Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi. Baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu, nitumie fursa hii kumpongeza mdogo wangu Mheshimiwa Nape Moses Nnauye kwa kuteuliwa na kuamini na Mheshimiwa Rais kuongoza Wizara hii ambayo kwa kweli Watanzania tuna Imani naye kubwa sana na nadhani ataendeleza pale ambapo rafiki yangu Dkt. Ndugulile aliachia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizi, nianze kwa kushukuru Wizara. Jambo langu la kwanza nilipoingia Bungeni ilikuwa ni kuomba mawasiliano kupitia mnara katika Kata ya Likawage, nashukuru Serikali ya Mama Samia imetekeleza hili. Kupitia mchango wangu, niombe kama ambavyo niliomba katika Mkutano wa Sita uliopita kwamba mnara huu ambao umekamilika kule Likawage utakaohudumia Vijiji vya Nainokoli, Likawage pamoja na Liwiti, basi Mheshimiwa Waziri impendeze aende akazindue rasmi na wana wa Likawage wanamsubiri kwa hamu kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo wanasema kushukuru ni kuomba tena. Pamoja na hayo sisi Wanakilwa tunaendelea kuomba tena kwamba, mawasiliano haya ya njia ya simu bado ni changamoto katika Kata zetu za Nanjilinji, Chumo, Kandawale, Kinjumbi, Kipatimu pamoja na Kikole. Iwapendeze wenzetu wa Wizara hii ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari katika mpango huu wa 2022/2023, Kata nilizozitaja ziingie katika mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa umahususi, niseme kwa masikitiko kidogo kwamba, katika Wizara hii eneo la Shirika la TBC, Wilaya ya Kilwa pekee katika Mkoa wa Lindi ndiyo ambao hatuna huduma ya TBC, wilaya nyingine zote zilizobaki wanapata huduma hii. Impendeze Mheshimiwa Waziri mdogo wangu Mheshimiwa Nape, awaelekeze watumishi wake, watendaji wenzake katika Serikali, katika Shirika hili la TBC na siye wana Kilwa tunahitaji kupata taarifa za Habari kupitia TBC FM, TBC Taifa na vyombo vingine vya TBC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nijikite katika ushauri. Tumeona mikakati ya Wizara kupitia taasisi zake zote nane ni mizuri sana. Hata hivyo, kwa upekee nishauri katika eneo hili la mawasiliano kwamba, kwa muda mrefu eneo la mawasiliano limeachiwa sekta binafsi. Imebainika hapa kwamba, muda si mrefu, Mungu akipenda tunapitisha bajeti ya kutosha, lakini pia bado tuna nafasi ya kukusanya makusanyo mengi kupitia taasisi za Wizara hii. Niwashauri Wizara kwamba eneo hili la mawasiliano libebwe na Wizara kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko kutegemea watoa huduma binafsi pekee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili niseme kabisa kwamba, Wizara itengeneze sera kama ilivyo katika Wizara zingine kwa mfano Wizara ya Maji, Sera mita 400 maji, mita 400 maji; na Wizara hii ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari iweke sera kama ni kila kata ama kila kijiji ama kila umbali wa kilometa kadhaa kadri ambayo utafiti na usanifu utakavyofanywa na wataalam na kuja na hayo mapendekezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)