Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ya ujenzi wa Taifa letu hasa kwa uzalendo wake mkubwa kwa nchi yetu, leo naomba kuanza mchango wangu kwa kuanza na Jimbo au Wilaya ya Liwale.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Liwale iko Mkoa wa Lindi, ni Wilaya miongoni mwa Wilaya kongwe hapa nchini tangu mwaka 1975. Wilaya hii inafikika kwa usafiri wa aina moja tu nao ni usafiri wa barabara na barabara zinazoingia na kutoka Liwale ni mbili tu; moja barabara ya Nangurukuru-Liwale na pili ni barabara ya Nachingwea-Liwale. Hivyo basi naiomba Serikali ione umuhimu wa kuzijenga barabara hizi kwa kiwango cha lami.

Pili nichukue nafasi hii sasa kuipongeza sana Serikali kwa kutekeleza kwa vitendo kwenye miradi mbalimbali iliyoko kwenye Wizara hii. Nikianza na Mradi wa SGR, pamoja na kumpongeza Mheshimiwa Rais nampongeza pia Mtendaji Mkuu wa TRC kwa kazi kubwa ya utekelezaji wa mradi huu kwa weledi mkubwa. Ushauri wangu hapa ni kwamba Serikali isijenge mradi huu kwa kutumia mkandarasi mmoja kwani ni hatari kwa usalama wa reli yetu na nchi mzima kwa ujumla. Hivyo ni bora kukawa na kampuni zaidi ya moja kwa vipande tofauti tofauti kama ilivyo sasa.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa bandari pamoja na mafanikio makubwa yaliyofikiwa na bandari zetu hapa nchini, hasa chini ya uongozi wa Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na Mtendaji Mkuu wa Bandari zetu. Lakini ni ukweli usiopingika kwamba bandari yetu ya Dar es Salaam haiwezi tena kubeba mzigo mkubwa hata kwa kuipanua tena na tena kwani tayari eneo limeshakuwa finyu. Hivyo basi Serikali ione umuhimu wa kujenga bandari ya kisasa nje ya Mji wa Dar es salam. Hapa nazungumzia Bandara ya Mtwara na Tanga, bandari hizi ziimarishwe zaidi ili kukabiliana na mzigo mkubwa unaotarajiwa nchini. Na hii niiombe tena Serikali kufanya mapitio ya mikataba ya Bandari ya Bagamoyo na ikionekana inaisaidia nchi yetu mradi huu uharakishwe zaidi.