Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa hii nafasi ya kuchangia. Nami napenda kwa kuanzia kwanza kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa uwekezaji aliouweka kwenye Wizara hii ikiwemo miundombinu ya barabara, miundombinu ya bandari na miundombinu ya anga. Kwa kweli kazi inayofanyika ni kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake ya Manaibu Waziri, kazi yako ni nzuri sana na kwa kweli umedhihirisha kuwa kazi unayoifanya kwa kweli itatuletea mapinduzi makubwa katika uchumi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nayasema hayo kutokana na maboresho yanayofanyika kwenye miundombinu ya bandari. Serikali imewekeza fedha nyingi kwenye miundombinu ya bandari. Mapinduzi ya Bandari zetu za Dar es Salaam, Tanga pamoja na Mtwara yanaweka nchi yetu katika ushindani mzuri katika ukanda huu wa Afrika Mashariki pamoja na Afrika ya Kati.

Mheshimiwa Naibu Spika, bandari zetu zikifanya vizuri, tutakuwa na nafasi kubwa ya kuhakikisha kuwa tunashindana na bandari zinazotuzunguka; Bandari ya Beira Mozambique, Durban, Weisberg pamoja na bandari nyingine zote; Robito ambazo zimekuwa zikinyang’anya soko letu la bandari ya Dar es Salaam na mzigo wa Bandari ya Dar es Salaam umekuwa ukiporomoka hasa kwa nchi ya Zambia, DRC Congo na hata Malawi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia uwezo wa bandari yetu kuhudumia nchi hizo tatu, nina imani ni zaidi ya tani milioni sita, lakini leo hii nilipokuwa naangalia taarifa, ni Shilingi milioni tatu tu ambazo zinahudumiwa na bandari yetu kupitia Dar es Salaam Corridor. Kwa hiyo, ukiangalia nchi kama ya DRC Congo ambayo ni 36% na nchi ya Zambia 31% na Malawi 5% ya mzigo unaopitia bandari yetu ya Dar es Salaam umepungua kwa kiasi kikubwa mno. Ukiangalia sababu ambazo zimetolewa kwenye hizi ripoti tulizonazo ni zile ambazo zipo ndani ya uwezo wa Serikali kujirekebisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, mojawapo ni uwezo wa utendaji wa reli zetu; Reli ya TAZARA na pamoja na Reli ya Kati. Mzigo mwingi ambao nimeusema hapo unapita kwenye barabara zetu. Kwa hiyo, mzigo huu umekuwa unasababisha hata kuharibu barabara zetu na kwa kiasi kikubwa unaufanya usafirishaji kwa kupitia Bandari ya Dar es Salaam kuwa wa ghali mno ukilinganisha na bandari nyingine. Mfanyabiashara anachoangalia, ni wapi atapata usafirishaji kwa bei nafuu?

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tukiongelea hapa bei ya mafuta, bei ya mbolea na bei ya mazao kuwa ni kubwa, lakini hizo bei zinasababishwa vilevile na gharama zilizopo kwenye usafirishaji. Leo hii bei ya mbolea kufika bandarini Dar es Salaam ni kama shilingi 140,000 lakini ikija kufika pembezoni mwa Tanzania itakuwa zaidi ya shilingi 170,000. Kwa hiyo, kukiwa na efficiency kwenye bandari yetu na Serikali ikachukua hatua za makusudi kuhakikisha mizigo yote hii inapita kwenye reli, hakutakuwa na haja hata ya kupunguza mapato ya Serikali. Kwa hiyo, tukiongeza ufanisi na tija tunaweza kuwapunguzia Watanzania wetu mzigo mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ombi langu na ushauri kwa Mheshimiwa Waziri, aangalie, naye ajiulize ni kwanini hawekezi pamoja na matatizo yote ya Mkataba wa TAZARA? Ni kwa nini hatujawekeza kwenye kuboresha Reli ya TAZARA? Kama asilimia 72 ya mzigo wote unaoenda nje ya Tanzania unapitia kwa barabara ambazo kwa mzigo ambao ungechukuliwa na TAZARA sasa huwezi kuwa na sababu yoyote ile ya kuangalia ni kwanini Wizara haitaki kuwekeza kwenye TAZARA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TAZARA ina historia ndefu, TAZARA haikuanzishwa tu na Mwalimu Nyerere pamoja na Kaunda, ilianza toka enzi; na mawazo yalikuwa ni ya Ma-settler, wakulima, walitaka kurahisisha usafirishaji wa pembejeo na usafirishaji wa mazao. Hata hivyo, ilitusaidia sisi baadaye wazo lilipokuja kwamba tuichukue TAZARA kama sehemu ya kutusaidia katika ukombozi, ndiyo sababu ikaitwa Reli ya Uhuru, lakini sasa hivi hii ni reli ya ukombozi na mapinduzi ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Rais ametoa kama Shilingi bilioni 13 mwaka huu 2022 kwa ajili ya maboresho madogo ya TAZARA. Nilivyoiangalia haraka, hii ni asilimia tatu tu ya mahitaji ya TAZARA. Naomba haya marekebisho ya mkataba yafanyike haraka ili tuweze kuwekeza kiasi cha kutosha. Nakuhakikishia kuwa uwezo wa Serikali wa Shilingi bilioni 200 mpaka Shilingi bilioni 400 ambazo zitaibadilisha hii TAZARA ika-transform na hii mizigo yote ambayo inachukuliwa na nchi shindani na bandari shindani ikaweza kuchukuliwa kupitia bandari yetu ya Dar es Salaam, hatutalalamika kuhusu fedha za kigeni, hatutalalamika vilevile kamba kodi kubwa. Kwa hiyo, tutakuwa tumepunguza mzigo mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nalisema hilo ili na wenzetu wanapoangalia waone namna ya kuweka michakato, ni namna gani tuboreshe upatikanaji wa mbolea na kusafirisha mizigo nje. Isiwe kila mmoja anaangalia kwake, Hapana. Hii ichukuliwe kwa pamoja, na nina imani katika hii crisis ya mafuta sasa hivi, tukiweza kuboresha TAZARA tukajenga bandari kavu upande wa reli ya kati na reli ya TAZARA, badala ya mafuta kuzagaa zagaa Dar es Salaam, kubakia kwenye Bandari ya Dar es Salaam kwa muda mrefu na ikaongoeza bei ya mafuta, hayo mafuta yangeenda moja kwa moja kwenye bandari kavu na wateja wa kutoka Congo, Zambia, Malawi na kadhalika wachukulie huko mipakani hayo mafuta badala ya kuyafuata Dar es Salaam ambapo mzigo unakuwa mara mbili. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Oran, ni kengele ya pili.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naomba niunge mkono hoja, lakini naomba sana reli ya TAZARA iweze kuboreshwa.