Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru kunipa nafasi hii. Nianze mchango wangu kwa kuchangia kuhusu Shirika la Reli. Ili nchi iweze kuendelea inahitaji kuwa na miundombinu ya reli. Shirika letu la Reli linahitaji kufanyiwa mabadiliko hasa ya kisheria. Tayari Serikali ilileta mabadiliko ambapo RAHCO ilitenganishwa na TRL. Niiombe na kuishauri Serikali ni vizuri ikaleta sheria hapa Bungeni shirika hili liunganishwe liwe kitu kimoja ili liweze kuwa na ufanisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, zipo changamoto nyingi sana ambazo zimejitokeza kwenye Shirika la Reli. Ni vyema Serikali ikapata ushauri wa Wabunge ikaangalia umuhimu wa kuliunganisha ili liweze kufanya kazi vizuri. Litakapokuwa limeunganishwa litaisaidia nchi na wananchi walio wengi watanufaika na utekelezaji wa sheria hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali wamekuja na mpango wa kujenga reli ya kati. Ujenzi wa reli ya kati tunahitaji Serikali ifanye mchakato haraka ili iweze kutengenezwa reli ambayo itawasaidia wananchi. Naomba Serikali iharakishe na iangalie kwenye maeneo ambayo yana umuhimu wa uwekezaji. Serikali itakapokuwa imejenga reli kuanzia Dar es Salaam - Tabora - Mwanza iangalie umuhimu sana wa kufikisha reli hii kutoka Tabora - Kigoma na tawi lake la kutoka Uvinza - Msongati. Pia tunahitaji reli hii itoke Kaliua - Mpanda - Karema kwa ajili ya uwekezaji. Ni vizuri Serikali ikaangalia umuhimu wa kuijenga hii reli kwa haraka ili iweze kutoa ufanisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine la pili ni suala la bandari. Bandari ndiyo lango kuu la uchumi wa nchi yetu. Bandari ya Dar es Salaam inahitaji kufanyiwa marekebisho kwenye maeneo hasa ya himaya ya pamoja ya forodha (single custom). Eneo hili ni muhimu sana kufanyiwa mabadiliko ya haraka kwani inalazimu kodi kwa mizigo ya nchi jirani kutozwa hapa nchini kabla ya mizigo hiyo haijatozwa nchini mwao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba na kuishauri Serikali iachane na mpango huu kwa sababu unawafukuza wafanyabiashara wa nchi jirani. Sheria hii inawafanya wafanyabiashara wakimbilie kupeleka mizingo kwenye bandari ya Mombasa, Durban na Msumbiji. Tunaiomba Serikali ifuate ushauri ili iweze kusaidia kutoa tatizo la kukimbia kwa wafanyabiashara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni warehouse rent ambayo inatozwa mara mbili, inatozwa na Bandari na TRA. Tunaomba Serikali iangalie suala hili na Mheshimiwa Waziri na timu yake tunaamini wana uelewa wa kutosha ili waweze kutoa hivi vitu ambavyo vinafanya kuwe na mgongano wa kimaslahi na kuwafanya wafanyabiashara wakimbie bandari yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba Serikali iboreshe bandari ambazo zipo mikoani, Mkoa wa Mwanza, Iringa kwa maana ya kule Njombe, maeneo ya Kyela, maeneo ya Ziwa Tanganyika kwa maana ya bandari ya Kigoma na Karema. Tunahitaji bandari hizi ziweze kuboreshwa ili ziweze kutoa huduma kwenye maziwa makuu, Ziwa Victoria na Tanganyika. Tukifanya ujenzi wa bandari na kuboresha hizo bandari, zitatoa uchumi mzuri kwenye maeneo husika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na maboresho ya bandari kwenye Mikoa ya Mwanza, Kigoma, Katavi, Mbeya kwa upande wa Kyela na kule Njombe maeneo ya Ziwa Nyasa, bado tunahitaji kuunganisha Bandari na Marine kwani zikiunganishwa zitafanya kazi pamoja kuliko ilivyo sasa hivi. Marine service haina uwezo wa ku-operate meli ambazo zipo kwenye maeneo husika. Tunaomba Serikali iangalie maeneo haya ili kufanya maboresho yatakayosaidia kukuza uchumi na kutoa ufanisi kwa hivi vyombo viwili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizugumzie suala la barabara. Serikali ina dhamira ya dhati kuunganisha mikoa yote nchini kwa barabara za lami. Niiombe Serikali iangalie umuhimu sana wa kuunganisha barabara zote ambazo zilichelewa kupelekewa maendeleo hasa zile zilizo pembezoni. Mkoani kwangu nina barabara ya kutoka Mpanda - Kigoma haijaunganishwa kwa kiwango cha lami. Nashukuru Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 16. Niiombe Serikali iharakishe kusaini mkataba ili barabara ile iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zipo barabara za kutoka mkoa wa Katavi kwenda mkoa wa Tabora, ni vyema Serikali ikaharakisha mchakato iliyonayo ili ziweze kukamilisha barabara hizi. Pia bado zipo barabara zinazounganisha mkoa wa Mbeya na mkoa mpya wa Njombe, mikoa ya kutoka Ruvuma kwenda Mtwara, lakini bado tunahitaji mkoa wa Kigoma kuunganishwa na Mkoa wa Kagera, tunahitaji barabara zote hizi ziunganishwe kwa kiwango cha lami ili nchi iweze kupitika vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie na suala la mawasiliano. Kwenye suala la mawasiliano Serikali bado tunahitaji iendelee kukuza ule Mfuko wa UCSAF ili uweze kutoa mawasiliano kwa wote. Vipo vijiji jimboni kwangu ambavyo viliahidiwa na Serikali kupatiwa mawasiliano kama vijiji vya Kata za Sibwesa na Katuma, lakini bado kuna vijiji vya Igagala, Majalila na Rugufu eneo la Mishamo tunahitaji mawasiliano ya kudumu ili wananchi waweze kupata huduma hiyo muhimu. Tunaiomba Serikali ielekeze nguvu kwenye maeneo hayo ili watu wote wanufaike na mfuko ule ambao unafadhiliwa na Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niishukuru Serikali na niombe ichukue ushauri ule na tunaunga mkono hoja, ahsante.