Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia, ya Habari kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Spika, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa hotuba nzuri iliojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendeleo endelevu na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa Kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni “Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na taarifa ya Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari inaonesha kuna mafanikio makubwa kwenye sekta za habari, mawasiliano ikiwemo mikakati ya kupunguza gharama za mawasiliano kwa wananchi. Utendaji kazi ulilenga pia kuboresha miundo ya TEHAMA kuwezesha mwelekeo mzuri wa kulea ubunifu ili Tanzania iendane na kasi ya dijitali ya kiuchumi (digital economy).

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza msukumo mkubwa kwenye kuendeleza maboresho ya mtandao wenye kasi zaidi na kuhakikisha matumizi mazuri ya Data Center ili kuwezesha ubunifu wa miundombinu ya TEHAMA hasa Serikalini iweze kusomana. Kutokana na kuwepo mifumo tofauti kwenye taasisi za Serikali ni muhimu sana kuunganisha mifumo yote iweze kusoma ili kuleta ufanisi unaoendana na dunia ya leo. Mwelekeo wa dunia ya leo ni kufanya shughuli zote za ki-TEHAMA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kuboresha muundo wa Wizara na Taasisi zake ili kuwepo na idara mahususi itayoongozwa na Afisa TEHAMA Mkuu (CIO) ngazi ya Kamishna. Kuwepo kwa muunganiko wa mifumo yote (Core Government System), ni muhimu kuboresha e-government na itawezesha ufanisi na kupunguza gharama kwa kiasi kikubwa sana. Kuwepo kwa Mkongo wa Taifa na Data Center ni fursa kwa kuwezesha kutengeneza mfumo wa kuratibu na kuendeleza ubunifu katika TEHAMA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, teknolojia imewezesha huduma ya kifedha juimishi (financial inclusion) na hii fursa pia kwa Serikali kuratibu miamala ili iwe sehemu ya mfumo rasmi wa malipo kwa usimamizi wa Benki Kuu na TCRA. Napendekeza maboresho kwenye tozo za miamala itakayoongeza mapato ya Serikali lakini ikizingatia kupunguza mzigo kwa wateja. Serikali kwa kushirikisha wadau, itumie uzoefu wa sasa kuboresha huduma za miamala kwa kuoanisha ufanisi kwa huduma ya kifedha juimishi na tozo mbalimbali na mchango wa huduma hii kwenye kukuza uchumi wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio makubwa ya utekelezaji wa Wizara ikiwemo zoezi la postikodi, kuna maeneo mengi ambayo bado hayajapata huduma za minara ya mawasiliano na hata kwenye maeneo kadhaa yenye minara katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya hayapati huduma ya mawasiliano. Vijiji vingi ikiwemo katika Kata za Ulenje, Iyunga Mapinduzi, Mshewe, Mjele, Ilembo na Ihango havina minara na vingine kuna minara ambayo kwa muda mrefu haina mawasiliano. Kwa kuzingatia lengo la kupeleka TEHAMA kwa kila shule, Serikali iharakishe kujenga minara maeneo yote kwenye vijiji na vitongoji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.