Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, azimio hili limechangiwa na Wabunge mbalimbali kwa sababu ya muda sitoweza kuwataja majina yao, lakini Wabunge hawa wote kwa kauli moja wamepongeza sana tuzo hii aliyoipata Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na pia kwa kutambuliwa kwake kuwa miongoni mwa viongozi 100 wenye ushawishi mkubwa duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa wameenda mbali, si tu kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa umahiri wake kwenye kuboresha miundombinu, lakini wameenda zaidi kupongeza umahiri wake katika kuboresha sekta mbalimbali ikiwemo Sekta ya Afya, Sekta ya Elimu, Sekta ya Maji na Sekta ya Kilimo ambazo ndio zinaenda kuchochea maendeleo ya nchi yetu kwa kasi sana na kuleta maendeleo ya watu na hasahasa wale wa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ni kielelezo cha uongozi bora, uongozi mahiri, sio tu kwa Tanzania bali kwa dunia nzima. Pia Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameonesha umahiri mkubwa sana katika kuboresha miundombinu katika nchi hii, jambo ambalo linaenda kuchochea uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameonyesha uthubutu kwenye kuendeleza na kusimamia miradi mikubwa ya miundombinu ambayo inaenda kuibadilisha Tanzania. Miradi hiyo ni miradi ya kuunganisha mkoa kwa mkoa, miradi ya kuunganisha Tanzania na nchi jirani, ambapo ameendeleza miundombinu ya reli ya kisasa yaani Standard Gauge Railway, barabara na madaraja makubwa nchini. Yote haya yanaenda kuleta mageuzi makubwa sana kwenye nchi yetu na kuchochea sekta mbalimbali za uzalishaji ambazo zitaenda kuleta athari chanya kijamii lakini pia kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, Watanzania tuna kila sababu ya kumuunga mkono Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan. Watanzania tumuunge mkono Mheshimiwa Rais kwa vitendo na vitendo hivyo ni kwa kila mmoja kutimiza wajibu wake; tufanye kazi kwa bidiii, tutimize wajibu wetu tunaopewa kwenye dhamana tulizokuwa nazo. Viongozi wote wa kila ngazi tuwahudumie wananchi, tumuunge mkono Mheshimiwa Rais kwa kuwahudumia wananchi. Nchi hii itajengwa na sisi wote. Hapo pia wananchi tuna wajibu wa kutimiza majukumu yetu kama raia wema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kuishukuru sana benki ya AfDB (African Development Bank) kwa mchango wake katika mafanikio haya. Naomba sana nichukue nafasi hii kuendelea kuwaomba sana benki ya AfDB iendelee kutoa ushirikiano mkubwa sana kwa Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan, kwa sababu dunia nzima imethibitisha kwamba fedha tunazozipata sisi kama Tanzania tunahakikisha zinaenda kwenye maendeleo ya watu. (Makofi/Vigelelegele)

Mheshimiwa Spika, sisi wote ni mashahidi kwamba Serikali ya Awamu ya Sita, Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan inasimamia matumizi bora ya rasilimali za Taifa, inasimamia na inapinga ufisadi na inasimamia utawala bora. Kwa hiyo tunaomba sana wadau mbalimbali waendelee kumuunga mkono Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ili aweze kuendeleza yale aliyoyaanza kwa kasi kubwa sana na sisi Watanzania tuendelee kuwa na imani naye, tuendelee kumwombea, naamini Mungu ataibariki Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, naafiki.