Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, kama wote tunavyofahamu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yupo Nchini Ghana kuanzia tarehe 23 Mei, 2022 kwa ajili ya ziara ya kikazi ambapo pamoja na mambo mengine amehudhuria mdahalo wa Wakuu wa Nchi kujadili fursa zilizomo na changamoto zinazokabili Nchi za Afrika kama vile kuongezeka kwa athari za mabadiliko ya tabianchi, kupanda kwa bei ya vyakula na matumizi ya nishati endelevu.

Mheshimiwa Spika, vilevile tumeshuhudia tarehe 25 Mei, 2022 Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan akipewa Tuzo ya Mwaka 2022 ya Babacar Ndiaye kwa mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita katika Ujenzi wa Miundombinu ya usafirishaji ambayo kwa kawaida hutolewa kwa Mkuu wa Nchi iliyofanya vizuri katika sekta hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zaidi ya kupewa tuzo hiyo, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ametajwa pia kuwa miongoni mwa Viongozi 100 wenye ushawishi mkubwa Duniani kwa mujibu wa Taarifa iliyotolewa na Gazeti maarufu la TIME la tarehe 24 Mei, 2022. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua sifa hiyo kubwa aliyoipata Rais wetu ambayo inailetea nchi yetu taswira nzuri Kitaifa na Kimataifa, naomba kutumia fursa hii kuliomba Bunge hili Tukufu ambalo ni chombo cha uwakilishi wa wananchi, kuridhia Azimio la Kumpongeza Mheshimiwa Rais kama ifuatavyo.

Azimio la Bunge kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa Viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya Ujenzi wa Miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Tarehe 24 Mei, 2022 akiwa katika ziara ya Kikazi Nchini Ghana amepokea tuzo kuu ya Mjenzi Mahiri ya Babacar Ndiaye (Africa Road Builders) kwa mwaka 2022 inayotolewa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), akiwa ni Rais wa 12 kupata Tuzo hiyo tangu ilipoanzishwa Mwaka 2016. (Makofi)

Na kwa kuwa tuzo hiyo imetolewa kwa kutambua mchango wake kama mwanamke mzalendo na Rais wa kwanza wa Tanzania kupata Tuzo hiyo akiwa anaongoza Serikali ya Awamu ya Sita kwa mafanikio makubwa katika kuendeleza sekta ya miundombinu na usafirishaji hususan eneo la barabara;

Na kwa kuwa Watanzania wote tunatambua juhudi kubwa anayoifanya Mheshimiwa Rais kuendeleza miundombinu ya usafirishaji ikiwemo kusimamia na kufungua miradi mbalimbali ya ujenzi wa barabara na reli hapa nchini;

Na kwa kuwa kwa hatua nyingine wakati wa tukio la kupewa tuzo hii Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ametambuliwa kama miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani kwa mujibu wa Taarifa iliyotolewa na Gazeti la TIME la tarehe 24 Mei, 2022, jambo ambalo linaendelea kumpatia sifa kubwa Rais wetu na Taifa kwa ujumla;

Kwa hiyo basi, Bunge hili katika mkutano wake wa saba, kikao cha Thelathini na Moja, tarehe 26 Mei, 2022 linaazimia kwa kauli moja: -

Kwanza, kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kutambuliwa na kupewa Tuzo Kuu ya Mjenzi Mahiri ya Babacar Ndiaye kufuatia mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita katika ujenzi wa miundombinu nchini Tanzania. (Makofi)

Pili, kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, kwa kutambuliwa kama miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa duniani jambo linaloliletea sifa nzuri nchi yetu ya Tanzania. (Makofi/Vigelegele)

Na tatu, kuendelea kumpa moyo Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa juhudi mbalimbali anazoendelea kuzichukua katika kuiletea nchi yetu maendeleo.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, naafiki.