Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Ujenzi. Nianze kwa kuishukuru sana Serikali kwa sisi Ludewa kwenye ile barabara inayoanzia Njombe kwa maana ya Itoni Ludewa mpaka Manda tumeweza kupata mkandarasi kwa ajili ya kujenga lami kiwango cha zege. Mradi huu unakadiriwa kutumia kiasi cha shilingi bilioni 95 na pia nishukuru ule mradi mwingine wa Mawengi hadi Lusitu nao ujenzi wa lami kwa kiwango cha zege unaendelea vizuri na sasa umefikia asilimia 86.

Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais na Waziri wa Fedha, hivi karibuni wameweza kulipa shilingi bilioni 45 kwa hiyo nishukuru sana Serikali kazi inaendelea vizuri. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kuiomba Serikali kwamba barabara hii haijafika bado Makao Makuu ya Wilaya imeishia pale Mawengi kutoka pale mpaka Makao Makuu ya Wilaya kwa maana ya Lot III inaanzia Mawengi mpaka Ngalawale pale Ludewa Mjini unafika Ngalawale. Kwa hiyo naomba sana barabara hii iweze kuendelea iweze kufika Makao Makuu ya Wilaya ili mwananchi anavyotoka Makao Makuu ya wilaya ya Ludewa kwenda Mkoani apite kwenye lami.

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika ninapende kuishukuru Wizara ya Ujenzi, Wizara hii ndiyo Mawaziri wake wamekuja Ludewa mara nyingi Zaidi, Mheshimiwa Kasekenya Naibu Waziri wa Ujenzi amekuja Ludewa mara mbili tokea mimi nimekuwa Mbunge. Ninamshukuru sana tulikwenda nae daraja la Luhuhu pale na Waziri wa Ujenzi halikadhalika tulikuwa naye Ludewa hasa ambacho napenda kushukuru baada ya kupata maafa ya madaraja kukatika nashukuru Serikali iliweza kumtuma Naibu Waziri wa Ujenzi, kwa kweli wana Ludewa walifarijika sana kumuona Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi.

Mheshimiwa Spika, hii barabara umeweza kuiona kuanzia pale Njombe mpaka Kipingu darajani, wananchi wanaomba sana barabara hii iweze kufika Manda kwa sababu Wilaya ya Ludewa ina rasilimali nyingi. Tunalo Ziwa Nyasa na sasa wananchi wameelimika wanataka kuanza miradi ya ufugaji wa samaki kwenye vizimba na nimeandika barua kwa Waziri wa Uvuvi kuomba pale watujengee soko la wavuvi pale Manda Nsungu. Hii barabara ikikamilika itafungua sana uchumi wa kule na kwa sabbu Waziri wa Mambo ya Ndani ametuletea Maafisa Uhamiaji pale itakuwa ni rahisi zaidi kuanzisha hata biashara na nchi jirani ya Malawi.

Mheshimiwa Spika, barabara hii ni muhimu sana na sasa tuna uwekezaji mkubwa wa makaa ya mawe ule Mlima Kimelembe kwenye hii barabara inayoanzia Itoni, Ludewa Manda Mlima Kimelembe pale wananchi wengi wa Ludewa wamepata ajali na magari na mabasi ya abiria yameanguka sana na kupoteza maisha ya watu na kuwasababishia wengine ulemavu. Kwa hiyo naomba sana hii barabara iweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna uwekezaji wa makaa ya mawe, tuna kampuni inaitwa Maxcoal Ludewa wanatarajia kusafirisha makaa ya mawe kuwa na lori 4,000 kwa mwezi. Lori 4,000 kwa mwezi ni nyingi sana. Kwa hiyo tunahitaji ile barabara iweze kukamilika ili iweze kufungua uchumi wa Wilaya yetu.

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika kuna barabara nimshukuru Kaka yangu Dkt. Joseph Mhagama Mbunge wa Madaba, asubuhi amezungumzia sana barabara inayoanzia Mkiu kwenda Liganga mpaka Madaba, barabara hii ni muhimu sana. Wananchi wa Ludewa wanaona kama wanaambiwa wale ugali kwa harufu ya nyama choma au kwa picha ya Samaki, kwa sabbu miaka yote tumekuwa tukielezwa kwamba tusubirie mradi wa Mchuchuma na Liganga uanze Mwekezaji ndipo ajenge ile barabara. Wazo hili wananchi wa Ludewa wanaona kama linawacheleweshea maendeleo, wanaamini kwamba inapaswa kuanza barabara ndipo mwekezaji aje. Kwa hiyo tunakuwa tunawekwa pembeni kwenye mipango mingine ya kupata fursa za kujengewa barabara ile kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo ninashukuru sana nimeona tumewekewa pale mita 400 za lami, eneo hili Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi umeupiga mwingi kwa sababu kuna ajali nyingi sana zilikuwa zinatokea pale, kutoka Kibao njiapanda ya Lugarawa unaacha zege unavyokuwa unaenda Lugarawa pale mmetupa mita 400 tunaamini kabla bajeti hii unavyohitimisha utakuwa umetufikiria utuongezee tena kwa sababu mita 400 ni kama viwanja vinne vya mpira, tunashukuru kwa sababu eneo lilikuwa korofi sana ila tunaomba utufikirie tupate hata kilometa Mbili angalau pale tutakuwa tumetibu tatizo.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna barabara inayoanzia Ludewa kwenda Lupingu nayo ilipata maafa sana, milima iliporomoka mimi nilikwenda kuwapa pole wananchi, ule udongo na vifusi, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mkuu wa Mkoa wa Njombe na Meneja wa TANROADS tulivyopata maafa haya walihamia kule walikaa na wananchi muda wote, ila sasa tunaomba barabara hii itengewe fedha za kutosha kuweza kutoa vifusi na kujenga mitaro ili isiharibike.

Mheshimiwa Spika, kuna barabara nyingine inaitwa Lupingu - Makonde - Lumbila hii ni barabara ya mpakani, Ziwa Nyasa tunajua historia ya hili Ziwa tumekuwa tukirushiana maneno na nchi Jirani, ndiyo maana Wabunge watangulizi wangu kuanzia Horace Kolimba, Chrispine Mponda na Mathias Kihaule walisisitiza sana kwamba barabara hii ni muhimu sana kwa ulinzi na usalama wa nchi yetu, na sisi tukakubaliana pale na Mkoa kwamba tuandike barua ofisi ya Waziri Mkuu kuweza kuomba barabara hii ichukuliwe kama ni ya muhimu sana kiulinzi na usalama, hasa jirani yetu maneno yalikuwepo kuwepo hapo nyuma nafikiri mnaelewa vizuri. Kwa hiyo, barabara hii tunaomba sana kwa sababu kule mwambao ule usafiri ambao unategemewa wa meli ile meli imefanya route moja tu kwa mwaka huu ikaharibika mpaka sasa imekuwa matengenezo.

Mheshimiwa Spika, nilimuona Naibu Waziri wa Uchukuzi amekwenda pale alijitahidi kuwakaripia kidogo lakini wananchi wa leo wanauelewa mkubwa sana, wanajaribu kupima wale watumishi walioko pale hivi wanawahurumia wananchi kiasi gani. Kwa sababu wananchi wanazama kwenye maji wanatumia maboti, bei ya vifaa vya ujenzi inakuwa kubwa sana kutokana na kukosekana kwa usafiri wa uhakika, kwa hiyo saruji hata ujenzi wa Serikali miundombinu kwenye mashule, kwenye vituo vya afya na zahanati inakuwa ni changamoto sana, gharama zinaongezeka sana. Tulipata shida sana ujenzi wa madarasa manne shule ya Sekondari Makonde wananchi wanabeba mizigo kichwani, kwa hiyo naomba sana hii barabara Serikali iweze kuipa uzito wa kipekee na kuendelea nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile ile meli ni muhimu sana tumekuwa tukiongea hapa na jirani yangu Mheshimiwa Eng. Stella Manyanya wananchi kule wametukalia kooni wanaona kama mimi na Mheshimiwa Manyanya hatusemi. Mwanzoni walikuwa wanalalamikia juu ya shape ya ile meli lile Ziwa Nyasa lina mawimbi makali sana.

SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa Kmoga, muda wako umekwisha.

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Nakushukuru sana baada ya hayo machache naunga mkono hoja. (Makofi)