Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote niungane na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake lakini na wataalam kwa ujumla. Nampongeza Waziri kwa dhati kabisa kwa hii operation ya postcode, Mheshimiwa Waziri amekuja muda mfupi tu, lakini kazi aliyoifanya kila mtu ameiona. Kwa kweli hongera sana kwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Mbinga, pamoja na pongezi hizi, kwa upande wa Mbinga nina masikitiko kidogo. Kazi imefanyika vizuri, kwa bahati mbaya tumekwenda kuvuruga miradi iliyokuwa inaendelea. Wilaya ya Mbinga ina shida sana ya barabara, barabara hizi za TARURA na unajua Halmashauri ya Mbinga Vijijini ni milima na mabonde. Kwa hiyo, kwa muda mrefu barabara zetu zinapitika kwa shida sana. Zipo barabara tulizitengea fedha kwa bahati mbaya sana barabara zile fedha zimeondolewa zimepelekwa kwenye postcode. Sasa sijajua kama na katika maeneo mengine kumefanyika hivyo. Kama maeneo mengine haijafanyika hivyo kwa nini sisi Mbinga; Barabara ya Ngima kwenda Litembo ambako kuna hospitali, Barabara ya Mitawa kwenda Ilela na Daraja la Linyani, fedha za miradi hii imeondoshwa imepelekwa kwenye mradi wa postcode.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kati ya yale mabao na barabara kipi muhimu zaidi, hivi ni nani anaweza kuvumilia kukosa kuona kibao na kukosa kupita njia nzuri kwenda hospitali? Litembo nilisema hapa ndipo tunapotibiwa sisi, barabara hii inapitiwa na Kata nne za Ngima, Mkumbe, Ukata na Kipololo, lakini pia Kata ya Ukilo zote hizi zinatumia barabara hii. Hali ya barabara hii ni mbaya sana. (Makofi)

TAARIFA

MHE. ENG. STELLA M MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nimshtue kidogo kaka yangu, Mheshimiwa Benaya nadhani kwa uchungu wa zile barabara zilizokosa fedha amesema hata yale mavibao yana haja gani. Kimsingi kwa kweli anuani za makazi ni muhimu na vile vibao ni muhimu, kwa hiyo ningeomba tu kwamba pamoja na uchungu huo lakini tujiweke vizuri kidogo. Ahsante sana.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei hii taarifa yake kwa sababu ananipotezea muda wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naomba unilindie dakika zangu. Namheshimu sana dada yangu Injinia Stella Manyanya na ndiyo Mwalimu wangu; lakini kwenye hili sijakaa mradi ule ni mradi mzuri, nafikiri kwenye maelezo yangu ya mwanzo sijui hakunisikia, ni mradi mzuri, lakini nilikuwa nahoji hapa, hivi mtu akikosa kusoma kibao na akakosa barabara, yupi ataumia hapa? Ndiyo hoja yangu ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii mwaka 2020/2021 iliondolewa fedha; tukaitengea fedha 2021/2022 inaondolewa tena fedha, hivi kweli kwa sababu zipi za msingi kiasi hicho? Pia nilikuwa nahoji hapa, hivi ilivyofanyika Mbinga ndivyo yalivyofanyika kwenye Majimbo mengine? Kama sivyo, kwa nini sisi tufanyiwe hivyo. Barabara hii inakwenda kwenye Hospitali pekee ya Halmashauri ya Wilaya Mbinga kwa maana ya Hospitali ya Misheni tunayoitumia sisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema hapa zaidi ya kata tano zinapita hii barabara na barabara hii utafikiri ni palio la ng’ombe, mashimo mashimo, mawe mawe, haipitiki.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mbunge, muda wa Mheshimiwa unakaribia kwisha, ngoja amalizie hoja yake anayoongea.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi wananchi wanalazimika kwenda Mbinga ndiyo waende Hospitali ya Litembo, wanalazimika kwenda Mbinga kilometa zaidi ya 30, wakati pale kuna kilometa 10 tu wanafika hospitalini. Mama Mjamzito anaongezewa safari ya kilometa ya zaidi 30, kwa kweli jambo hili limenisikitisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na uzuri wa mradi huu pamoja na mimi naheshimiana sana na Mheshimiwa Nape, lakini nataka kwenye majumuisho anieleze fedha hizi zitarejeshwaje na miradi hii itatekelezwaje, bila hivi mimi nitaondoka na Siwa hii. Haiwezekani hili Siwa mimi nitatoka nalo ni lazima aniambie Mheshimiwa Nape miradi ile inakwenda kuishaje? (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kapinga.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naam!

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kapinga hebu kaa chini, hebu kaa chini kwanza.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge.

KUHUSU UTARATIBU

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni ya 71(j) lugha inayotumika ambayo kwa kiasi fulani inakera. Mheshimiwa Kapinga ninamheshimu sana na ninafahamu bado ni kijana ni Mbunge wa mara ya kwanza, kwenye record zetu hakuna mtu amewahi kuondoka na Siwa, kwa hiyo, wewe utakuwa ni Mbunge wa kwanza kuondoka na Siwa. Hili Siwa ndilo Bunge lenyewe. Kwa mujibu wa utaratibu wa Mabunge ya Jumuiya ya Madola Siwa hili limewekwa ndiyo heshima yetu, ndiyo tunalolisalimia hapo na ndiyo inayoshika mamlaka ya Spika. Kwa hiyo, wewe ukiondoka na hili Siwa maana yake umeondoka na hili Bunge lote umekwenda nalo Mbinga. Kwa hiyo, ninakuomba tu ama ufute maneno hayo ili uendelee kutoa mchango wako mzuri na mimi naamini wewe ni Mbunge mzuri sana. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kapinga.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kufuta maneno hayo. (Makofi)