Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.
Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha uendelezaji wa miradi ya kimkakati na pia utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miezi kumi ya bajeti inayoishia Juni, 2022 Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi imetekeleza miradi mingi ya miundombinu ya barabara, reli, bandari, na uimarishaji wa safari za anga ikiwemo ujenzi na uboreshaji wa viwanja vya ndege. Utekezaji huu ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM 2020-2025.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa CCM na Serikali nzima kwa hatua nzuri za utekelezaji wa mradi wa kihistoria wa ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR pamoja na uboreshaji wa bandari utaimarisha kwa kiasi kikubwa uchumi wa nchi yetu. SGR na Bandari ni nguzo imara ya kiushindani katika biashara ya usafirishaji wa ndani na nchi za maziwa makuu na hata za Kusini mwa Afrika na Kati. Bandari za Tanzania ni lango la usafirishaji kwa Zambia, Malawi, DR Congo, Uganda, Burundi, Rwanda, Sudan ya Kusini na hata Zimbabwe na Msumbiji.

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya kazi kubwa kuhakikisha ujenzi wa SGR unaendelea kwa kasi ile ile na pia napongeza jitihada za kuendelea kutafuta vyanzo vya fedha vya masharti nafuu kugharamia ujenzi huo. Pamoja na ujenzi wa reli ya kisasa, Serikali imefanya maboresho makubwa ya miundombinu na huduma katika bandari zetu hususan bandari ya Dar es Salaam ili kukabiliana na ushindani mkubwa wa bandari zingine za ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika. Bandari ya Dar es Salaam inakumbana na ushindani mkubwa toka Bandari za Mombasa (Kenya), Beira (Msumbiji), Nacala (Msumbiji), Durban (Afrika Kusini), Lobito (Angola) na Walvis Bay (Namibia). Maboresho ya bandari zetu iendane na kuondoa changamoto zingine ambazo zinasabisha gharama kubwa za usafirishaji kwa bandari zetu na kusababisha kupoteza biashara ya usafirishaji kwa bandari shindani. Ufanisi wa bandari unategemea pia maboresho ya barabara, Reli ya Kati (TRL), Reli ya TAZARA, utendaji wenye tija wa wadau wote wa bandari na hata watumishi ili kupunguza gharama za usafirishaji kwa wateja wa bandari zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa karibu asilimia 72 ya mzigo wote wa nchi za nje unaosafirishwa kwa kupitia Dar es Salaam Corridor ambapo DR Congo ni asilimia 36, Zambia asilimia 31, na Malawi asilimia tano. Pamoja na fursa za kijiografia ya bandari zetu, mzigo unaopita sasa kwenye Bandari ya Dar es Salaam, ni asilimia 50 tu ya biashara yote ambayo kwa sasa inashikiliwa na bandari shindani. Kwa ajili ya kunusuru biashara hii inayopotea na kuchukuliwa na bandari shindani, Serikali ichukue hatua za haraka kuboresha huduma za TAZARA ikiwa ni pamoja ya maboresho ya miundombinu ya reli, ununuzi wa vichwa vya treni, mabehewa, na vitendea kazi vingine.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Serikali kwa haraka ishughulikie maboresho ya mkataba wa TAZARA na kisha kutafuta fedha za masharti nafuu angalau kiasi cha shilingi bilioni 200. Katika kipindi hiki cha ushindani mkubwa na hata mfumuko wa bei wa mafuta ya petroli, mbolea na bidhaa mbalimbali, usafirishaji wa reli ni mojawapo ya suluhisho kubwa la kupunguza mzigo wa bei kubwa kwa wateja wa bandari zetu na hata wananchi. Kutokana na TAZARA kuhudumia mzigo wa tani chini ya 200,000 (asilimia sita tu) kati ya tani milioni tatu ni kiasi kidogo sana na kupelekea mzigo kuelemea barabara zetu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na maboresha ya reli ya TAZARA napendekeza kuendelea na ujenzi wa bandari kavu ya Mbeya ambayo ina fursa kubwa katika kipindi hiki katika kuwezesha kupunguza gharama za kusafirisha kwa wateja wa bandari na hata kupunguza bei za mafuta ya petroli, pembejeo na mazao ya kilimo. Bandari kavu ya Mbeya ni njia panda kwa wateja wa nchi za Malawi, Zambia, DRC Lubumbashi na hata kwa Zimbabwe na Msumbiji. Serikali ichukue hatua za haraka kuinusuru reli ya TAZARA hata ikibidi kurekebisha mikataba ya umiliki na uongozi ili mradi iendeshwe kwa tija. Serikali ichukue hatua za makusudi kwa kutumia zaidi TAZARA kusafirisha mizigo ambayo imeelemea hata uwezo wa barabara zetu. Usafirishaji wa mizigo kwa kutumia TAZARA ilenge kupunguza gharama za mafuta ya petroli, pembejeo kwa wakulima na wakati huo kupunguza gharama za kusafirisha mazao ya wakulima.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuboresha TAZARA, napendekeza kukamilisha taratibu za ujenzi wa bandari kavu ya Mbeya ambapo Mamlaka ya Bandari kwa kipindi kirefu wamewahakikishia wananchi kulipa fidia ya eneo lao wanalolichukua.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto za mfumuko wa bei za mafuta na pembejeo, kuna fursa kubwa na hasa mahitaji makubwa ya mazao ya kilimo kwa soko la ndani na nje. Uzalishaji kwa tija unategemea kwa kiasi kikubwa ubora wa miundombinu ya barabara, reli na hata anga. Serikali iweke msukumo zaidi kwenye kuboresha miundombinu ya barabara kurahisisha usafirishaji wa pembejeo na mazao ya kilimo. Kutokana na fursa za uzalishaji mkubwa kwa Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, napendekeza muendelezo wa uboreshaji wa barabara za TANZAM kipande cha Igawa - Tunduma; barabara ya bypass ya Uyole - Songwe; barabara ya Mbalizi – Shigamba – Isongole kutokana na uzalishaji wa mazao ya kilimo; barabara ya Mbalizi – Galula – Makongosi kutokana na uzalishaji mkubwa wa mazao ya kilimo na madini; na pia barabara ya Isyonje – Kikondo – Makete ambayo ni muhimu sana katika kusafirisha mazao ya kilimo ikiwemo maua, parachichi na viazi kwa soko la nje.

Mheshimiwa Spika, uboreshaji wa barabara hizi pamoja na uwanja wa ndege wa Songwe ni muhimu sana kwa usafirishaji wa mazao yetu kwa soko la ndani na nje, na kwa kiasi kikubwa utaongeza mapato ya fedha za kigeni. Maboresho ya uwanja wa ndege wa Songwe uende sambamba na ujenzi wa maghala mahususi wa maua, mbogamboga, parachichi, nyama, viwanda vya kuongeza thamani za mazao na madini, na EPZ/ Industrial Park.

Mheshimiwa Spika, kutokana na ajali za mara kwa mara za Mlima Iwambi Mbalizi na msongamano wa magari yakiwemo malori ya mizigo na mafuta ya petroli, naomba Serikali kuchukua hatua za haraka kujenga barabara ya mchepuo ya Uyole - Songwe kilometa 40 na pia upanuzi wa barabara ya TANZAM kipande cha Uyole mpaka Ifisi/Uwanja wa Ndege wa Songwe.

Mheshimiwa Spika, katika vipindi mbalimbali, viongozi wa Kitaifa waliagiza upanuzi wa kipande hiki cha TANZAM pamoja na ujenzi wa bypass ya Mbalizi – Iwambi kilometa 6.5. Pamoja na kwamba mikakati hiyo ilikuwa ya muda mfupi, mpaka leo hii huo mkakati haujatekelezwa na wananchi wanaendelea kupoteza maisha kwa ajali za mara kwa mara katika eneo hilo. Hatari zaidi ni kwa magari makubwa yanayosafirisha mafuta kupita barabara yenye msongamano mkubwa katikati ya Jiji la Mbeya na Mji wa Mbalizi. Msongamano wa magari makubwa katika barabara ya TANZAM ni sehemu ya changamoto zinazopelekea bandari zetu kupoteza biashara kwa bandari shindani.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.