunayohitaji kama Jeshi la Kujenga Taifa na pale ambalo tunahitaji kuchukua maeneo haya basi tushirikiane tuweze kupata maeneo haya, lakini pale ambapo maeneo yamekwishachukuliwa tuwaombe sana wasirudi kwenye maeneo haya. Kwa kufanya hivyo ni hatari kwao lakini pia ni kuzusha migogoro mipya. Kwa hiyo tushirikiane wote tuweze kwa kutoa elimu hii ili wote tuweze kutatua tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo limejitokeza ni uboreshaji na kuongeza makazi ya wanajeshi; hili ni suala muhimu sana na tunalipa uzito unaotakiwa naomba tu kulijulisha Bunge lako tukufu kuwa Wizara inaendelea na utekelezaji wa mpango wa nyumba 10,000 kwa wanajeshi na hadi sasa nyumba 6,064 zimeshajengwa katika mikoa mbalimbali. Mpango uliopo ni kukamilisha hizo takribani 4000 zilizobaki na kuongeza zaidi pamoja na kwamba katika mwaka huu hatukuweza kutenga fedha, lakini bado tunaendelea kutafuta rasilimali ili kuhakikisha kwamba tunaongeza nyumba kwa ajili ya makazi ya wanajeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia kwa niaba ya watumishi wote kabla kulikuwa na hoja zingine chache ziizoletwa ambazo nyingine amenisaidia kuzijibu Naibu Waziri namshukuru sana kwa hilo, lakini nilipenda kuongelea suala la kuajiri vijana, alitoa hoja kwamba kuna vijana walifanya shughuli mbalimbali, lakini hawakuweza kuchukuliwa.

Nipende tu kuwafahamisha kwamba naimesemwa vizuri sana nafikiri na Mheshimiwa mmoja kwamba sababu kubwa ya kuwachukua vijana kwenda JKT ni kuwajengea stadi na hivyo ndivyo tunafanya na imeongezwa kwamba tuwajengee ufundi, hata hilo linafanyika. Kwa hiyo wanapokwenda JKT kinachotarajiwa pale ni kwamba wanajengewa stadi na baada ya pale waweze kwenda kujitegemea.

Kwa hiyo si rahisi kuweza kuwachukua vijana wote wanaokwenda JKT waende kuajiriwa kwa sababu kwanza hilo siyo lengo, lengo ni kuwapatia stadi lakini ushauri mzuri kabisa tumeupokea wa Mheshimiwa Asia Halamga na pia huu ulitolewa na Mheshimiwa Haji Amour kwamba pamoja na hayo tuweze kujaribu kuunganisha nguvu kama Wizara ya Kilimo na Wizara ya Viwanda kuona kwamba baada ya hapo tunawafanyia nini. Nipende tu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba hili tayari tunalifanyia kazi, tayari nimekwishaongea na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na jana wakati akiwasilisha hoja yake moja ya eneo tuliloona tunaweza kulifanyia kazi mara moja ni kwenye upungufu wa sekta ya mafuta. Alieleza hapa kuna ukwasi mkubwa sana, kwa hiyo, tunataka tuone kwamba tunaweza kujumuisha nguvu zetu namna gani na kuwatumia hawa vijana wakaweza kushiriki katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia mazungumzo yanaendelea tuone kwamba na Wizara ya Viwanda tunaweza kushirikiana nao namna gani. Ushauri tumeuchukua lakini nipende kukuhakikishia kwamba tayari tunaufanyia kazi hata kabla ya hapo sisi tumekuwa tukijiuliza kwamba tukishawapa hizi taaluma basi waende kufanya nini, tuwawezeshe vipi, tunashukuru kwamba mmeongeza sauti katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mazingira; upandaji wa miti tunashukuru kwa pongezi hizo lakini ushauri kwamba tuongeze pia tumeuchukua, tutaufanyiakazi na ushauri wa kutoa elimu katika kutunza mazingira.

Mheshimiwa Spika, uwekezaji usio na tija, naomba tu niseme kwamba uwekezaji unaofanywa na Jeshi umekuwa na tija kubwa sana rasilimali tunazozipata kutoka Serikalini ni kidogo na nikiwapa takwimu ni kwa kiasi gani uwekezaji huu umeweza hata kusaidia Jeshi la Ulinzi na Wananchi wa Tanzania kutekeleza majukumu yao ya msingi mtashangaa. Kwa hiyo, lakini kama yapo uwekezaji ambao unafikirika hauna madhara basi tutauangalia tuhakikishe kwamba madhara ya namna hiyo tunajikinga nayo lakini uwekezaji huu ni muhimu na umekuwa na tija sana.

Mheshimiwa Spika, mengine yalijibiwa; barabara limejibiwa lakini pia nipende tu kuwahakikishia kwamba barabara za doria na ulinzi ni kitu muhimu sana na hiki tayari nimekwishafanya mazungumzo na Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi na si barabara hiyo moja tu iliyoelezwa, ziko barabara nyingi na tayari baadhi zimeshaanza kufanyiwa kazi lakini baadhi tunaangalia jinsi gani ya kuziingiza katika mipango ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upandishaji vyeo wanawake; wanawake wanafanyakazi kama wanaume na hakuna ubaguzi katika upandishaji vyeo, vyeo vinapandishwa bila kujali jinsia kinachotakiwa katika Jeshi tu ni weledi, kwa hiyo, wanawake wanaendelezwa na wanapandishwa vyeo na wapo katika sehemu mbalimbali.

Kuhusu malimbikizo ya likizo hili limekwishafanyiwa kazi katika hotuba nimeeleza kwamba pamoja na mambo mengine Serikali imetoa kipaumbele kuhakikisha kwamba tunalipa madeni yote na hili limeshafanyiwa kazi kama wapo waliobaki basi hao wataendelea kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, michezo ni muhimu tumesikia na tutaendelea kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, naomba pia kwa niaba ya watumishi wote wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na taasisi zake kupokea shukrani na pongezi kwa kazi nzuri inayofanywa ya kulinda mipaka yetu. Wengi mmetoa shukrani nazipokea kwa niaba ya Wizara na kudumisha amani na mmetoa maeneo mengi yanayofanyiwa kazi nzuri ikiwa ni pamoja na katika sekta ya afya, katika sekta ya elimu, lakini pia mmeeleza katika jinsi Jeshi lilivyosimama kuhakikisha kwamba nchi yetu imebaki salama wakati tumepata msiba wa Mheshimiwa wa aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na maeneo mengi. Kwa hiyo tunapongeza na pia kutoa mfano kwamba kwa kazi nzuri tumeweza kuokoa kiasi cha shilingi bilioni 65 katika ujenzi wa Kikombo, mifano ilikuwa mingi lakini napenda kushukuru na kuhakikishia Waheshimiwa Wabunge kuwa kazi zote zinazofanywa na Jeshi la Ulinzi na Wananchi wa Tanzania zinafanywa kwa weledi, umahiri na uzalendo wa hali ya juu na hii ndiyo misingi ya utendaji wa Jeshi letu na kazi nzuri zitaendelezwa daima. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri muda umeshaisha, lakini nakuongeza dakika tatu umalizie na Waheshimiwa Wabunge naongeza nusu saa tumalizie shughuli iliyo mbele yetu. (Makofi)

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, ahsante na kazi nzuri hizi zitaendelezwa kufanywa daima tu.

Mheshimiwa Spika, tumepokea pongezi ahsante baada ya ufafanuzi huu na kabla sijahitimisha hoja yangu naomba niwashukuru kwa dhati Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii, waliofatilia hotuba na mijadala na naamini tutaendelea kushirikiana katika kudumisha ulinzi na amani na kuwaletea watanzania maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jitihada kubwa zinazofanywa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu katika kudumisha amani na kuwaletea wananchi maendeleo zinapaswa kuungwa mkono na sisi sote kama ambavyo mmeeleza ninyi wenyewe mmeshuhudia kwamba anafanyakazi kubwa kama Amiri Jeshi Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa inamshukuru kwa dhati kwa namna ambavyo amekuwa akisimamia ulinzi na usalama na kuwa mstari wa mbele katika kutatua changamoto zinazoikabili Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na taasisi zake tangu aingie madarakani.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa pia mstari wa mbele kuidumisha diplomasia ya ulinzi na ameendelea kuiletea heshima nchi yetu kama Amiri Jeshi Mkuu mwanamke wa kwanza katika historia ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie lugha hii ingawaje siyo rasmi kwamba ameupiga mwingi kwa kutusimamia kitaifa lakini pia kutupaisha kimataifa. Tuendelee kumuunga mkono Rais wetu mpendwa na napenda kusema kuwa wanawake wanaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na watanzania wote kuwa chini ya uongozi mahiri wa Amiri Jeshi Mkuu Mama Samia Suluhu Hassan, Wizara ya Ulinzi na Taasisi zake zipo imara kuhakikisha kuwa nchi ipo imara na salama muda wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla ya kuhitimisha naomba nitoe wito kwenu Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote kuwa ulinzi wa Taifa letu ni jukumu la kila Mtanzania, ni jukumu la kila mmoja wetu na kila mmoja wetu anao wajibu wa kulitekeleza jukumu hilo. Wanajeshi wetu wanafanya kazi kubwa sana usiku na mchana kwa weledi, uhodari na uzalendo wa hali ya juu nawapongeza sana kwa moyo huo wa kujituma na kwa kazi kubwa wanayoifanya niwaombe sasa tuwaunge mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na baada ya maelezo hayo naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naafiki.