Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Prof. Norman Adamson Sigalla King

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Makete

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. PROF. NORMAN A. SIGALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kunipa nafasi. Kwanza kabisa nianze kumpongeza Waziri Mheshimiwa Mbarawa na msaidizi wake kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya, lakini na mtihani mkubwa walionao wa kuhakikisha kwamba nchi hii inabadilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie maeneo machache kwa haraka haraka. Umuhimu wa Kuunganisha RAHCO na TRL. Wabunge wengi wamechangia, lakini nimepitia sheria ya uanzishwaji wa TRL pamoja na RAHCO, ambacho nimebaini majukumu ya RAHCO bado ni majukumu ya msingi sana.
Pendekezo langu ni muhimu sana RAHCO aondolewe kwenye kusimamia reli ya kati, kwa sababu aliikuta, irudi TRL lakini majukumu ya RAHCO yaendelee kwenye reli mpya zote ambazo hatujajenga ikiwemo reli ya Mtwara Corridor. Miundombinu ya reli zote mpya ambazo hazijajengwa zibaki kwa RAHCO lakini aondolewe kwenye kusimamia reli ya kati, Reli ya kati ibaki TRL. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo naomba nisisitize umuhimu wa ujenzi wa reli ya kati kama wenzangu walivyosema kwa kutoa dimension tofauti kidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa sasa duniani kote concession agreement ndio utaratibu wa uchumi wa dunia hii, uchumi wa tender ni wa kizamani kidogo nachelea kusema. Watu wanaotafuta biashara duniani anakushawishi, niko tayari kufanya a, b, c, kwa faida hii na mimi nitakupa hivi. Hivi ndivyo walivyofanya Kenya, Rwanda, Uganda, Djibouti na Ethiopia kujenga reli zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa utaratibu wa concession agreement nchi haingii kwenye hasara ya kulipia kwa sababu deni linalipwa na uendeshaji wa mradi husika, ndiyo maana ni muhimu sana viongozi wetu wanaoisimamia Wizara hii walione hili kwa namna ya kipekee sana ili kuharakisha ujenzi wa reli ya kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo niweke mfano mwepesi ili twende pamoja na wenzangu. TRL yenyewe kabla ya uteuzi wa Mkurugenzi Mtendaji wa sasa ilikuwa inaenda hovyo. Baada ya kuteuliwa CEO wa sasa ndugu Masanja TRL Inafanya vizuri, hii inakupa picha kwamba si wakati wote tatizo ni mfumo, kuna wakati mwingi na sehemu kubwa ya Waafrika tatizo letu ni watu wanao-execute nafasi hizo. Ukichagua CEO mbaya shirika linaweza likafa siyo kwa sababu ya mfumo, ndio maana TRL leo inafanya vizuri hakuna kilichobadilika. Sheria ni zile zile lakini baada ya kubadilisha CEO tu TRL inaenda vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashawishika kusema ni wajibu wa Serikali kuangalia kwamba competency based on recruitment, promotion and appointement become the key in terms of allowing other people to execute these positions. Lazima tuteue, tuajiri na tuwapandishe vyeo watu wetu kwa kufuata weledi usiotia mashaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kidogo habari TRA na TPA na hasa utaratibu wa kutoza kodi mbili (storage charge na wherehouse charge). Ni vizuri sana Wizara iharakishe kuondoa kabisa TRA asitoze tozo la kutunza mizigo libaki TPA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ni vizuri sana niongeze kusema habari ya simu fake.
T A A R I F A...
MHE. PROF. NORMAN A. SIGALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kidogo kuhusu simu fake. Watu wengi fasili ya simu fake wanadhani kwamba ni simu za shilingi 30,000; shilingi 25,000 ndizo simu fake. Ukweli ni kwamba simu nyingi za bei ndogo ni simu genuine. Mpaka sasa hivi, baada ya TCRA kuanzisha utaratibu huu ni asilimia 14 tu ya simu ambazo hazijahakikiwa. Wengi wanasema kwa nini waagizaji hawakufanya hivi kabla ya hapo?
Naomba niseme kwamba hili limetokana na kwamba TCRA haikuwa na mitambo ya kutambua simu fake na simu original. Baada ya kupata mitambo ni lazima tuingie sasa kwenye utaratibu wa kuhakiki simu hizo. Wengi mnajua simu fake madhara yake ni nini. Ninaweza kukupigia simu wewe nikakugombanisha, nikakufanyia madhara na mfumo wa utambuzi ukashindwa kutambua, ndiyo maana ni lazima tuwe na simu halisia ili kulinda afya na ulinzi wa watu wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nichangie kidogo kuhusu barabara. Niipongeze Serikali kwa kutenga fedha kwenye barabara, lakini naomba nisisitize barabara zinazounganisha mikoa kwa mikoa chonde chonde, ni Katavi kwenda Tabora, Kigoma kwenda Tabora barabara ya Njombe kwenda Makete kwenda Mbeya, barabara ya kutoka Chimala - Matamba kwenda Hifadhi ya Kitulo ni muhimu sana zikapewa kipaumbele kwa sababu ya uchumi wetu na kuimarisha uchumi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo niombe sana Wizara ikamilishe viwanja vya ndege hasa vile ambavyo kwa sura ya kijiografia vinaunganisha na nchi jirani. Viwanja vya Songwe - Mbeya, Mwanza, Kigoma, Mtwara na viwanja kama hivyo. Baada ya kusema hayo naunga mkono hoja.