Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa kwanza. Kwa kuwa muda ni mchache, kwanza nimpongeze kipekee Mheshimiwa Nape Moses Nauye, Waziri; tokea ateuliwe kushika nafasi hii, amerejesha heshima, amani na utulivu kwenye Sekta ya Habari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita kwenye eneo moja tu la TEHAMA na katika hilo nitajikita kwenye kuwa na mfumo mmoja wa kieletroniki katika kuendesha shughuli za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na kauli nyingi na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais ambaye mara tatu akiapisha Makatibu Wakuu, akipokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu mwaka 2021 na vilevile akipokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali mwaka huu tarehe 30 mwezi Machi, amesisitiza jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo hatua kubwa sana iliyofanywa na Serikali katika uwekezaji kwenye Sekta ya TEHAMA. Tunacho kituo cha National Internet Data Center (NIDC) ambacho kina miundombinu mikubwa na ya kisasa kabisa katika suala la TEHAMA, lakini Serikali kupitia sheria Na.10 ya mwaka 2019 imeanzisha wakala e-GA (e-government) ambaye anafanya kazi ya kusimamia mifumo ya TEHAMA kwenye Serikali. Pia asilimia 100 Serikali ina political will katika kuhakikisha Sekta ya TEHAMA ina flourish na kwa kufanya hivyo imeanzisha wizara maalumu kwa ajili ya Teknolojia ya Habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake ametueleza kwenye mobile connectivity kwamba sasa tunawatumiaji zaidi ya milioni 55 wa simu na milioni 29 wa mitandao ya internet.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uchache, upo upungufu. Upungufu wa kwanza, nchi yetu haina central database system ambayo ina taarifa zote za Mtanzania. Kwenye Taifa letu tunayo NIDA wanaandikisha vitambulisho, tunayo RITA wanatoa vyeti vya kuzaliwa, tunayo TRA wanatoa TIN Number; na hii kuipata siyo mchezo, upeleke nyaraka nyingine toka taasisi nyingine; Tunaye humu ndani Seif Gulamali anatoa Kadi za Yanga; tunao CRDB nao wanatoa kadi zao kwa wateja wao; tunayo Tume ya Uchaguzi na yenyewe inaandikisha Watanzania hao hao; tunao NHIF mmeona wanatibia wanaume mpaka ujazito kwa kutoa vitambulisho vyao na kuandisha watu; una leseni ya udereva; una kadi ya Chama cha Mapinduzi; kwa utaratibu huu hatuwezi kufikia pale tunapotaka kufika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kwa kuwa muda ni mdogo, niyaseme machache. Leo Mtanzania akiomba mkopo, ataombwa nyaraka hii, ataombwa nyaraka nyingine kwa sababu hakuna sehemu moja ambapo benki inaweza ikaenda ikakuta taarifa zote za Mtanzania huyu za kuweza kumsaidia. Hata huo mkopo ukiwa approved; juzi nilienda ofisini kwa mtu mmoja nikakuta anasaini nyaraka za mikopo, alikuwa na nyaraka siyo chini ya 40 amesaini signature 219, kitu ambacho tungekuwa na mfumo wa kieletroniki, angesaini tu pale kieletroniki agreed, angepata mkopo wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, e-GA ipo chini ya Ofisi ya Rais, Utumishi. Leo Waziri anawasilisha hapa TEHAMA, yupo Wizara nyingine na hilo nalo ni tatizo kwenye mfumo wa kisheria wa nchi yetu. Nimeenda e-GA vijana wale wanafanya kazi nzuri, nawapongeza sana, lakini wakati naondoka nikashangaa, nikapewa nyaraka hizi. Wewe una mamlaka ya kieletroniki, una-print nyaraka za nini? Kama kweli tuna nia ya kwenda kietroniki, leo hapa nani amewahi kuprintiwa nyaraka na face book? Nani kaprintiwa nyaraka na Instagram? Nani amewahi kuprintiwa nyaraka yoyote na simu yake ya mkononi au anamjua hata meneja wa kampuni ya simu anayoitumia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuseme mifumo ifuatayo kwa ufupi wake. Tunao mfumo wa TANePS. Huu siyo mfumo, ni kitu kimetengenezwa cha kumsaidia tu Mtanzania, mzabuni asi-print nyaraka za PDF ofisini kwake, bali azi-upload ziende kule zikafanyiwe kazi. Ingekuwa ni mfumo, ulitakiwa kieletroniki umtambue mzabuni, utangaze zabuni, ufanye evaluation, uandae mkataba, ukafanye vetting mkataba uliozidi Shilingi bilioni moja, uende ukafanye maombi ya msamaha wa kodi ya ongezeko la thamani (VAT), ufanye contractor management, uandae certificate, umlipe mkandarasi, tusipate zile hasara alizozionesha CAG za ucheleweshaji wa malipo kwa kuwa kazi zinafanyika kwenye manual system. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi nitaje hasara zinazopatikana nchi katika mifumo ya kieletroniki. Ukisoma ripoti ya CAG ukurasa wa 348 TANROAD peke yake wamelipa Shilingi bilioni 224 kwa ukosefu wa mifumo ya kulipa hii, wanalipa kwa manual system. Leo Bodi ya Mikopo inao wadaiwa 155,722 wanaodaiwa Shilingi bilioni 422 hawajui wako wapi? Yaani kuna Watanzania wamesoma degree, halafu Bodi ya Mikopo haijui itawapata wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tukisema Bima ya Afya kwa watu wote bila kuwa na mfumo wa kieletroniki ambapo Watanzania wote wanapatikana, itakuwa ni ndoto. Kama tu hii NHIF inashindwa kutibia watu na inajiendesha kwa harasa, hatuwezi kufika. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika tano ni chache, nitachangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, senior anasema uniongeze kidogo Mwenyekiti ukiridhia.

MWENYEKITI: Nilishakuongeza sekunde karibu 40 mpaka sasa. Kwa hiyo, nikushukuru kwa mchango wako.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)