Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Awali ya yote ninamshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa nguvu na afya kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa, pia nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri zinazoendelea kufanyika chini ya Mama yetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu kwa upande wa miundombinu pamoja na ujenzi wa barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kwanza barabara. Barabara ni uchumi, barabara ni maendeleo, barabara ni mawasiliano, jambo ambalo mimi ninaishauri Serikali, ni kweli wamekuwa wakijijitahidi kujenga barabara lakini mimi ninao ushauri, tunapojenga barabara hebu tuangalie vipaumbele vya Serikali hasa kwa upande wa mambo ya uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano unajenga barabara, nimekuwa nikizungumzia sana barabara za Kyerwa, sizungumzii ili zijengwe tu zile barabara kwa mfano barabara ya Mgakolongo kwenda mpaka Mlongo ni barabara inayounganisha nchi ya Uganda pia ni barabara ambayo ni muhimu sana, hasa vivutio ambavyo viko Kyerwa tunayo Ibanda na Rumanyika hifadhi za Ibanda na Rumanyika ambayo ni muhimu sana. Waganda wamekuja wakija kule kwetu pamoja na watu wa Rwanda kuja kupumzika kipindi cha sikukuu. Kwa hiyo niombe sana Serikali inapojenga barabara hebu tuangalie, hizi barabara umuhimu wake ni upi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo jingine pamoja na kusemea hizi barabara zetu kwa nchi nzima ya Tanzania tunalo zao la kiuchumi zao la kimakakati zao la kahawa, hakuna Wilaya ambayo inalima kahawa nyingi kama Wilaya ya Kyerwa. Kwa hiyo, wananchi wamekuwa wakipata adha sana pamoja na wafanyabiashara kusafirisha yale mazao, kwa sababu barabara zetu unakuta mara nyingi hazijatengenezwa haziko vizuri. Kwa hiyo niombe sana hili ninalirudia na nimekuwa nikilisemea sana, siwezi kuruka sarakasi lakini mimi ni Mtumishi wa Mungu nisije nikakunyanganya hicho kiti niombe sana, barabara hii umeiweka kwenye bajeti na mmeshatangaza barabara ya Mrushaka kilometa 50, kutoka makao makuu ya Wilaya kwenda mpaka Karagwe. Niombe sana Waziri, tender imeshatangazwa na imeshafunguliwa, sasa huu mchakato wa kuanza barabara naomba ukamilike haraka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia barabara ya Mgakorongo kwenda mpaka Murongo, barabara hii ni muhimu sana kama nilivyoieleza niombe sana umetuahidi mnajenga kilomita 50 tukoka Murongo kuja mpaka Kigarama sasa ninaomba mchakato huu ukamilike haraka ili barabara zetu hizi ziweze kupitika na ziweze kuongeza uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine ni suala la bandari. Bandari ni muhimu sana, hasa ukiangalia bandari yetu tunazungukwa na nchi nyingi sana ambazo ni muhimu Serikali imeanza kuboresha nasi kama Kamati tumekwenda tumejionea uboreshaji unaoendelea kwenye bandari zetu. Ninaomba sana Serikali iendelee kuongeza nguvu ili hizi bandari zetu ziweze kushindana na bandari nyingine, ninaamini bandari yetu itakapokuwa imeboreshwa nina uhakika majirani zetu watakimbilia kwetu kwa sababu ndiyo karibu. Kwa hiyo, niombe sana tuwezeshe Mtendaji wetu tumpe fedha za kutosha, yale mahitaji yake anayohitaji kuboresha bandari yetu aweze kuiboresha na bahati nzuri ni mbunifu mzuri. Tumuunge mkono, tumtie moyo ili asonge mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nisemehe upande wa meli. Nchi yetu imejaliwa tunayo Maziwa, tuna Mito, tuna Bahari, ninaamini tukizitumia vizuri tunaweza tukakuza uchumi wa Taifa letu. Tayari Serikali imeanza kujenga meli kubwa, tunayo MV. Mwanza Hapa Kazi Tu na nyingine, niombe sana Serikali iendelee kuweka nguvu kubwa tutumie haya Maziwa yetu, tutumie bahari tulizonazo ili kuongeza uchumi lakini pia kurahisha usafiri wa majini. MV. Mwanza pale Hapa Kazi Tu tuliitembelea ni nzuri na kazi inaenda vizuri sasa ninaomba Mheshimiwa Waziri, pale mmemuweka kijana ambaye anafanyakazi vizuri, muongezeeni nguvu, mpeni pesa aendelee kusimamia. Pia niombe Mheshimiwa Waziri niombe sana hawa watu ambao mmewaweka na mmewapa kazi kubwa sana wanafanyakazi nzuri wasiendelee kukaimu, mtu anapokuwa anakaimu anakuwa hajiamini. Kwa hiyo niombe sana Serikali iweke pesa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambao nilisemee ni kuipongeza sana Serikali na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo anaendelea kuendeleza kazi ambazo alianza mtangulizi wake na yeye akiwa Makamu wa Rais tunaona anaendelea kuweka nguvu kubwa kwa upande wa SGR, SGR ni muhimu sana. Kwa hiyo, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri endeleeni kuongeza nguvu hizi kelele panapokuwepo na ushindani lazima kelele zitokee. Kwa hiyo, ninaomba nisimamie haki, mtende haki lakini vipande vilivyobaki viweze kukamilishwa ili kurahisha usafirishaji katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine tukimaliza kujenga hizi reli zetu za SGR, ninyi wote ni mashahidi barabara zetu zimekuwa zikiharibika sana kwa sababu ya magari ya mizigo.

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa mchango mzuri, kengele ya pili.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaomba sana Serikali iweke nguvu mkamilishe, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)