Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nami napenda kuanza kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema kwa kutujalia kukutana hapa leo tukiwa na afya njema ili kukamilisha kazi tuliyoianza jana tarehe 23 Mei ambapo niliwasilisha hoja hii.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kukushukuru wewe binafsi, Mheshimiwa Naibu Spika na Wenyeviti wa Bunge kwa jinsi ulivyoongoza wakati wa majadiliano ya hoja hii. Aidha, nichukue fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwa wawazi na kutoa michango yao ya kina wakati wa majadiliano haya. Ninawathibitishia kwamba michango hiyo tunaichukua kwa uzito mkubwa ili kuendelea kuleta ufanisi wa utekelezaji wa majukumu ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, naomba kipekee nimshukuru Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Mheshimiwa Sulemani Moshi Kakoso kwa hoja zilizotolewa na Kamati yake. Nikiri kwamba hoja hizo ni muhimu na Wizara itazifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru Waheshimwia Wabunge wote waliochangia katika bajeti yangu. Waheshimiwa Wabunge 79 wamechangia wakati wa majadiliano ya hoja hii ambapo Waheshimiwa 70 wamechangia kwa kuongea na Waheshimiwa tisa wamechangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, muda mchache uliopita Waheshimiwa Manaibu Waziri wa Wizara yangu wamemaliza kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge kwa kuzingatia maeneo ya kisekta, ninawashukuru sana kwa jinsi ambavyo wamejibu baadhi ya hoja. Nitajaribu kujibu hoja chache zilizobakia.

Mheshimiwa Spika, aidha, naomba kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba Wizara itajibu hoja zote za Waheshimiwa Wabunge kwa maandishi na kuziwasilisha Bungeni kabla ya kuhitimishwa kwa Mkutano wa Bunge hili la bajeti unaoendelea.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nianze kuhitimisha hoja yangu kwa kutoa ufafanuzi wa ujumla kwa baadhi ya hoja zilizojitokeza. Maeneo muhimu yaliyojitokeza katika hoja nyingi za Waheshimiwa Wabunge, hoja tuliyoijadili ndani ya siku mbili ilihusu Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ambayo imegusa masuala mbalimbali yaliyojikita katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa ujenzi na ukarabati wa barabara mbalimbali nchini ikiwemo masuala ya ulipaji fidia kwa barabara na viwanja vya ndege. Waheshimiwa Wabunge wengi karibu asilimia 96 wamezungumzia mambo ya barabara. Hii inaonesha kwamba barabara ni njia moja muhimu ya usafiri na lazima Serikali tujipange kuhakikisha kwamba tunatatua matatizo ya barabara nchini.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine lililozungumziwa ni changamoto ya huduma za vivuko nchini. Mheshimiwa Naibu Waziri amelizungumzia hili lakini nami nikipata muda nitalizungumzia baadaye.

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu lililozungumziwa ni changamoto mbalimbali kuhusu usafiri wa anga na utekelezaji wa miradi ya viwanja vya ndege likiwemo suala la fidia. Hapa tena Naibu Waziri anayesimamia Sekta ya Uchukuzi amezungumiza suala la usafiri wa anga na Mheshimiwa Naibu Waziri anayesimamia Sekta ya Ujenzi amezungumzia suala la ujenzi wa viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Spika, suala jingine lililojitokeza ni ukamilishaji wa ujezi wa Reli ya Kisasa ya SGR na ukarabati wa Reli iliyopita. Eneo la SGR nitalizungumza sasa hivi nitalitolea ufafanuzi baadhi ya maeneo. Eneo jingine ambalo limezungumziwa ni uboreshaji wa huduma za usafiri wa majini hususan ujenzi wa meli mpya na ukarabati wa meli za zamani hili nitalizungumzia mimi kwa undani kidogo.

Mheshimiwa Spika, eneo jingine lilojitokeza ni masuala ya uboreshaji wa huduma za hali ya hewa hususan maslahi ya watumishi. Pamoja na kwamba Manaibu wangu wametoa ufafanuzi wa kina kwenye maeneo mbalimbali kwa kuzingatia hoja zilizotolewa, naomba sasa nitoe ufafanuzi kwa baadhi ya hoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hoja ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu zilizowasilishwa na Mheshimiwa Mwenyekiti wetu. Hoja ya kwanza ilikuwa ni kama ifuatavyo, utekelezaji wa miradi ya barabara kuu, barabara za Mikoa na ujenzi wa madaraja upo chini ya kiwango. Kamati imeona kuwa hali hii hairidhishi majibu ya hoja hiyo ni kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa miradi uko chini kutokana ya miradi mingi kuchelewa kuanza kwa sababu ya kuchelewa kutolewa kwa msamaha wa kodi ya ongezeko la thamani yaani VAT. Miradi mingi ilipata misamaha wakati wa kipindi cha mvua kwa vile ikashindwa kuanza kutokana na hali hiyo. Lakini sasa miradi mingi imeshapata msamaha wa VAT naamini speed ya kufanya miradi hiyo itaongezeka kwa kasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili, iliyowasilishwa na Mheshimiwa Mwenyekiti ni fedha ya Bajeti iliyoidhinishwa mwaka 2021/2022 zilitumika kulipa madeni badala ya kutekeleza miradi iliyokusudiwa. Majibu ya hoja hiyo ni kama ifuatavyo, hadi mwisho wa Julai mwaka huu jumla ya shilingi bilioni 418.92 zililipwa kwa ajili ya kazi za miradi ya barabara zilizofanyika katika kipindi cha Mwaka wa Fedha 2021/2022. Aidha, bajeti ya ujenzi wa barabara na madaraja katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 ilikuwa ni bilioni 491.7, shilingi bilioni 314.11 zililipwa kwa ajili ya madeni ya kuanzia mwezi Julai, 2021 hadi huko nyuma na hizi zilitolewa pesa tofauti siyo pesa za bajeti ya mwaka huu. Baadhi ya fedha za bajeti kama utaratibu ulivyo zilipelekwa kwenda kufanya matengenezo ya barabara ambazo sasa hizi zinatoka kwenye mfuko wa barabara.

Mheshimiwa Spika, hoja ya tatu, kutowepo kwa mpango unaoruhusu ujenzi wa barabara kwa kupitia ubia hii hoja iliwasilishwa na kamati yetu. Majibu ya hoja hiyo ni kama ifuatavyo, katika Mwaka wa Fedha 2022/2023 Serikali inapanga kuanza kushirikisha Sekta Binafsi katika ujenzi wa barabara na madaraja kwa kutumia utaratibu wa EPC plus Financing.

Mheshimiwa Spika, jumla mtandao wa barabara nchini ambao unasimamiwa na TANROADS kilomita 36,362 kati ya kilomita hizi kilomita 11,513 ni barabara za lami. Kwa upande mwingine hadi kufikia mwezi Mei mwaka huu jumla ya kilomita 1,206.5 zinaendelea kujengwa kwa kiwango cha lami ambayo gharama yake ni takribani shilingi trioni 2.9.

Mheshimiwa Spika, gharama za kujenga barabara zote ambazo hazina lami ambazo ni kilomita 24,849.05 inahitajika takribani shilingi trioni 37 kuweza kukamilisha mtandao wote wa lami ambazo unasimamiwa na TANROAD. Mwarobaini wa tatizo hili kuamua sasa kuanza utaratibu mpya wa kutumia EPC plus Finance maana yake nini, maana yake mtu mwenye uwezo wake, ataleta fedha, akileta fedha sisi tutaendelea kumlipa kidogokidogo lakini tunaendelea kujenga barabara. Utaratibu huu unatumika duniani kote na ndiyo utaratibu pekee tutakaoweza kutupelekea kujenga barabara kwa haraka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ziko barabara ambazo tunaamini ukizijenga leo na ukiweka tollgate utapata hela, kwa mfano barabara ya Kibaha, Mlandizi, Chalinze, Morogoro express way yenye urefu wa kilomita 205 tukijenga barabara hii kwa kutumia EPC plus Finance na tukaweka tollgate tunaamini kwamba tutaweza kupata fedha na fedha hizo zitakwenda kwenye miradi mingine. Watu wale ambao hawataki kutumia tollgate kutakuwa na njia mbadala wataweza kutumia bila matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa vile hapa tunatoa option kwa watu ambao wanauwezo watalipa pengine shilingi 3,000 shilingi 4,000 kwa trip waliyokuwa hawana uwezo watatumia barabara ya kawaida. Nafikiri hili ni jambo zuri na lazima tuendeleze. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika utaratibu huu vilevile tutafanya ukarabati wa barabara ya Igawa, Tunduma yenye urefu wa kilomita 218 na Uyole, Songwe by pass yenye urefu wa kilomita 48.9. Kuna barabara kwa mfano Handeni, Kiberashi, Kwamtoro, Singida yenye urefu kwa kilomita 411 hii tutaijenga kwa EPC plus Finance lakini hatutaweka tollgate kwa sababu wananchi wetu wa maeneo ya kule hawana uwezo wa kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna barabara kwa mfano Kidatu, Ifakara, Lupilo, Malinyi, Kilosa, Kwampepo, Londo, Kitanda, Lumecha, yenye urefu wa kilomita 486 na hii tutaijenga kwa utaratibu wa EPC plus Finance lakini hatutaweka tollgate kwa sababu wananchi wetu uwezo wao siyo mkubwa na wananchi wetu hawana njia mbadala ya kuweza kupitia. Kwa vile, tutakwenda na utaratibu huu na tunaamini tukianza utaratibu huu tutafungua kwa kiasi kikubwa mtandao wa barabara nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine iliyowasilishwa na Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati na wajumbe wengine, inasema kutokuwepo kwa bajeti ya ukarabati wa barabara zilizopandishwa hadhi. Jibu la hoja hii ni kama ifuatavyo, barabara inapopandishwa hadhi Meneja wa Mkoa husika huingiza katika mpango wake ili izingatiwe katika bajeti ya mwaka husika kupitia mfuko wa barabara. Kwa vile barabara tunapoipandisha moja kwa moja Meneja wa Mkoa anaichukua na anatoa hela kwa ajili ya ukarabati. Kwa vile kazi kubwa tunayotakiwa kama kuna changamoto ya barabara zileteni Wizarani tutazipandisha kama zimezidi vigezo then tutaweka fedha kwa ajili ya ukarabati kama taratibu na Sheria zinavyoelekeza.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine iliyotolewa na Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati na wajumbe wengine, athari za mikataba kwa Wakandarasi kwa kuchelewa kulipwa madeni. Majibu ya hoja hii ni kama ifuatavyo, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Serikali ililipa madeni ya Wakandarasi kupitia hati za madai zilizowasilishwa kwa kila mwezi hivyo kupunguza athari za ucheleweshaji. Kwa muda wa mwaka huu kwa kipindi hichi tumekuwa kila ikiletwa certificate tunailipa, leo ukienda daraja la Kigongo, Busisi hatuna deni, leo ukienda daraja la Wami hakuna deni, na miradi mingi mingi ambao hakuna deni, certificate ikiingia tunalipa. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kulijua hili kwa sababu athari ya deni ni jambo kubwa sana. Na sisi tutahakikisha mchakato ukifika Wizarani haucheleweshwi unakwenda Wizara ya Fedha naamini na Wizara ya Fedha Waziri yupo mchakato utaenda mapema ili tusicheleweshe ku-create interest rate ambayo haina faida yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna hoja nyingine inasema miradi mipya ya barabara kushindwa kuanza kutekelezwa wakati wake kwa mwaka 2021/2022 kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo fedha zake kutumika kulipa miradi ya nyuma. Majibu ya hoja suala hili ni kama ifuatavyo, hadi kufika mwezi Aprili mwaka huu mikataba ya miradi ifuatayo ilisainiwa.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa kwanza ni barabara ya Ntendo, Muze, Kilyamatundu yenye urefu wa kilomita 179 sehemu ya Ntendo, Kizungu yenye kilomita 25 ilisainiwa. Karatu, Mbulu, Haydom, Sibiti, River, Lalago, Maswa yenye urefu wa kilomita 389 sehemu ya Mbulu, Garibabi ilisainiwa yenye urefu wa kilomita 25. Matai, Kasesya yenye urefu wa kilomita 50 sehemu ya Matai, Tatanda ulisainiwa. Mradi wa Tarime, Mugumu wenye urefu wa kilomita 87.14 sehemu ya Tarime, Nyamanga ulisainiwa. Na miradi mingi ilisainiwa na sasa hizi kazi imeanza lakini utaratibu unachukua muda kwa sababu mkisaini Mkataba hatua inayofuata kwanza ni Mkandarasi kuleta performance bond baada ya kuleta performance bond kuna kipindi cha miezi kama mitatu ya mobilization kwa vile ndiyo unaona Mkataba ukishasainiwa kazi inachelewa kuanza. Lakini na Waheshimiwa wabunge naomba niwahakikishie kwamba Wizara tunajipanga na hakuna sababu ya kuchelewesha miradi.

Mheshimiwa Spika, kuna hoja ya Mheshimiwa Jerry na jana alilia bahati mbaya sana, Mkandarasi Sino Hydro Cooperation Limited anayejenga barabara BRT Phase II utendaji kazi wake ni mbovu kwa nini kapewa tena kazi ya BRT III. Majibu ni kama ifuatavyo, Kampuni ya Sino Hydro Cooperation Limited ilipatikana kwa njia ya ushindani competitive bidding ambapo alionyesha kukidhi vigezo vyote vya zabuni ikiwa ni pamoja na kuwa na gharama ya chini takribani bilioni tano ikilinganishwa na Kampuni iliyofuata, alikuwa na bei ya chini bilioni tano. Aidha, Wizara kupitia TANROADS itasimamia kikamilifu ujenzi kwa mujibu wa Mkataba.

Mheshimiwa Spika, nilifanya ziara kwenye Mradi wa BRT mara tatu na niligundua kuna mapungufu katika utendaji wa kazi na kama kawaida tulimtaka Mkandarasi arejee kazi hiyo kwa gharama yake mwenyewe. Na hivyo anavyoendelea au tunavyoendelea Mkandarasi huyo anarejea kazi hiyo kwa fedha yake mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, katika ziara ya mwisho ambayo niliifanya mwezi Aprili mwaka huu tulikubalina na Mkandarasi fly over ya makutano ya Kilwa Road na Mandela pale Uhasibu upande mmoja uweze kufunguliwa tarehe 30 na vilevile fly over ya makutano ya Chang’ombe na Nyerere tutaruhusu kupita magari tarehe 30 mwezi huu ule upande mmoja. Hii tunafanya yote kuhakikisha kwamba wananchi wa Dar es Salaam hawapati shida ya usafiri.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Mradi wa BRT umefikia actually performance actually 58.8 wakati planned performance ile iliyotarajiwa working plan ilikuwa iwe 57.5 Mkandarasi yuko nyuma ya asilimia 1.7, hii tutambana Mkandarasi na tunaendelea kumbana kuhakikisha kwamba anafanya kazi kwa speed inayotakiwa.

Mheshimiwa Spika, naomba nijikite kwenye hoja ya pili, ujenzi wa reli ya kati ya kiwango cha standard gauge. Ujenzi wa reli ya kisasa ulianza rasmi mwaka 2017 kwa Awamu ya Kwanza kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza yenye urefu wa kilomita 1,219. Ujenzi huu umegawika katika vipande vitano or lot tano, lot ya kwanza ni kutoka Dar es Salaam, Morogoro yenye urefu wa kilomita 300 gharama ya Mradi huu ni takribani dola za Kimarekani bilioni 1.215 sawa na shilingi trioni 2.7.

Mheshimiwa Spika, Mkataba ulisainiwa mwezi Februari mwaka 2017 maendeleo ya ujenzi mpaka sasa hivi Mkandarasi amefikia asilimia 96.5. Malipo yaliyolipwa kwa Mkandarasi takribani dola bilioni 1.004 gharama kwa kilomita moja ni dola za Kimarekani milioni 4.05 kwa kilomita hii pamoja na VAT. Mwendokasi wa reli hii utakuwa ni kilomita 160 itatumia umeme na uwezo wake wa kubeba mzigo itakuwa ni excel tan ya tani 35. Mkandarasi Yapi, na naomba tu niwaambie Waheshimiwa Wabunge wakati wa mchakato wa Mradi huu ilikuwa ni shida kubwa kwa sababu walichukua bidding document Makandarasi karibuni 30 lakini akarejesha Mkandarasi tu mmoja tu Yapi.

Mheshimiwa Spika, tukazungumza na Mkandarasi na kukubaliana na tukaendelea kulikuwa na maneno mengi lakini watu walikuwa hawasemi kama wanavyosema leo. Watu leo jambo kidogo linaenda huku na huku lakini na hapo kulikuwa na changamoto na tuliweza kusimamia mradi huu na kazi inaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, kipande cha pili ni kutoka Morogoro, Makutupora chenye urefu wa kilomita 422 chenye gharama takribani dola za Kimarekani bilioni 1.923 sawa na shilingi trioni 4.4 za Kitanzania. Mkataba ulisainiwa Septemba mwaka 2017 na umefikia asilimia 82.68, gharama kwa kilomita moja ni dola za Kimarekani milioni 4.55, malipo yaliyofanywa mpaka sasa hivi ni dola za Kimarekani bilioni 1.2154 Mkandarasi ni Yapi Merkezi.

Mheshimiwa Spika, kipande cha tatu ni kutoka Makutupora, Tabora chenye urefu wa kilomita 368 gharama ya ujenzi wa kipande hichi ni dola za Kimarekani bilioni 1.908 sawa na shilingi trioni 4.4, malipo ya awali ni dola za Kimarekani milioni 263.9 ambazo Mkandarasi ameshalipwa. Mkandarasi ameanza maandalizi ya utekelezaji, gharama kwa kilomita moja hapa ni dola za Kimarekani milioni 5.18 bei imepanda kwa sababu reli hapa inapita kwenye maeneo ya Rift Valley kwa vile ujenzi wake huwezi ukalinganisha na maeneo kama Dar es Salaam kwa vile gharama itapanda na mambo mengine yanaongezeka kidogo.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, dakika tatu, malizia.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kipande kinachofuata ni kipande cha Isaka, Mwanza chenye urefu wa kilomita 341, Mkataba ulisainiwa tarehe 15 Mei, 2021 mpaka sasa hivi Mkandarasi amefikia kazi ya utekelezaji ni asilimia 6.8 actually lakini aliyotakiwa kufanya iwe asilimia 6.85 kuna kuna tofauti ya asilimia 0.1 huwezi ukasema kwamba Mkandarasi huyu haja-perform. Kitu kinachokusababisha kufahamu mkandarasi ame-perform ni working plan siyo kwenda kuona, ukiona haikusababishi kusema Mkandarasi ame-perform ama haja-perform tunavyoamini sisi kutokana na namba hizi Mkandarasi ame-perform. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa tuta Mkandarasi amefikia asilimia 13.7 mbele ya mpango kazi amekwenda zaidi asilimia mbili. Gharama ya kipande hichi ni bilioni 1.32 na Mkandarasi mpaka sasa hivi amelipwa dola milioni 201.012. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipande kinachofuata Tabora, Isaka kina urefu wa kilomita 165, kipande hichi kilitangazwa zamani na wazabuni, lakini mzabuni aliyejitokeza ali-quote price ya dola za Kimarekani bilioni 1.4987 na Mkandarasi huyu alikuwa ni Motor Angelo kutoka Ureno na Transnet ya South Africa. Tenda hiyo ilifutwa na tukaamua tuje na utaratibu wa single source kama sheria inavyoelekeza. Sasa baada ya kufanya mchakato huo bei sasa imeshuka kutoka dola za Kimarekani bilioni 1.498 mpaka dola za Kimarekani milioni 712.8 bila VAT ukichukua na VAT unapata dola za Kimareka milioni 900.1, sasa ukilinganisha wewe unakuta kwamba single source hapa imeleta faida kuliko competitive bidding. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri sasa omba fedha, toa hoja.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naafiki.