Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianzie kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoifanya toka amekaa kwenye hicho kiti lakini pamoja na timu yake yote ya Wizara hii pamoja na Naibu wake kwa kweli wanajitahidi sana. Na nakupongeza kwa jinsi ambavyo umesimamia suala la anuani ya makazi, tumekuona ukizunguka huku ukitoa maelekezo hayo ndiyo tunayoyahitaji sisi watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze sana kwa namna ya kipekee Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mkazo wa matumizi ya TEHAMA katika kufanya shughuli zetu mbalimbali. Na hivi sasa kuna shule za Sekondari zinajengwa kila Mkoa tena za wasichana kwa ajili ya kuwezesha katika masuala ya TEHAMA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende pia kuchukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Spika wetu wa Bunge la Tanzania kwa jinsi ambavyo ameamua kuendelea kuboresha huduma za Maktaba ili sasa Wabunge pamoja na wadau wote wanaopenda kufuatilia shughuli za Bunge waweze kupata taarifa mbalimbali za Bunge pamoja na kujisomea majarida mbalimbali au vitabu mbalimbali kupitia mtandao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naamini kwamba Wizara hii itashirikiana na Bunge letu hili Tukufu kuhakikisha kwamba linakuwa ni kweli Bunge la kimtandao. Kwa sababu hata wakati tunaanza hivi vishikwambi watu walisema hivi itawezekana, lakini imeshawezekana sisi wote tunatumia vishikwambi na shuhguli za Bunge zinaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina suala moja zito sana kwa kuliangalia linaweza kuwa ni la kawaida lakini ni zito. Waheshimiwa Wabunge wengi wanashindwa kuhudhuria vikao vya Baraza katika halmashauri zetu kutokana na shughuli hizo kugongana na shughuli hizo ambazo zinatakiwa ziendeshwe kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wakati Mheshimiwa Mbunge analazimika kutembea usiku kucha kwa ajili ya kuwahi kikao cha Baraza na kurudi, jambo ambalo linagharimu lakini pia ni hatari kwa maisha yake kwa sababu anakuwa amechoka hata madereva wanakuwa wamechoka. Sasa nilikuwa najiuliza kwa sababu hii Mihimili ya Dola inafanya kazi kwa ushindani lakini pia kwa kuhakikisha wanatoa huduma zinazotakiwa kwa wananchi. Sisi Wabunge tunapokosa kuhudhuria Mabaraza yetu yanapokaa ni kwamba ni mambo mengi tunashindwa kuchangia na kuweza kusimamia halmashauri zetu inavyopaswa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilikuwa nasema niiombe sana Wizara hii ya Habari, Mawasilinao na Teknolojia ya TEHAMA pamoja na Bunge letu Tukufu kuanzisha kona ya Madiwani nikimaanisha Wabunge hapahapa Bungeni. Sisi tunavyokuwa hapa tuweze kuhudhuria vikao vyetu vya Baraza vya halmashauri wakati tukiwa tunaendelea na shuhguli za Kibunge kwa njia ya Mtandao. Kule kwenye halmashauri zetu bado hazijafungwa zile huduma za kuwezesha hayo mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana na hilo leo mchango wangu hasa unajikita hapo. Niwaombe kuna mfuko huu ambao ni wa mawasiliano kwa wote ambao umefanya kazi nzuri sana wa kusaidia kwenye maeneo yetu hata huko Vijijini, nawapongeza sana. Lakini pia vyombo vya Habari vinajitahidi, lakini katika hili naomba Wizara yetu hii chini ya wewe Mheshimiwa Waziri Nape Nnauye pamoja na Mheshimiwa Spika wetu sisi tunahitaji hiyo huduma ili tuhudhurie vikao vyetu vya Mabaraza bila kukosa. Haiwezekani Mbunge inafikia unahudhuria vikao viwili tu au pengine kimoja na pengine usihudhurie kabisa simply kwa sababu unakosa mawasiliano kama haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia inapotekea tatizo ni mwanzo wa kufikiri juu fursa nyingine. Kuna tatizo la upandaji wa bei ya mafuta sasa kwa nini tutembeze gari kutwa, usiku kutwa mara mbili, mara tano, wakati pengine kwa kutumia mtandao tu tungeweza kutekeleza hayo majukumu yetu vizuri kabisa. Na nikisema hivyo simaanishi kwamba sisi Wabunge sasa tutakuwa hatuendi kwenye Majimbo yetu. Tunazungumzia kipindi tunachokuwa Bungeni tunataka tuweze kuwasiliana na watu, tuweze kukaa kwenye vikao vyetu vinavyohitajika ili na sisi tuweze kuchangia na kutoa tija kwa wananchi wetu. Hili nalinzungumza kwa kweli nikiwa serious kwa sababu kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu…

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. ENG. STELLA M. MAYANYA: Mheshimiwa Waziri Mkuu anatumia sana mtandao katika kuwasiliana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)