Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie bajeti hii ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Awali ya yote napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri sana anayoifanya katika kuwaletea Watanzania maendeleo. Anafanya kazi kubwa sana, wote tunaona miundombinu inavyojengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nilikuwa natoka Dar es Salaam kwa njia ya barabara nikaona magari ya IT kutoka bandarini kwenda nchi jirani mengi sana msururu, foleni ya magari barabarani kuonyesha kwamba bandari imeboreshwa na magari mengi yanaingilia Dar es Salaam kwenda huko Malawi, Zambia, Rwanda na kwingineko. Hayo ni maendeleo makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukipongeza Chama cha Mapinduzi kwa kuwa na mipango mizuri, sera, ilani na kadhalika ambapo yote kwa ujumla wake ni kuboresha maisha ya Watanzania, ipo vizuri na inajipanga vizuri. Naipongeza Wizara ya Ujenzi, Mheshimiwa Waziri, Manaibu Waziri, Watendaji wote, TANROADS na taasisi nyingine ambao wako katika Wizara hiyo kwa kazi kubwa wanayoifanya kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nianze kuchangia mambo mawili ambayo yananihusu moja kwa moja. Kule Kagera miaka ya nyuma tulipima uwanja wa Kajunguti, home Kajunguti. Ulipimwa vizuri, vipimo vikaonekana kwamba uwanja unafaa pale, fidia kwa wananchi ikahesabiwa ikawa inatafutwa kwamba thamani ya uwanja ule ilikuwa ni nini? Ikabainishwa, ikajulikana, lakini baadaye haukujengwa ule uwanja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ule uwanja ni muhimu sana. Pale ulipopimwa kujengwa ni mahali sahihi kabisa. Leo tuna Jumuiya ya Afrika Mashariki, ina Kenya ndani yake, ina Uganda, Sudan ya Kusini, Rwanda, Burundi, Kongo DRC, na sisi wenyewe Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Kajunguti, home Kajunguti ni katikati ya nchi hizi saba. Kwa hiyo, uwanja huo ungejengwa pale ungekuwa ni kitovu kikibwa sana cha uchumi cha nchi hii. Kutoka pale kwenda Kampala kwa gari ni masaa mawili, kutoka pale kwenda Kigali, Rwanda kwa gari ni masaa mawili na nusu, kutoka pale kwenda Bunjumbura kwa gari ni masaa matatu, kutoka pale kuingia Uganda kwa gari ni nusu saa, kwenda Kenya kwa gari au kwa maji ni masaa mawili na nusu, na vilevile kwenda Sudan siyo mbali, Tanzania ndiyo sisi wenyewe tupo hapa. Kwa hiyo, ingekuwa ni kitovu cha uchumi na kuleta maendeleo makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yale yaliyozunguka pale yana mvua nyingi, yana rutuba. Mfano Masaka pale Uganda Kusini au Mbarara au Kisumu kule Kenya kwa wakulima wa maua na mboga mboga, tuna samaki pale Ziwa Victoria. Pale zingekuja ndege za mizigo, zingepeleka mizigo hii Ulaya, Marekani, na kadhalika na ndani ya muda mfupi maua au mboga mboga zikiwa fresh. Tungepata uchumi mkubwa sana kwa kuwa na uwanja ule. Kwa hiyo, napendekeza kwamba uwanja huu ujengwe na kazi iweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili pale Jimbo la Bukoba Vijijini lina barabara moja kubwa muhimu, ni muhimu sana. Barabara inayoanzia Kietema kwenda Kanazi kutokea Igwela, Katoro hadi Kyaka kilomita 66. Barabara hii ni muhimu sana sana sana na nimeizungumzia sana barabara hii hapa Bungeni na nje ya Bunge. Humu ndani Bungeni peke yake leo ni mara ya tano naizungumzia barabara hii kwa njia ya mchango kwa njia ya maswali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Wabunge wengine walioongea jana majibu ni tunajenga, tunajenga, tunafanya upembuzi yakinifu, tunajenga lakini barabara ile haijajengwa. Ile barabara ni muhimu kwa sababu inahudumia karibia jimbo zima, Wilaya nzima ya Bukoba Vijijini. Inahudumia kwenye Jimbo langu peke yake kata 20 kati ya Kata 29 ukiunganisha na Jimbo la Nkenge la Mheshimiwa Kyombo Kata tatu linahudumia jumla ya Kata 23 kupeleka mazao sokoni kule mjini, pembejeo kwenda kwa wananchi kule ndani ni barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wagonjwa, kule ndani kuna watu karibu 400,000 wanaohudumiwa na barabara hii. Ukiwa na watu 400,000 kwa siku moja wagonjwa hawapungui 1,000 ambao wanakwenda mjini kutibiwa wanatumia barabara hii. Sasa kila neema ina matatizo yake, kule kuna mvua nyingi sana. Mwezi uliopita, mwezi wa nne masika tulipata mvua siku tatu mfululizo bila kuacha, siku tatu usiku na mchana inanyesha. TANROADS wanajitahidi sana wanakarabati ile barabara mara kwa mara lakini wanakarabati leo kwa njia ya kifusi cha changalawe, kesho yake ni mashimo ni mahandaki haipitiki, kwa hiyo, haifai inatakiwa iwe kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wanafia kule vijijini hakuna njia ya kupita kwenda hospitali, hakuna huduma. Uchumi unakwama, pembejeo haziwezi kwenda kule ndani, mbolea na mbegu na nini kwa ajili ya mazao ya kahawa na mazao mengine. Kwa hiyo, tunaomba barabara hii ijengwe. Na kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, CCM na Serikali yake imeweka kwenye Ilani ya Uchaguzi wa Mwaka huu 2020 - 2025. Hata iliyopita 2015 ilikuwemo kwenye Ilani lakini haikujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na siyo tu Ilani, nashukuru kwamba TANROADS wamefanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na imekamilika lakini ujenzi haujaanza. Naomba ujenzi wa barabara hii uanze kwa sababu ni barabara muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ina daraja kubwa sana pale katikati linaitwa Kalebe, daraja la Kalebe ni daraja kubwa sana, kubwa lakini la kizamani sana, limezeeka kweli kweli. Limejengwa miaka mingi na ndiyo njia pekee ya kutoka huko kwenye Kata 23 hizo kwenda Mjini Bukoba. Hakuna njia ya mchepuko, kama hiyo njia haipitiki au daraja halipitiki basi watu wanabaki huko ndani kama mtu anaumwa anafia huko hakuna njia mbadala. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lile daraja lilipojengwa lilikuwa na uwezo wa kubeba tani tano wakati huo likiwa jipya zima. Sasa limezeeka ninahakika limepungua uwezo lakini magari ya tani 15, malori ya kahawa, ya mbolea, watu wanakwenda kwenye harusi, kwenye sherehe mbalimbali, mabasi yanapita pale tani 10, tani 15, litauwa watu lile daraja, litaua. Miaka ya nyuma pale Dar es Salaam kulikuwa na daraja la chuma kutoka Banana kuja Kinyerezi tani saba ilikuwa mwisho.

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Rweikiza kwa mchango mzuri; kengele ya pili.

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja lakini naomba daraja hilo lijengwe. (Makofi)