Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Profesa Makame Mbarawa na Naibu Mawaziri wake wawili; Mheshimiwa Atupele Mwakibete na Mheshimiwa Godfrey Kasekenya kwa kazi kubwa wanazofanya kwenye kutengeneza mitandao ya barabara na ujenzi wa miundombinu mbalimbali nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, mimi nitachangia kuhusu reli ya TAZARA na changamoto za barabara katika Jimbo la Moshi Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa kwanza ni kuhusu umuhimu wa reli ya uhuru ya TAZARA. Reli hii inayomilikiwa na Serikali ya Tanzania (50%) na Zambia (50%) ilianza kazi yake mwaka 1976 ikiwa na mashine 102. Lakini taarifa za hivi karibuni zinaonesha kwamba hivi sasa ziko engine 14 tu.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hii, changamoto kubwa ya TAZARA kwa sasa hivi ni vitendea kazi duni. Reli hii ilianzishwa ikilenga kusafirisha shaba ya Zambia pamoja na kuingiza bidhaa Zambia kupitia bandari ya Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, pamoja na ukweli kwamba reli hii ni kitega uchumi muhimu, katika miaka ya hivi karibuni matumizi ya reli hii yamedorora sana. Mizigo mingi kwenda nchi jirani husafirishwa kwa malori jambo linalosababisha uharibifu mkubwa wa barabara. Kama hatua stahiki zingechukuliwa kuboresha miundombinu ya reli hii, mizigo kwenda Zambia, Malawi na eneo la Kusini ya Congo ingesafirishwa kutokea bandari ya Dar es Salaam na kuipatia Serikali kipato cha uhakika.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa pili ni kuhusu changamoto za barabara katika Jimbo langu la Moshi Vijijini. Kata ya Mabogini inakojengwa Hospitali ya Wilaya kuna changamoto kubwa ya ubovu wa miundombinu ya barabara. Hii inajumuisha barabara ya TPC - Mabogini - Kahe yenye urefu wa kilometa 11.4. Barabara hii imekuwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi toka mwaka 2010 ambapo waliahidi kuitengeneza kwa kiwango cha lami, lakini hadi leo ujenzi haujatekelezwa. Kwa kuwa iko chini ya TARURA, na kwa kuzingatia bajeti finyu ya TARURA, hadi leo ahadi hiyo haijatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, ni kutokana na hali hiyo, nikiwa kama mwakilishi wa wananchi hawa, nilipeleka ombi kwa Baraza la Maendeleo la Mkoa wa Kilimanjaro (RCC) kuipandisha hadhi na kuiombea ihudumiwe na Wakala wa Barabara (TANROADS). Ombi hili liliridhiwa na RCC na bodi toka mwaka wa 2021.

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Moshi Vijijini, barabara ya Umbwe - Sere inahudumiwa na TANROADS. Wameshaweka mitaro katika baadhi ya maeneo na haijajengwa hata kidogo kwa kiwango cha lami. Barabara hii ni muhimu kwani ni sehemu ya kusafirisha watalii kwenda Mlima Kilimanjaro kupitia njia ya Umbwe.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali kwa kuendeleza ujenzi wa barabara ya Kiboriloni - Kikarara - Tsuduni - Kidia ambayo itaunganisha makao makuu ya Halmashauri ya Moshi kwa kiwango cha lami. Barabara hii inajengwa na TANROADS na bado haijakamilika.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kibosho Shine - Kwa Raphael - International School ilikuwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi toka mwaka 2005 na inajengwa na TANROADS lakini hadi leo haijakamilika. Bado kipande cha kama kilometa nane.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Rau - Uru - Shimbwe yenye urefu wa zaidi ya kilometa 13 ilikuwa kwenye ahadi ya kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahadi hii ilitolewa na Rais. Pamoja na kuikumbusha Serikali kwa kuuliza swali Bungeni, bado ujenzi wa barabara hii haujapewa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Uru - Kishumundu - Materuni iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa mpango wa kuijenga kwa kiwango cha lami. Lakini hadi sasa hatujaona nia ya Serikali kutekeleza ahadi hii.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo ya hapo juu, naishauri Serikali ifanye yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza ninaishauri Serikali za Tanzania na Zambia wakae na kuangalia uwezekano wa kuiboresha reli ya Uhuru. Hii ni pamoja na kufanya maboresho ya ile mikataba na sheria ya awali ya kuanzishwa mradi huu ili viendane na hali halisi ya sasa hivi tofauti na ilivyoanzishwa mwaka 1976.

Mheshimiwa Spika, pili, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi iingize barabara ya TPC - Mabogini - Kahe yenye urefu wa kilometa 11.4 kwenye mtandao wa TANROADS kwani RCC na bodi walikubaliana na ombi hili tangu mwaka wa 2021. Ninaiomba Serikali itenge fedha za kutosha na ujenzi wa barabara hii uanze mara moja kwani Hospitali ya Wilaya inajengwa eneo hili.

Mheshimiwa Spika, tatu, ninaiomba Serikali itenge fedha za kutosha na ikamilishe kipande cha barabara ya Kibosho Shine - Mto Sere kinachojengwa na TANROADS. Vilevile ninaishauri Serikali ifikirie kujenga kwa kiwango cha lami kipande cha Sere hadi geti la Umbwe la kupanda Mlima Kilimanjaro. Barabara hii ni mbovu mno pamoja na kwamba hutumika kusafirisha watalii wanaopanda Mlima Kilimanjaro kupitia njia ya Umbwe na kuingizia Serikali kipato kupitia sekta ya utalii.

Mheshimiwa Spika, nne, ninaiomba Serikali itenge kiasi cha fedha za kutosha na kukamilisha ujenzi wa barabara ya Kiboriloni - Kikarara - Tsuduni - Kidia kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, tano, ninaiomba Serikali ikamilishe ujenzi wa barabara ya Kibosho Shine - Kwa Raphael - International School kwa kiwango cha lami kama ilivyoainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi toka mwaka 2005. Ujenzi wa barabara hii umechukua zaidi ya miaka 12.

Mheshimiwa Spika, sita, ninaishauri Serikali itekeleze ahadi ya kujenga barabara ya Rau - Uru - Shimbwe kwa kiwango cha lami yenye urefu wa zaidi ya kilometa 13 kama wananchi walivyoahidiwa wakati wa kampeni.

Saba, ninaishauri Serikali itenge fedha na kuanza ujenzi wa barabara ya Uru - Kishumundu - Materuni.

Mheshimiwa Spika, baada ya ushauri niliotoa hapo juu, naunga mkono hoja.