Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, naungana na viongozi wenzangu wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa majaliwa yake kwetu sote kwa jinsi anavyolijalia Taifa letu baraka zake kupitia majanga mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, viongozi na watendaji wengine wote Serikalini kwa jinsi wanavyosimamia utekelezaji wa Ilani ya CCM 2020 – 2025, hongereni sana.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mbulu Mjini nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu wa Wizara, Naibu Makatibu Wakuu, watendaji wote wa Wizara hii kwa utendaji wao uliotukuka, kwanza kutusikiliza na kufanyia kazi maoni yetu. Kwani ni ukweli usiopingika kuwa tatizo la ukosefu fedha na mahitaji ya ujenzi wa miundombinu ni changamoto katika utekelezaji wa majukumu yao. Aidha, kwa namna ya pekee napenda kumpongeza Mtendaji Mkuu wa TANROADS nchini Engineer Rogatus na watendaji wake wa makao makuu, Meneja wa TANROADS wa Mkoa wa Manyara na watendaji wote wa TANROADS Mkoa kwa kuhakikisha barabara za Jimbo la Mbulu Mjini zinapitika wakati wote pamoja na jiografia yetu kuwa juu ya Bonde la Ufa.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe mchango wangu kupitia hotuba ya Wizara hii; kwanza tunaishukuru sana Serikali kwa kutujengea Daraja la Magara kwani wananchi wa Wilaya ya Mbulu ni wanufaikaji wakubwa sana. Tunaiomba sana Serikali itusaidie kumwezesha kupata fedha za kuweka zege kilometa tano katika Mlima Magara Meneja wa TANROADS Mkoa wa Manyara kwani tunatumia hela nyingi kuchonga na kuweka changarawe kila mwaka na pindi mvua ikinyesha mara moja tu barabara hiyo hujifunga bila usafiri na meneja wetu anatumia fedha nyingine zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa barabara ya Karatu - Mbulu, - Haydom – Meatu – Sibiti - Lalago kilometa 389 kwa kiwango cha lami tunaishukuru sana Serikali kwa hatua ya kumpata mkandarasi wa kilometa 25 kipande cha Mbulu – Garbabi. Hata hivyo tunaomba mkandarasi aanze kabla ya Julai, 2022. Serikali iharakishe mchakato wa manunuzi ya tender kwa kilometa 25 kipande cha Garbabi kilometa 25 Labay ili kujibu kiu na matarajio ya wananchi majimbo sita wanasubiri kwa hamu barabara hii.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mji wa Mbulu ni miongoni mwa miji mikongwe iliyoanzishwa na wakoloni nchini na kwa kuwa mji huu uko juu ya Bonde la Ufa na barabara zinazotuunganisha na miji ya Arusha na Babati zilizo fupi ni lazima upite Mbulu - Magara - Mbuyu wa Mjerumani kilometa 48 mpaka Arusha badala ya kupitia Karatu kilometa 228 na Mbulu - Kuta- Babati kilometa 68 badala ya 124 kupitia Dareda. Hivyo basi tunaiomba Serikali itupatie fedha za zege kilometa 13 kwenye maeneo hatarishi sana kwenye barabara hizo.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto ya upatikanaji wa fedha za kutosha katika Mfuko wa Barabara kwa mapato ya ndani na wafadhili, ni muhimu sasa Serikali ikae kikao cha pamoja na wachumi wabobezi wa ndani na Kamati ya Bajeti kwa haraka ili kupata vyanzo vipya vya mapato na kuleta mapendekezo ya Finance Bill kabla ya Bunge letu kuhitimisha ili kusaidia utatuzi wa jambo hili.

Mheshimiwa Spika, tunaishauri Serikali kwa kushirikiana na Wizara zingine mtambuka wakae kuangalia upya sheria za usimamizi na utunzaji wa barabara kukabiliana na uharibifu wa miundombinu na mwingiliano katika kushauri, kuelimisha na kuchukua hatua inapobidi.

Mheshimiwa Spika, mwisho ninaomba Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri wafanye ziara ya kutembelea barabara ya Mbuyu wa Mjerumani, Magara, Mbulu na Babati, Kiru, Mbulu kwani kwa heshima na staha siyo vizuri mimi kushika shilingi ya Mheshimiwa Waziri wakati hajui mazingira ninayoisemea. Kwani barabara hizo ni changamoto kubwa sana kwa wananchi wa Jimbo la Mbulu Mjini japo kuwa TANROADS Mkoa wa Manyara wamejitahidi sana japo kwa gharama kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, naunga hoja mkono kwa asilimia mia moja na naomba kuwasilisha.