Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu. Nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya na kuona umuhimu mkubwa wa kutumbukiza fedha katika Wizara hii kuweza kuboresha miundombinu katika nchi ili kuendeleza uchumi wa nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Manaibu wote wawili na watendaji wa taasisi ambazo ziko chini ya Wizara hii, lakini kubwa zaidi naomba nitumie nafasi hii kumpongeza Meneja wa TANROAD, Mkoa wa Morogoro kwa kazi kubwa ambayo anaifanya katika kuboresha miundombinu katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii vilevile kumpongeza Mheshimiwa Rais na Wizara kwa kutenga fedha ili kujenga kiwango kwa kiwango cha lami kilomita 78 barabara ya Bigwa Kisaki, lakini vilevile kutenga fedha kujenga kwa kiwango cha lami kilomita 11.6 barabara ya Ubena Zamozi – Ngerengere – Mvua – Kisaki - Matemele barabara ambazo zote hizi zinakwenda katika Bwawa la Mwalimu Nyerere pia inakwenda katika hifadhi kubwa namba moja katika Tanzania ya Julius Kambarage Nyerere.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana tulipata fedha ya kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya Bigwa Kisaki kilomita 15, ilitangazwa, lakini kutokana na umuhimu wa barabara hii na usikivu wa Mheshimiwa Samia Saluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waliweza kuifuta tenda hiyo na sasa tunatakiwa itangazwe kilomita zote 78.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Wilaya ya Morogoro ambayo inachukua majimbo matatu Jimbo la Morogoro Mjini, Morogoro Kusini Mashariki la mdogo wangu Babu Tale na Jimbo la kwangu la Morogoro Kusini wana umuhimu mkubwa sana wa barabara hii. Hata hivyo, huko barabara inakokwenda Serikali inakwenda kuongeza mapato kupitia utalii wa Hifadhi ya Mwalimu Nyerere, lakini naamini kabisa Bwala la Mwalimu Nyerere lilikikamilika linaweza kuwa nacho ni kichocheo kingine cha utalii kwa sababu ni bwawa kubwa katika Afrika. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri mwaka jana tumevumilia, mwaka huu ni imani yangu kabisa atakapokuja kufunga hoja yako atatuambia ni lini barabara hii itatangazwa ili apatikane Mkandarasi na tuweze kujenga kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoa pongezi hizo, nipende kusema neno moja TANROADS wanafanya kazi kubwa. TANROADS wako kwenye barabara, TANROADS wako kwenye madaraja, TANROADS wako kwenye viwanja vya ndege na TANROADS wako mpaka kwenye ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, nini matokeo yake? Kuna changamoto ambazo zipo kwenye ujenzi wa barabara. Niombe kuishauri Serikali, kuna fedha ambazo zinatengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara, ni asilimia 42 tu, nini maana yake?

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni kwamba, tunatengeneza barabara kama hatutoweza kuzifanyia matengezo ya mara kwa mara, maana yake hata zile barabara tunazotengeneza zitakufa na kama zitakufa maana yake zitaendelea kugharimu fedha nyingi kwenye Serikali na matokeo tutakuwa hatuwezi kusonga mbele. Kwa hiyo ombi langu kwa Serikali katika hili suala la fedha za matengenezo ya barabara, tuangalie uwezekano wa kupandisha kutoka asilimia 42 angalau tufike asilimia 70 ili barabara ziweze kutengenezwa vizuri na zipitike mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile mimi ni mkandarasi, kuna changamoto katika watumishi, watumishi wengi wa TANROADS wamegawiwa kama kuna kusema kuna usimamizi wa mabwawa, viwanja vya ndege, wa madaraja na watumishi wa TANROADS ni wachache, matokeo yake, unafika mahali kwamba Mhandisi mmoja anasimamia miradi zaidi ya 10 mpaka 15, techinician mmoja anasimamia miradi zaidi ya 10 mpaka 15, nini kinachoweza kujitokeza? Kama wakandarasi wakiwa sio makini, wanaweza kufanya kazi zikawa sio nzuri na matokeo yake fedha tunazopeleka zitapotea bure. Kwa hiyo niiombe Serikali, itengeneze utaratibu wakutoa kibali cha ajira kwa TANROADS ili wapatikane wataalam wa kuweza kusimamia hii miradi ambayo ina fedha nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine vilevile magari ni chakavu na vifaa vya kupimia ubora wa kazi za barabara ni vibovu. Naiomba Serikali nayo iangalie jambo hili ili value of money ambayo tunaipeleka iwe katika utaratibu unaokubalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuishauri Serikali, katika upande wa mizani mimi napata uwoga na mashaka, barabara zetu tunatumia fedha nyingi kuzitengeneza, lakini watumishi wa kwenye mizani ni watumishi ambao wako katika utaratibu wa mikataba. Huyu mtu ambaye unampa kazi kubwa ya kusimamia barabara unampa kazi kwa ajira ya mikataba, anaweza kushawishika na rushwa na ndio hayo tunayaona barabara zetu zinazidi kuharibika kadri tunavyotengeneza. Namwomba Mheshimiwa Waziri aangalie utaratibu mpya wa kuajiri watumishi kwenye Kitengo cha Mizani wapate ajira ya kudumu wakiwa na uhakika kwamba sasa hiyo kazi wamekabidhiwa na naamimi kwamba wataisimamia katika utaratibu unaostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine niombe vilevile kupata hawa watumishi wengine wa TANROADS utakuta wanaajiriwa kwa mikataba miaka mitatu, minne, wakati zinapokuja kutangazwa nafasi za ajira na wao wanaambiwa waende wakaombe. Wanapofika kule wanakosa, hii inawavunja moyo, lakini kubwa zaidi tunaajiri wengine wapya ambao wanakuja kuanza kujifunza kazi. Ningeomba Wizara wakati wa kuajiri watumishi, tuwachukue watumishi angalau wamekaa TANROADS kwa miaka mitatu au minne wakaajiriwa moja kwa moja, waende wakafanye kazi wanaoijua. Naamini kabisa tukienda hivyo tutafanya kazi mambo mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, niingie upande mwingine wa TRC. Nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo ameifanya katika uwekezaji wa reli, tunaona reli ya SGR loti zote sita ziko motomoto. Tumeona ukarabati mkubwa ambao unafanyika katika reli ya kati. Ombi langu kwa Serikali, kwanza nitumie fursa hii kumpongeza Mtendaji Mkuu wa TRC, pamoja na menejimenti yake, tumeshuhudia hapa Wabunge wanalalamika kupanda kwa miradi kupitia riba katika miradi ambayo imefungwa na TRC katika SGR hakuna kupanda kwa mradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nini maana yake, ni ubunifu mkubwa ambao amefanya mtendaji huyu na timu yake. Sasa ombi langu katika hili Mheshimiwa Waziri, hii ni fedha yetu tumetoa, lakini naamini hata kwenye barabara fedha zetu tunatoa, sasa tufike mahali tuje katika utaratibu waliotumia TRC katika kufunga mikataba. Tufuate utaratibu huu pia katika kufunga mikataba ya barabara zetu, isije ikajipandisha zaidi, ikawa tunalipa riba ambazo hazina sababu na tunashindwa kusonga mbele kutengeneza barabara kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna changamoto TRC pamoja na uwekezaji mkubwa, ombi langu kwa Serikali, nilikuwa mfanyakazi wa Railway. Kipindi cha nyuma kulikuwa na mabwawa matatu pale la Igandu, Kidete pamoja na Kimangia. Mabwawa yale yalikuwa yanapunguza kasi ya maji na kwenda kufanya uharibifu wa reli katika kipande cha Kilosa na Kideti, ombi langu mabwawa yale yalikuwa chini ya Railway sasa hivi yako chini ya Wizara ya Kilimo na Umwagiliaji, niombe Wizara ya Uchukuzi, Wizara ya Kilimo na Umwagiliaji yaangalie utaratibu gani…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa mchango mzuri, kengele ya pili.

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga hoja. (Makofi)